12/30/2005

Hukujua Kuwa Michuzi Anaimba Sauti ya Nne?

Michuzi sio tu ana ujuzi wa kupiga picha bali pia ni mwimbaji mashuhuri sana hasa akiwa nchi za nje. Katika picha hii Watanzania tuliokuwa katika mkutano kuhusu utandawizi na demokrasia katika jiji la Helsinki, Ufini mwezi Septemba, tunatumbuiza. Siku hii ilikuwa ndio mwisho wa mkutano. Tukiwa katika tamasha la kuaga wana mkutano, Mama Maria Shaba ghafla alitufuata mimi na Michuzi nje. "Watanzania lazima tuwakilishe."
Nikamuuliza, "Tuwakilishe vipi?"
Akasema, "Toka tuje wanaoimba na kutumbuiza ni Wafini, kwani sisi hatuna sauti? Lazima tukaimbe."

Basi akatukusanya Watanzania mmoja mmoja. Hakuna kukataa. Hao jukwaani. Mnajua tuliimba wimbo gani? Buni....tuliimba Malaika. Michuzi akiwa ndio sauti ya nne. Katika picha unamuona Mama Shaba akiwa ameshika kipaza sauti. Pia unaweza kumuona Mama Mwingira wa Tango kushoto kwa Maria Shaba. Mimi nadhani nilikuwa naimba sauti ya 60! Baada ya kumaliza wimbo wa Malaika, tuliaga jukwaa, huku tukishangiliwa kwa nguvu, kwa wimbo wa Bob Marley: Get Up, Stand Up. Wimbo huu ndio wimbo rasmi wa shirika la kutetea haki za binadamu la Amnesty International.
Ili uione picha kwa uzuri zaidi bonyeza juu ya picha yenyewe (peleka mkono wa kipanya cha tarakilishi yako).

Kikosi Kamili Chini ya Kocha Fide Pale Helsinki


Sio muda mrefu nimemaliza kuonga na Jeff Msangi ambaye alikuwa akimzungusha mjini Toronto Boniphace Makene. Katika maongezi yetu tuligusia umuhimu wa kuanza kupanua matumizi ya blogu zetu kwa kuweka picha pale panapofaa na hata kuingilia blogu za sauti na video. Wakati wake utafika.

Baada ya kuongea na Jeff kuhusu picha nikatembelea kamera ya Michuzi nikakuta amewaka picha ambayo imenikumbusha picha ambazo nilisahau kabisa kuziweka kwenye blogu. Bonyeza hapa uone picha aliyotupiga Michuzi nikiwa na mzee mwenyewe Mti Mkubwa (ambaye amebatizwa jina jipya: Mti Mkubwa Mkavu). Basi ndipo nikaanza kuchimba picha nilizonazo toka Helsinki.

Nimeweka picha ya kikosi kamili cha Watanzania wanaoishi Helsinki na wale ambao tulikuwa tuko ziarani hapo. Utamuona Michuzi mwenyewe na Mti Mkubwa Mkavu wakitabasamu. Picha hii ilipigwa na rafiki yangu, Vikii wa jarida la mtandaoni la nchini Malaysia, Malaysiakini. Hapa tulipokuwa ni eneo la kujidai la Watanzania wanaoishi jijini hapo (Fide: klabu ile inaitwa nini tena?).
Ukitaka kuiona picha hii vizuri, peleka mkono wa kipanya chako juu ya picha kisha bonyeza.
**Nyongeza:
Ametokea mtu akaweka majina ya walioko kwenye picha hii kwenye sehemu ya maoni. Pia jina la klabu yenyewe, Chelsea Sports Pub. Majina ya walioko kwenye picha haya hapa:
Pichani kutoka kushoto ni Lwitiko Mwalukasa, Benard Kakengi, Mapinduzi Mwankemwa, Mzee Kimaro, ? , Raymond Mutafungwa, ? , Dennis Londo, Muhidin Issa Michuzi, F MtiMkubwa Tungaraza, Ndesanjo Macha, Magonera Malima, na Kisakisa Kiwara. Picha ilipigwa ndani ya Sports Pub Chelsea. Ukifika Helsinki usiwe na wasiwasi wa kuwapata Watanzania fika Chelsea Sports Pub utawakuta wakinywa na kusogoa masuala mbali mbali ya kijamii, kisiasa, na kiuchumi.

Unaifahamu Afrika Kwa Kiasi Gani?

Mmoja wa waanzilishi wa Mradi wa Sauti za Dunia, Ethan Zuckerman, ameaandaa ka-mtihani kadogo kuhusu Afrika. Jaribu kufanya mtihani huo uone unafuatilia masuala ya Afrika kwa kiasi gani. Nimekosa swali moja kwa ujinga! Tena swali lenyewe linahusu jambo ambalo ninalifuatilia kwa karibu sana, matumizi ya simu za mkono Afrika. Bonyeza hapa ujaribu bahati yako. Kisha bonyeza hapa usome aliyoandika kuhusu ka-mtihaki hako na maoni ya waliojaribu. Iwapo hutaki "kuibia" nakushauri ufanye mtihani wenyewe kabla ya kusoma maoni ya watu maana pale utapata baadhi ya majibu. Ukifanya hivyo utakuwa unajidanganya mwenyewe. Ukipata F tuambiane!
Huko nyuma niliwahi kutoa jaribio jingine lilloandaliwa na mradi wa SchoolNet. Jaribio lao, kama ambavyo utaona, linakupa nafasi ya kuchagua unataka maswali magumu au mepesimepesi. Kama umetoka Afrika, chagua maswali magumu kabisa. Chini ya ramani utakayoiona ukibonyeza kiungo nitakachokupa ndio kuna sehemu ya kuchagua kama unataka mteremko au la. Bonyeza hapa ujaribu. Kama umepata sifuri tuambie usifiche!


12/29/2005

Isikilize Sauti ya Baragumu

Zamani kulikuwa na gazeti Tanzania lililoitwa Baragumu (labda limefufuka tena, sijui). Baragumu ninayozungumzia sio hilo gazeti bali ni blogu mpya ya ndugu yetu ambaye alikuwa mwanablogu hata kabla hajawa na blogu yake mwenyewe kutokana na ushiriki wake kupitia maoni yake katika blogu mbalimbali. Huyu ni ndugu Mwaipopo anayeblogu toka Alabama. Bonyeza hapa ukamsabahi.

12/26/2005

Kumbe Kaka Pori naye anablogu?

Jua ndio linachomoza kwenye uwanja wa blogu za Kiswahili (huku tukiwa bado tunatafuta neno muafaka la chombo au uwanja huu...Da Mija ameweka kiungo cha uwanja wa kuendesha mjadala huu). Napenda kumtangaza mwanablogu mpya, Kaka Pori. Kwa maneno yake mwenyewe anasema kuwa lengo la blogu yake ni:
"Tumetawaliwa kiakili kiasi kwamba tumesahau kabisa sisi ni akina nani. Sasa basi, kwa kupitia blogu hii, tutaamshana, kukumbushana na kupeana hamasa ya kujitambua kwa kupeana habari chanya na mawazo jengevu. Ili tuweze kujenga jamii chanya, tunahitaji umoja, mshikamano, kujielewa na kuelewana, kuhabarishana, n.k. Nipo nanyi nyote na ninaomba kujiunga nanyi."
Bonyeza hapa umtembelee na kumkaribisha. Utamaduni wa kukaribishana ni mzuri sana na ninaombe tuuendeleze.
Kiungo nilichoongelea hapo juu cha kibanda cha kubunga bongo kuhusu neno muafaka la blogu utakipata ukibonyeza hapa.

12/23/2005

Mbona Kasheshe Bloguni?

Majuzi nilikuwa nafanya mahojiano kuhusu blogu zetu za Kiswahili. Jambo moja ambalo nilisema kuwa napenda kuona likitokea ni kuwepo kwa blogu za watu wenye fikra mbalimbali zinazotofautiana. Kujadiliana na watu wanaofikiri kama wewe ni sawa ila unaweza usikue kifikra na pia usipate changamoto ya kuhoji fikra zako mwenyewe na kutafuta maarifa zaidi. Sio vyema tukiwa na blogu za watu wote wanaokubaliana. Kwahiyo nchi kama Irani (ambayo ina blogu zaidi ya laki moja) na Marekani ambapo zipo blogu za wananchi wenye fikra za mrengo wa kushoto, katikati, kulia, n.k. Hapo utakuta mawazo ya watu wanaotetea mfumo na mambo yalivyo hivi sasa na blogu zenye kunyooshea kidole mfumo wa utawala, utamaduni, elimu, n.k. Utakuta pia blogu za vichekesho na kejeli, blogu za fasihi, n.k. Pia unakuta zipo blogu za picha, za video, za sauti (podikasiti), n.k. Unaweza pia kuona kuna blogu nyingine za kufundishia, za kutangazia biashara, za wasafiri, wanamichezo, n.k.
Chemi Che Mponda alipoandika juu ya matako makubwa nikaona kuwa huenda huo ndio mwanzo wa blogu zinazozungumzia masuala ambayo hatupendi kuyazungumzia hadharani. Bonyeza hapa usome. Ndugu Swai naye alianzisha blogu yake akawa anaandika masuala kwa staili yake na masuala ambayo wanablogu wengine hatuandiki. Lakini amekuwa kimya kwa muda. Bonyeza hapa uone blogu yake.
Sasa amekuja mwanablogu wa picha ambaye bado sijamuelewa hasa mwelekeo au nia yake. Pia hajaandika jina lake na anasema anaishi "cybercity." Yaani mji wake uko kwenye mtandao wa kompyuta. Utaona kuwa huyu bwana ni mtu wa utani sana. Hii ni staili nyingine ya blogu (naamini kuwa waliopigwa picha wametoa ruhusu picha zao kutumia. Katika mwongozo mpya wa wanablogu wapya ninaoandika, ninazungumzia masuala ya kisheria kuhusu blogu zetu hizi. Nitagusia kuhusu matumizi ya picha) ya picha tofauti na ile blogu ya kwanza ya picha ya Issa Michuzi. Itazame hapa.
Huyu bwana nimeanza kuhisi kuwa ni nani. Ila kwakuwa hajapenda kujitangaza jina sio vizuri kumtaja hata kama unamfahamu. Katika mwongozo ninaoandika, ninaongelea pia kuhusu namna ya kublogu kama hutaki ujulikane kuwa wewe ni nani. Kuna mbinu za kiufundi ambazo unatakiwa kutumia maana hata usipotumia jina lako, ni rahisi mtu kujua kompyuta unayotumia na huduma za intaneti unazipata toka kwa nani. Kila kompyuta ina namba ambayo ni rahisi sana kuipata. Njia hii imetumiwa majuzi huko China kumtia jela kwa miaka 10 mwandishi wa habari wa China. Yahoo! iliisaidia serikali ya China kumtambua mwandishi huyu. Bonyeza hapa usome habari hiyo.
Bonyeza hapa umuone mwanablogu mpya wa picha.
*****************************
Ninasafiri kwa siku mbili tatu hivi kimapumziko. Nitakuwa nachungulia mtandaoni kwa chati. Nadhani jumatatu ndio nitaweza kuandika tena nikiwa nimetulia. Kama nitaandika kabla ya hapo itakuwa ni juujuu au jambo la muhimu sana.
********************************
Wakati huo huo: ninajiandaa kusherehekea sikukuu ya Kwanzaa. Sikukuu hii husherehekewa kwa kukumbuka na kuenzi nguzo saba. Bonyeza hapa uzione. Zaidi juu ya sikukuu hii baadaye. Kwa sasa bofya hapa usome kuhusu sikukuu hii.

12/21/2005

TAFAKARI YA MAISHA: Mwanablogu mwingine aingia uwanjani

Nani alisema kuwa kule Musoma hakuna wanablogu? Acha utani...yupo mwanablogu mpya wa Tafakari ya Maisha toka Musoma. Anauliza ni kitu gani cha muhimu kati ya uhai na kuvaa? Sasa kama kawaida yetu tumkaribishe. Bonyeza hapa umtembelee na kumpa maneno mawili matatu ya kishikaji.

12/20/2005

Blogu Ziitwe Ngwanga?

Mjadala huu huwa unazuka na kutokomea. Jeff ameuanzisha tena. Bonyeza hapa usome aliyoandika. Pia tazama sehemu ya maoni. Soma changamoto ya Mwaipopo (ambaye nasikia ataingia rasmi kwenye blogu hivi karibuni). Da Mija akapokea wito wa Jeff. Anapendekeza neno Ngwanga litumike badala ya neno "blogu" ambalo baadhi wanaona kuwa neno hili tumelichukua kutokana na uvivu tu. Yaani tumechukua neno la Kiingereza "blog" tukaongeza "u." Bonyeza hapa. Pia tazama maoni yaliyotolewa hapo kwa Da Mija. Unaweza kuchangia hapo kutokana na pendekezo la Da Mija.

Nafasi ya Fasihi Andishi, Simulizi katika Blogu za Kiswahili

Kama unatazama blogu za Kiswahili kwa karibu, utagundua kuwa kuna jambo moja zuri sana linajitokeza. Blogu zinakuwa sio tu eneo la kujadili masuala ya kisiasa, kiutamaduni, na kijamii bali pia ukumbi wa kutoa kazi za fasihi andishi: riwaya, tamthilia, visa, mashairi, n.k. Hili ni jambo kubwa sana. Nimelizungumzia majuzi kwenye muhtasari niliouandika kwenye blogu ya Sauti za Dunia. Bonyeza hapa uusome. Katika muhtasari huo nilisema hivi (kwa Kiingereza):

It is a common practice among Swahili poets to challenge each other using various poetry techniques and deep Swahili. For example, one poet writes a poem and another poet responds to that poem through a poem of his/her own. This practice has long been associated with Uhuru, the only Tanzanian newspaper that for many years provided a space for Swahili poets to publish their work. Two poet bloggers, Kasri la Mwanazuo and Fasihi za Ufasaha are moving this practice to cyberspace through their blogs.

This is a particularly interesting moment in the Kiswahili blogosphere. The possibility that blogging can become one of the ways in which Tanzanian writers and poets can bypass problems related to cost of publication and economics of distribution is an exciting one. For example, because of limited distribution, Swahili novels are mostly read in Tanzania and Kenya. If Swahili literary works are available online in digital format, making them globally accessible, Swahili speakers in Oman, India, the US, China, Mexico, South Africa and elsewhere will be able to read them. Utilizing this opportunity,
Kasri la Mwanazuo is planning on releasing his first novel on his blog.
Utaona kuwa katika muhtasari huo ninasema kuwa kazi za fasihi andishi hata fasihi simulizi za Kiswahili (tukianza kutumia blogu za sauti [podikasiti]) ambazo kawaida husomwa Afrika Mashariki tu (hasa nchi mbili, Kenya na Tanzania) zinaweza kuanza kusomwa na wasomaji zaidi ya milioni 100 wa Kiswahili ambao wametapakaa sehemu mbalimbali duniani. Kwa kuwa mzungumza Kiswahili anayependa fasihi ya Kiswahili anayeishi India au Oman hawezi kununua vitabu vilivyoko pale TPH, mtaa wa Samora, kazi hizi za fasihi zikipatikana katika mtandao wa Intaneti (kupitia blogu, podikasiti, fasihi pepe, n.k.) mtu huyo ataweza kujisomea. Kwa maana hiyo fasihi ya Kiswahili haitakuwa ni fasihi ya kikanda bali ya dunia. Tunajua kuwa wachapishaji wetu wanakabiliwa na tatizo la mtaji wa kuweza kusambaza kazi za Kiswahili duniani.
Jambo jingine ni kuwa kuna watu wengi ambao ni watunzi wazuri sana wa riwaya, mashairi, au tamthilia lakini kutokana na gharama kubwa za kuchapa vitabu, kazi zao zinabaki kwenye shajara au madafatari yao binafsi. Wanazisoma wenyewe. Teknolojia ya blogu inaweza kusaidia, kwa kiasi fulani, baadhi ya watunzi hawa kwa kuwapa eneo la kuchapa kazi zao kwenye mtandao wa Intaneti. Hata kama mtunzi mwenyewe hana utaalamu wa masuala ya kompyuta anaweza kutumia ndugu au marafiki au wakereketwa ili waweke kazi zake mtandaoni.
Upo pia uwezekano wa kazi za fasihi zilizotolewa mtandaoni kutolewa katika muundo wa vitabu kwa ajili ya wasomaji wasio na mtandao wa Intaneti au wanaotaka kusoma kazi hizo katika vitabu. Kwa mfano, mwablogu Salam Pax wa Iraki amechapisha yaliyoko kwenye blogu yake kwenye kitabu ambacho kimepata umaarufu sana. Bonyeza hapa uone kitabu chake na hapa ili usome habari zake.
Kama ulifuatilia tuzo, ambayo niliitangaza hapa, ya blogu duniani utakumbuka kuwa aliyeshinda (ukiacha blogu ya Sauti za Dunia ambayo ilishinda kwa upande wa Kiingereza) kwa blogu za lugha zote zilizoshiriki ni blogu ya kifasihi ya Kihispania ambayo inaelezea maisha ya familia moja. Blogu hiyo inaitwa, Heshima Kidogo, Mimi ni Mama Yako. Bonyeza hapa uone tangazo la kushinda kwake. Bonyeza hapa uone blogu yenyewe.
Kwahiyo kama mnafahamu watunzi ambao wanatafuta njia ya kuweka kazi zao mikononi mwa wasomaji ila hawana namna, waelezeni kuwa blogu ni moja ya njia ambazo hazihitaji gharama kubwa. Sio mwanzo na mwisho ila ni moja ya upenyo.
Ninawaombeni pia mufuatilie kazi zilizopo hivi sasa mtandaoni za fasihi. Majuzi nilimtangaza mwanablogu mshairi Ustaadh, Rashid Mkwinda(ngominenga)(Malenga wa Kilwa). Nikamrushia dongo mshairi mwingine, Makene, kuwa akae chonjo. Bonyeza hapa usome tangazo hilo. Makene, mzee wa Kasri la Mwanzuo, akajibu kwa mashairi mawili ya haraka haraka katika sehemu ya maoni. Nami nikaweka shairi fupi la Ustaadh Mkwinda jibu kwa Makene na mimi. Bonyeza hapa usome mashairi hayo. Makene hakuishia hapo, akakaa chini na kumkaribisha Mkwinda kwa shairi. Bofya hapa usome shairi hilo. Mkwinda naye akamwandikia Makene. Bofya hapa na pia tazama sehemu ya maoni kwa mashairi la Makene. Mkwinda akaandika pia shairi jingine kwa Makene na mimi. Bofya hapa. Nadhani nitamjibu Mkwinda kwa Kichagga!
Mkwinda kaandika shairi, baada ya mchezo wa kuigiza wa uchaguzi Tanzania, akiuliza kama ulikuwa ni uchaguzi au uchakuzi. Lisome hapa. Makene kabla hajaondoka kwenye Kanada aliandika shairi la salamu kwa wanablogu wa Kiswahili. Bofya hapa ulione. Kinachotokea katika mashairi haya ya nipe nikupe ni sawa na hali ambayo imekuwepo kwa miaka mingi katika ukurasa wa mashairi wa gazeti la CCM, Uhuru. Bonyeza hapa uone ukurasa huo, Uga wa Malenga.
Huko nyuma Mwandani aliwahi kuandika mshairi kadhaa (ninatafuta viungo vyake...Tunga unavyo haraka haraka unipatie?). Ukiacha mashairi kuna kazi nyingine za kusisimua kama aliyoandika Jeff hivi karibuni. Kazi yake hii: Nyerere Yuko Wapi?, nimeipenda sana. Isome kwa kubonyeza hapa. Makene naye ana kazi yake iitwayo Safari ya Mashua. Bonyeza hapa kwa sehemu ya kwanza na hapa kwa sehemu ya pili. Jana ameandika kisa kilichomtokea ndotoni. Bofya hapa. Kasri la Mwanazuo tuliongea siku si nyingi juu ya kufungua ukurasa wa Fasihi Pepe za Kiswahili (Makene, sijasahau nilichokuahidi!).
Kwangu mimi mambo haya ni kile kitu ninachopenda kuita, "ishara ndogo za mambo makubwa." Hizi ni ishara ndogo za mambo makubwa yanayokuja mbeleni. Ninatazama mambo haya ninatabasamu. Tunafanya jambo moja kubwa sana bila wenyewe kujua. Au pengine tunajua...

12/17/2005

Samaki Mkunje Angali...
















Samaki jamani lazima umkunje mapema mapema. Ndio anavyokunjwa mwanamapinduzi wa kesho, Ukweli Ndesanjo, kama unavyomuona hapo kwenye picha ya juu. Hiyo ilikuwa ni Oktoba mwaka huu wakati wa maandamano ya Vuguvugu la Mamilioni na Zaidi. Hapo anamtazana na kumshangilia mwanamuziki aliyehamia Marekani toka Haiti, Jean Wycleaf. Picha ya chini yakea ndio Wycleaf mwenyewe anaonekana kwenye luninga (iliyokuwa ikirusha matangazo kwa walioko mbali na jukwaa kuu). Ingawa anamshangilia Wycleaf kwa furaha, Ukweli anawapenda zaidi Fela Kuti na Bob Marley. Masikini, hatakaa awaone wakitumbuiza hadharani.

Tuko Tayari Dakika Hii...


Naendelea kuweka picha zaidi nilizopiga wakati wa maandamano ya Vuguvugu la Watu Milioni na Zaidi kule Washington, DC, Oktoba mwaka huu. Hawa ni wanachama wa kundi la New Black Panther Party (tofauti na lile kundi la wazee wengine wa shoka la Black Panther). Hapa unaona mwenyewe wanaume wa shoka wako tayari tayari kwa lolote lile. Joji Kichaka, we endelea kuleta za kuleta...

Picha hiyo hapo chini ndio kiongozi wao, Malik Zulu Shabazz. Huyu bwana analindwa na utitiri wa wanaume wa shoka sijapata kuona. Bonyeza hapa usome kwa kifupi juu yao.



12/16/2005

Wanaume wa shoka....















Wanaume hawa wa shoka ni akina nani? Hawa ni walinzi wa kiongozi wa kundi la New Black Panther Party, Malik Zulu Shabazz. Malik ambaye ni mwanasheria ni machachari sana kwa siasa zake kali ziilizojengwa juu ya falsafa za akina Malcolm X, Marcus Garvey, Kwame Toure, n.k. Malik Zulu Shabazz ndiye aliyeko mbele katika picha hii. Picha hii niliipiga siku ya maandamano ya Vuguvugu la Watu Zaidi ya Milioni, Washington, DC.

Kanye West na Joji Kichaka















Hii picha niliipiga wakati wa maandamano ya Vuguvugu la Mamilioni na Zaidi kule Washington, DC. Kama unakumbuka, mwimbaji Kanye West alipokuwa akitumbuiza kwenye tamasha kwa ajili ya waliathirika na Katrina alisema kuwa Joji Kichaka hana habari na watu weusi. Swali kwenye picha hiyo linatokana na kauli hiyo ya Kanye West.

12/14/2005

Kurunzi la Ndugu Mark Hiloooo: Blogu Mpya!

Mark Msaki ni mwanafunzi wa udakitari katika chuo kikuu cha Kwa Zulu Natal kule Afrika Kusini. Amesema kuwa ingawa yeye sio mwandishi wa habari, ana nasaha na maoni ambayo anapenda kuyatoa hadharani. Na chombo ambacho anamependa kukitumia kufanya hilo ni blogu. Kaanzisha blogu yake ambayo ameiita Kurunzi. Bonyeza hapa usome na kumkaribisha.

12/13/2005

Waulizeni Kituo cha Haki za Binadamu, hao "binadamu" ni akina nani?

Majuzi niliandika kuhusu Tuzo ya Haki za Binadamu ya Majimaji aliyopewa Jaji James Mwalusanya. Kama hukusoma niliyoandika, bonyeza hapa usome. Tuzo hiyo ilitolewa na Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu. Niliwapongeza kwa kumpa Jaji Mwalusanya tuzo hiyo kutokana na mchango wake katika ujenzi wa demokrasia Tanzania kupitia maandiko yake na hukumu mbalimbali ambazo amewahi kutoa.
Lakini nikawanyooshea kidole wanaharakati hawa wa Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kwa kosa ambalo linatokana na ugonjwa ambao inaelekea ni mbaya kuliko ambavyo wengi tunadhani. Ugonjwa huu ni ule unaotufanya kutumia lugha ya kiingereza hata pale ambapo walengwa wetu lugha yao kuu ni Kiswahili. Tazama majina ya mashirika yasio ya kiserikali, vyama vya upinzani, kampuni za kibiashara, maduka, baa, bendi, na hata vikundi vya utamaduni. Utakuta majina ya kiingereza ndio yanaonekana kuwa ni bora zaidi.
Achilia mbali majina, tuje kwenye tovuti. Nimeongelea kwa muda mrefu kuhusu tovuti ya ikulu, waziri mkuu, bunge, tume ya uchaguzi, mwanablogu mmoja (sijui alikuwa ni Nkya au Egidio) akatukumbusha pia tovuti ya Makumbusho ya Taifa, n.k zina taarifa muhimu kwa Watanzania kwa lugha ya kiingereza. Niliwahi kusema kuwa iwapo Rais akiongea na Watanzania anatumia kiingereza basi sitalalamika iwapo tovuti ya ikulu ni ya kiingereza. Iwapo wabunge ni wawakilishi wa wananchi ambao lugha wanayotumia asubuhi, mchana, na jioni ni Kiswahili, kwanini tovuti ya bunge lao na miswada ya sheria iwe ni ya kiingereza? Kama huu sio ugonjwa ni nini?
Sasa nilipokuwa naongelea kuhusu Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu, nikauliza: kuna sababu gani ya tovuti ya kituo hiki kuwa ya kiingereza wakati ambapo wanatuambia kuwa lengo lao kuu ni kuwawezesha Watanzania wasiojiweza kiuchumi, kijamii, kiutamaduni, na kiroho kwa kuwapa mafunzo ya haki za binadamu na kuwapatia msaada wa kisheria? Kama nia ya kituo hiki ni kuwasaidia hao Watanzania, kwanini watumie lugha ya watu wengine na sio lugha wanayotumia Watanzania masaa 24?
Soma mwenye lengo kuu la kituo hiki (kwa kiingereza). Nimetoa kwenye tovuti yao (wino mzito nimeuweka mwenyewe):
The primary task of the Legal and Human Rights Centre is to create legal and human rights empowerment amongst the socially, economically, culturally and spiritually disadvantaged and marginalized groups within the Tanzania society through legal and human rights training, provision of legal aid, information generation and dissemination through publications and radio programmes, research on legal and human rights issues and networking and alliance building with other institutions which share this mission.
Nilipoandika kuhusu hili, mwanablogu Jeff, akatoa maoni yake akitaka kujua kama "binadamu" wanaozungumziwa na kituo hiki ni pamoja na babu na bibi yake kule Kilimanjaro. Alisema, "Huenda wanadamu wanaoongelewa hapa sio babu yangu na bibi yangu kule Kilimanjaro."Wanadamu" hawa nadhani ni wale ambao tayari wanazijua baadhi ya haki zao za msingi.Kituo kinafanya kuwakumbusha tu pale wanapoonekana kuzisahau."
Mwanablogu Da Mija akatoa wazo: "Mimi naona tuanze kuwaandikia moja kwa moja kuwauliza kwanini wanatumia kiingereza kuwaandikia waswahili, je wanajua madhara yake?"
Suala hili la lugha wengine wanaweza kuona kuwa ni jambo dogo sana. Hapana. Kama ambavyo tovuti ya shirika lisilo la kiserikali Uingereza haitakuwa ya Kiswahili maana hawatumii lugha hii ndivyo hivyo tunaamini kuwa tovuti ambayo inatoa taarifa, elimu, na maarifa kwa Watanzania haina haja ya kuwa ya kiingereza. Hili ni suala la kujikwamua. Kama tovuti hizi zinatengenezwa kwa ajili ya wafadhili, tuambiwe. Ila kama zinatengezwa kwa ajili ya kutoa taarifa na elimu kwa Watanzania, basi hakuna sababu ya kukopa lugha ambayo wengi tunaielewa kijuujuu. Ukitaka kujua lugha gani uitumie unapotaka kutawanya habari, taarifa, elimu, n.k. kwa Watanzania, nenda kwenye vituo vya mabasi, uwanja wa mpira, baa, saluni, vijiwe vya kahawa, mashambani, kampeni za kisiasa, n.k., tazama Watanzania wanatumia lugha gani sehemu hizo.
Kama Da Mija alivyosema, tunapaswa kuwaambia Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu kuwa ni busara na heshima kwa taifa na utamaduni kujenga tovuti yao kwa Kiswahili. Haki za binadamu wanazotetea zinajumuisha pia haki za kitamaduni. Haki za kuwa na utamaduni wako, kuujua, na kuuheshimu.
Bonyeza hapa uone tovuti yao. Anuani yao ya barua pepe ni hii: lhrc@humanrights.or.tz
Na simu yao ni hii: 2773038, 277 3048

Bonyeza hapa usome moja ya makala zilizowahi kuandika kuhusu suala la kimombo kwenye tovuti za umma.

Mkutano wa wanablogu, changamoto, tufanye nini?

Mkutano wenyewe ulifanyika tarehe 10 Desemba. Wanablogu toka pande mbalimbali za dunia walikutana katika makao makuu ya shirika la habari la Reuters (wakiwemo Paul Kihwelo wa kitivo cha sheria Chuo Kikuu Huria Tanzania, ambaye blogu yake itakuwa hewani karibuni na Fatma Karama). Mambo kadhaa yalijitokeza ambayo yanatuhusu wanablogu wa Kiswahili. Mawili makuu: 1. Jinsi gani ya kuongeza idadi ya blogu? 2. Je mradi wa Sauti za Dunia ufanye nini kuhusu blogu ambazo sio za kiingereza?
Ningependa tutazame hayo masuala mawili na kujadiliana kitu/mambo gani tunaweza kufanya. Tayari nimejadiliana kwa kifupi na Jeff na Paul. Mawazo yetu wote yanahitajika. Jambo mojawapo ambalo Jeff nami tumeligusia ni kuwa tunaweza kupeana changamoto: kila mwanablogu alete wanablogu wawili wapya...wawili tu...kwenye blogu za Kiswahili. Paul Kihwelo amezungumzia umuhimu wa sisi kukutana. Alizungumzia jambo hili kwa kirefu alipokutana na Ethan Zuckerman, mmoja wa waanzilishi wa Sauti za Dunia. Na anaporudi Tanzania atalifanyia kazi.
Wakati huo huo kuna "wiki" ambayo imeundwa kwa ajili ya kubunga bongo na kukusanya mawazo kuhusu nini cha kufanya ili kuimarisha mradi wa Sauti za Dunia na kupanua wigo wa blogu duniani. Unaweza kuchangia mawazo yako. Kuhusu suala la lugha na tafsiri bonyeza hapa. Kuhusu suala la kuongeza na kuvutia watu zaidi katika ulimwengu wa blogu, bonyeza hapa. Ukitaka kuona "wiki" nzima bonyeza hapa.
**Wiki: wiki ni aina ya teknolojia ambayo inaruhusu ukurasa wa kwenye tovuti kuhaririwa au kuandikwa na mtu yeyote bila haja ya kuwa na neno la siri au ufahamu wa lugha ya kompyuta kama "html." Teknolojia hii ndio tunayotumia katika kutengeneza kamusi elezo ya Kiswahili. Ukibonyeza hapa utaiona kamusi hiyo na unaweza kushiriki kuiandika. Pia kwa wale ambao nimewahi kuwagusia kuhusu mradi ule ninaosimamia wa kuandika katiba kwa kutumia "wiki," basi teknolojia yenyewe ni kama hii.
Rebecca MacKinnon, mmoja wa waanzilishi wa mradi wa Sauti za Dunia, ameandika muhtasari mzuri sana wa mkutano huo wa wanablogu. Tafadhali ukiwa na muda usome ili tusije kupitwa na mazungumzo yanayoendelea duniani kuhusu blogu. Bofya hapa usome muhtasari huo.

Na Huyu ndiye Kenyan Pundit


Na huyu ndiye mwanablogu Ory wa blogu ya Kenyan Pundit akiwa kwenye mkutano wa wanablogu uliomalizika mwishoni mwa wiki nchini Uingereza. Ory ni kati ya wanablogu ambao kupitia blogu zao wanilitia hamasa ya kuanza kublogu. Moja ya kazi kubwa ambayo ameifanya karibuni kupitia blogu yake ni kuripoti zoezi la kura ya maoni ya katiba mpya nchini Kenya.
Ukitaka picha hiyo iwe kubwa zaidi, bonyeza juu yake.

"Uhuru" wa Tanzania na kichefuchefu cha Wimbo wa Taifa

Fide alituma ujumbe wa barua pepe kwa watu kadhaa hivi karibuni akihoji mantiki ya kumtaka Mola awabariki viongozi wa Afrika. Nilipenda sana ujumbe wake ule nikaufanya kuwa ni sehemu ya makala yangu ya jumapili iliyopita katika gazeti la Mwananchi, nchini Tanzania. Katika makala ile nilijadili kwa kifupi sana jambo ambalo msomaji na rafiki yangu, Frank Massawe, ameuliza hapa kwenye blogu. Katika makala hiyo nimegusia pia tukio tulilofanya jeshini (mwanablogu Nkya akiwemo) la kuchora mstari ardhini na kutamka afande mmoja pale Ruvu aruke huo mstari kama ni mwanaume!
Ninaiweka makala hiyo hapa na pia katika kona ya makala zangu, upande wa kuume wa blogu hii, chini ya picha yangu. Bonyeza hapa uisome.

Waacheni Wenye Lugha Yao!

Hii inanikumbusha enzi zile nikisoma gazeti la Uhuru.
Majuzi nilitangaza kuwa kuna mwanablogu mpya aliyekuja kwa nguvu na kutishia wale wote wanaotaka kujichukulia cheo cha u-malenga. Nikampiga dongo Kasri La Mwanazuo. Kama hukusoma tangazo hilo lisome kwa kubofya hapa.
Basi Kasri hakusita, akarudisha dongo kwangu na Mkwinda kwa shairi hili hapo chini:
Ndesanjo acha udhia, kidole ninyooshea
Gange umemgusia, vitisho kumtupia
Kasri limechimbia, mizizi imarishia
Itakuwa songombingo, kutaka libomolea.
Wazo la kulijengea, asili mbali anzia
Nikali bado tambua, Baba Mama ungania
Pumzi ilinambia, Kasri kwenda jengea,
Itakuwa songombingo, kutaka libomolea.
Mkwinda mwana fikia, Kasirini jifunzia
Fikira kutafunia, Fasihi kufahasia
Kisha weledi jazia, gange bora patilia
Itakuwa songombingo, Kasri libomolea.
Ndesanjo nanyamazia, karatasi kushikia
Kesho napaswa ketia, mtihani kufanyia
Nikisha kumalizia, Mkwinda ntamchapia
Kasri jumba la ghali, kicheko kubomolea!
*********************************************
Hakuishia hapo. Baada ya kuona Mkwinda kawa kimya akafyatua shairi jingine:
Sina ajizi fyatua, bomu nilolizindua
Awali nilidhania, muda bado kufikia
Kumbe mwanichungulia, kwa lengo kunilipua
Nataja hali hatari, Kasri kulilindia.
Ugaidi sikujua, waweza kunifikia
Hima sipendi jutia, tahadhali naanzia
Ijapo sitasemea, Walinzi naandalia
Hii ni hali hatari, Kasirini sogelea.
Nilisema nakimbia, kurasa kutazamia
Bado sijamalizia, ni mbili zilobakia
Moja itashika tama, leo napoifutia
Nikirudi hadithia, Kasri mtazamia.
Mkwinda u wapi kaka, utata umezulia
Umechupa kwa haraka, kisa watu nitishia
Tambua sijatishika, cheche ninakutemea
Kama wataka ingia, balaghashia vulia.
********************************************************
Mkwinda akasema isiwe tabu. Akaandika shairi fupi akitutisha kwa kalamu yake (mimi na Makene). Hili hapa:
Ya mja ada unene, nimepata makene,
Katu si vyema ujivune,kauli pasi mapene,
Kalamu iwe ni nene,andiko lionekane,
Ndesanjo nawe makene, kalamu vyema tumieni.
******************************
Mtembee Kasri la Mwanazuo kwa kubonyeza hapa na bofya hapa umtembelee Mkwinda.

12/10/2005

Mwanablogu Mpya: Malenga na Wataalamu wa Kiswahili Kaeni Chonjo!

Kasri la Mwanazuo kaa chonjo. Rashidi Mkwinda ni mwanablogu mpya wa Kiswahili ambaye anapenda sana lugha ya Kiswahili. Na pia ni mshairi anayependa kujibu wasomaji wake kwa mashairi. Tazama shairi lake hili:

Kilo chako ndicho, hicho sitarijie kisicho,
Katu sikodoe macho,ukadhani ndicho hicho,
Kwa macho utamanicho, kitakutoboa macho,
Epuka njia za chocho,si maisha pochopocho.

Blogu ya Mkwinda inaitwa Fasihi za Ufasaha. Bofya hapa umtembelee na pia kumkaribisha uwanjani.

Matumizi ya Bendera Kuashiria Lugha kwenye Tovuti

Tovuti ya chama cha Chadema ilikuwa ina picha ya bendera ya Waingereza ikiashiria toleo la kiingereza la tovuti hiyo. Mwanablogu Nkya wa Pambazuko akahoji kuhusu matumizi ya bendera ya nchi nyingine kwenye tovuti ya chama cha siasa Tanzania. Bonyeza hapa usome Nkya alipoandika kuhusu bendera hiyo. Chadema wakakubaliana na Nkya na sasa wameondoa bendera hiyo.
Kuna makala inayoelezea jinsi ambavyo sio sahihi kutumia bendera katika tovuti kuashiria lugha fulani. Huyu ndugu anasema kuwa wakati mwingine tendo hili linaweza kuchukuliwa kuwa ni tusi hasa kama bendera inayotumiwa ni ile ya wakoloni. Bofya hapa usome makala hiyo.

Simu za Mkono na Intaneti Tanzania

Wakati mkutano wa wanablogu ukiendelea (bonyeza hapa kuhusu mkutano huo) katika mjadala uliokuwa ukiendelea katika ukumbi wa majadiliano kwa njia ya Intaneti (kwa kutumia "Internet Relay Chat".....kuhusu "Internet Relay Chat" bonyeza hapa. ), Angelo Ambuldeniya aliniuliza juu ya upatikanaji wa huduma za Intaneti kwa kutumia simu za mkono nchini Tanzania. Wakati huo tulikuwa tunajadili juu ya blogu za mkononi iwapo hii ni moja ya njia za kuwawezesha watu wasio na mtandao wa Intaneti (ila wana simu za mkono) kublogu. Swali kuu lilikuwa: je ni namna gani tunaweza kuongeza blogu duniani hasa katika nchi ambazo wananchi wake wengi hawana kompyuta?
Nina swali kwa wale walioko Tanzania, je kuna kampuni ngapi kwa jumla ambazo zinawezesha watumiaji wa simu zake za mkono kutembelea mtandao wa kompyuta? Gharama yake je?

Mkutano wa Wanablogu Uingereza: Blogamundo kusaidia tafsiri

Mjadala mzuri sana unaendelea hivi sasa kuhusu jinsi ya kufanya "Sauti za Dunia" kuwa kweli ni Sauti za Dunia. Suala kubwa ni kuhusu jinsi gani mradi wa Sauti ya Dunia utajumuisha lugha nyingine zaidi ya kiingereza. Je zianzishwe blogu chini ya mradi huu za lugha mbalimbali kama Kiswahili? Au kuwe na ukurasa maalum wa kutafsiri kwa lugha mbalimbali?
Pat Hall amekuwa akifikiria maswali kuhusu blogu na lugha kwa muda mrefu. Yeye na wenzake wanatengeneza programu ambayo itawezesha mambo yanayoandikwa katika blogu ya Sauti za Dunia kwa kiingereza kutafsiriwa kwa lugha nyingine. Tena unaweza utafsiri kitu toka kiingereza kwenda Kichina kisha Kiswahili! Bofya hapa uone tovuti ya mradi huo uitwao Blogamundo.
Kama nimekuacha hewani, ninazungumzia mkutano wa wanablogu unaoendelea jijini London. Bofya hapa kuhusu mkutano huo.

Kenyan Pundit anaongelea blogu za Kenya

Mjadala unaondelea hivi sasa katika mkutano huu hapa ni kuhusu jinsi ya kujenga na kuimarisha blogu za nchi mbalimbali. Mwanablogu Ory, Kenyan Pundit, amemaliza kuongelea kuhusu blogu za Kenya zinavyoshamiri. Amezungumzia makazi ya blogu za Kenya kuwa ni moja ya mafanikio ya wanablogu wa Kenya. Bofya hapa uone makazi hayo.

Blogu za Tanzania, Wowowo, na Mkutano wa Uingereza

Unajua bado siamini amini kuwa siko ndani ya jengo la Reuters nikihudhuria mkutano mkubwa kuhusu blogu. Siamini bado kuwa ndege niliyokuwa niende nayo ilikatisha safari kutokana na hali mbaya ya hewa. Kama nilitaka kung'ang'ania kwenda ingenipasa kuondoka leo na kuwasili Uingereza Jumapili (siku ambayo ndio nilikuwa niondoshe mguu toka hapo kwa Malikia Lizabeti). Huu mkono ulioleta hii nuksi, balaa, mkosi, kisirani, bahati mbaya na kadhalika lazima niutafute. Sijui niende kwa Mandondo Tanga au kwa niende Mlingotini, Bwagamoyo. Hapana, kipindi cha uchaguzi bei za Mlingotini ni kubwa sana sitaziweza. Sitaweza kushindana na pochi ya wagombea ubunge na urais.
Haya, ngoja niweke kejeli pembeni. Jeff Msangi ndiye mwanablogu pekee ambaye namuona akishiriki kwenye mkutano huu tokea Toronto, Canada kwa njia ya "Internet Relay Chat." Kaniuliza swali moja kuhusu idadi ya blogu za Watanzania. Hivi sasa kwa hesabu za haraka kuna blogu 42. Idadi hii inajumuisha blogu za Kiswahili, kiingereza, na zile za lugha zaidi ya moja. Lakini pia kuna blogu zile ambazo haziandikwi mara kwa mara. Halafu kuna blogu nne kuhusu Tanzania zinazoandikwa na Wamarekani walioko vijijini nchini Tanzania.
Chemi Che Mponda naona atazua balaa ndani ya blogu. Kaanzisha mjadala ambao najua utakuwa mtamu sana. Kaandika mada maalum kwa "wapenzi wa matako makubwa." Kanifanya nimkumbuke David Mailu, mwandishi wa Kenya ambaye vitabu vyake tukiwa wadogo tulikuwa tunavisoma huku tukijificha. Chemi anasema kuwa wowowo kubwa ni jambo la kujivunia sana na anatamani kuwa wowowo yake ingekuwa kubwa zaidi! Mija akatoa maoni akimuuliza kama ataandika juu ya matiti makubwa baada ya kuandika juu ya wowowo kubwa. Chemi anadai kuwa mada ya matiti makubwa inakuja. Bonyeza hapa umsome.

Mkutano wa Wanablogu Uingereza

Bonyeza hapa uende kwenye blogu inayotuma habari na picha moja kwa moja toka kwenye ukumbi wa mkutano katika jengo la Reuters.

Balaa Bin Mkosi!

Balaa. Mkosi. Kisirani. Bahati mbaya.
Haiwezekani. Mkono wa mtu. Kuna namna. Sio hivi hivi!!

Ni kwamba siko ndani ya ukumbi wa mkutano wa wanablogu Uingereza. Ndege niliyokuwa niondoke nayo haikuondoka kutokana na hali mbaya ya hewa. Nina huzuni kubwa. Nitaeleza zaidi hili baadaye kwani mkutano umeanza na ninaufuatilia mtandaoni. Kama hufahamu ninazungumzia mkutano gani basi bonyeza hapa utapata taarifa zote. Pia utapata taarifa jinsi ya kuhudhuria mtandaoni na kutoa maoni yako pia na jinsi ya kutazama kwa video ya mtandaoni.

Nitaandika mara kwa mara mambo yanayojadiliwa kwa wale ambao hataweza kujiunga kwa kutumia teknolojia ya IRC.

Nimepata ujumbe toka kwa mwanablogu Fatma Karama kuwa tayari yuko ukumbini hapo Uingereza. Mtanzania mwingine anayehudhuria ni Paul Kihwelo. Mshikaji Paul ni mkuu wa kitivo cha sheria katika Chuo Kikuu Huria Tanzania.

Baadaye jamani maana napitwa na mjadala.

Ukiingia IRC (kwa wanaoweza) unaweza kuingia: idhaa hii: #gvtrans
Au hii: #globalvoices

12/09/2005

Mkutano wa Wanablogu Uingereza

Jumamosi tarehe 10 ndio siku ya ule mkutano mkubwa unaokutanisha wanablogu toka pande zote za dunia. Majina ya wanablogu watakaodhuhuria unaweza kuyaona ukibofya hapa.
Nitaandika kuhusu mkutano huo moja kwa moja toka katika makao makuu ya shirika la habari la Reuters. Lakini pia unaweza kufuatilia mkutano huo kupitia video ya moja kwa moja ya mtandaoni kwa kubofya hapa. Au bonyeza hapa. Mjadala nitakaoshiriki mimi ambao utatazama maingiliano na mahusiano kati ya uandishi wa habari wa asili na blogu utakuwa ni saa tano u nusu kwa saa za London. Unaweza kujua itakuwa saa ngapi hapo ulipo kwa kubonyeza hapa. Lakini pia unaweza kushiriki kwa kuchangia mawazo kwa njia ya "Internet Relay Chat" (IRC). Kwa maelezo jinsi ya kushiriki kwa njia hii bofya hapa.
Halafu kuna kitabu cha picha ambacho kina baadhi ya picha wahudhuriaji. Bofya hapa uwaone.
Mkutano huo utakapomalizika, kwakuwa tutakuwa tumechoka, itabidi kujimwaga katika jiji la London ili kupumzisha mwili na akili. Ukitaka kufuatilia mapumziko yetu hayo bonyeza hapa.
Siku ya ijumaa baadhi ya wanablogu watakutana kwa chakula cha usiku. Kukutana huko kunafanikishwa kwa kutumia teknolojia ya "wiki." Bonyeza hapa uone.
Mkutano huu umeandaliwa na Kituo cha Intaneti na Jamii cha Berkman. Bonyeza hapa ukitaka kujua zaidi kuhusu kituo hiki. Wengi wa washiriki ni wanablogu wanaojihusisha kwa namna moja au nyingine na blogu ya Mradi wa Sauti za Dunia. Bonyeza hapa kuhusu mradi huo.

Siku ya Uhuru ni Kama Mchezo Fulani wa Kuigiza?

Fidelis Tungaraza, Mti Mkubwa, ametupa tafakari kuhusu wimbo wetu wa taifa. Msome katika waraka niliouweka katika ujumbe nilioutuma kabla ya huu. Sasa katupa ujumbe mwingine ambao umeniacha nikishika tumbo kwa kicheko. Katika ujumbe wake anaonyesha jinsi ambavyo matukio ya kitaifa yalivyo kama vile mchezo fulani wa kuigiza usio na mbele wala nyuma. Ujumbe huo hapo chini:

KAMANDA: HIMA! HIMAAA!!!

ASKARI NA CHIPUKIZI WA CHAMA: TANZANIAAAA!!!!

KAMANDA: HIMA! HIMAAA!!!

ASKARI NA CHIPUKIZI WA CHAMA: TANZANIAAA!!!

KAMANDA: GWAR'DE! HESHIMA KWA JEMEDARI MKUU WA MAJESHI NA RAIS WA SERIKALI YA JAMHURI YA MUUNGANO WA TANZANIA, NA KWA WATANZANIA WOTE, HESHIMAAAA TOA!

ASKARI NA CHIPUKIZI WA CHAMA: WAH, WAH, WAH!

INAINGIA NYIMBO YA TAIFA IKIPIGWA NA BENDI ZA JWTZ, JKT, MAGEREZA, NA POLISI.

Kama namuona Marehemu Mzee Mayagilo akiimbisha bendi ya polisi.

Mungu Ibariki Afrika
WABARIKI VIONGOZI WAKE (Hapa ndipo kilipo kiini cha mgogoro wa nyimbo hii)

Nyimbo ya taifa imekwisha sasa inakuja hotuba toka kwa Mtukufu Rais wa Jamhuri ya Muungano ambaye pia ni Jemedari Mkuu wa Majeshi na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi, Mjumbe Tume Ya Waziri Mkuu Tony Blair, Mwakilishi wa Rais Bill Clinton kwenye asasi ya UKIMWI na mambo mengine mengine. Huko mikoani wakuu wa mikoa kina Nicodemus Banduka, Athumani Kabongo na wengineo nao wanatoa hotuba zao. Baada ya hapo sikuu imekwisha tunaendelea kama jana.

Mungu Wabariki Viongozi wa Afrika! Ati Nini??

Wakati ambapo Tanzania haijawahi kutawaliwa, tunaambiwa kuwa tarehe kenda Desemba ni sikukuu ya uhuru wa Tanzania! Sasa katika kukumbuka siku hii, Mti Mkubwa (Fidelis Tungaraza), ambaye tunamfahamu kwa changamoto zake, anatupa tafakari kuhusu wimbo wetu wa taifa. Je ni kweli tunataka mungu awabariki viongozi wa Afrika kama tusemavyo tunapoimba wimbo huo? Soma aya toka kwa Fidelis. Nimezipata toka kwenye waraka pepe aliotuma kwa watu kadhaa akiwemo mwanablogu Da Mija. Nabandika hapo chini:


"Miye naupenda sana wimbo wa taifa wa Tanzania (Mungu Ibariki Afrika). Wimbo huu siye Watanzania tumeukopa toka Afrika ya Kusini. Nyimbo hii ni nzee sana ilitungwa kunako mwaka 1897 kwa hiyo una miaka takribani mia moja na kumi na moja! (111)! Muziki wa nyimbo hii ni utunzi wa Hayati Enoch Sentonga, ambapo maneno yake yalitungwa na Hayati Enoch Sentonga na baadaye yakaja kukarabatiwa na Mshairi Samuel Mqhayi. Wimbo hatujaukopa Watanzania tu na Wazambia nao na wazimbabwe hali kadhalika. Lakini sijui kwa sabau gani Wazimbabwe waliuacha wimbo na kuchukua mwingine.

Wimbo huu huwa unanipa na kunitoa raha pale unapofika kwenye mstari wa WABARIKI VIONGOZI WAKE! Ukifika hapo huwa unanikumbusha sura za viongozi walionuna wakiwa wamesimama pale mein stend, neshino stedium, huku askari wa vikosi vya ulinzi na usalama pamoja na chipukizi wa chama wakiwa wamekauka juani na saluti kali. Halafu na Watanzania wapenda amani na utulivu, wafanyakazi, wakulima na "wazururaji" wakiwa wametanda kwenye sehemu zingine za uwanja wakishiriki kwenye hiyo ghafla aidha kwa ridhaa zao au vinginevyo. Miujiza ya Tanzania Mei Dei au Saba Saba wanafunzi wa shule za msingi, sekondari na hai skuli wote wanashiriki kikamilifu!

Turudi kwenye Mungu Ibariki Afrika, hususani pale kwenye mstari wa WABARIKI VIONGOZI WAKE. Hapo nadhani ndipo Watanzania tulipopewa uwezo wa pekee wa kuweza kumtia kizunguzungu Mwenyezi MUNGU! Maanake Mwenyezi Mungu akiwatazama hao viongozi tunaomuomba awabariki Mwenyezi Mungu mwenyewe anapata kizunguzungu. Lakini dua letu siyo kama linaishia kwa viongozi wetu wa Tanzania pekee yake bali tunawaombea na majirani zetu kama Waganda wakati ule wakiwa na Idd Amin Dada, Malawi na Dr Hastings Kamuzu Banda, Zaire na Mobutu Sese Seko Kuku Mbwendu wa Zabanga, viongozi wazalendo wa Wahutu na Watutsi wa Rwanda na Burundi, kina Alphonso Dhlakama kiongozi wa Chama cha RENAMO cha Msumbiji. Dua zetu pia zilikuwa zinawaombea kina Eyadema, Omar Bongo, Paschal Lisouba, Jean Baptist Bokassa, Macias Nguema, Mfalme Hassan, Jaffar Nimeir, Omar Bashir, na Hassan Tourabi, John Voster, Tommy Ndabaningi Sithole, Abel Muzorewa, Morgan Tsivangirai, Jonas Savimbi, Gatsha Mongasuthu Buthelezi, na wengineo wote wamo kwenye dua hiyo ya WABARIKI VIONGOZI WAKE.

Kesho 09 Desemba Watanzania tutaimba tena MUNGU IBARIKI AFRIKA, WABARIKI VIONGOZI WAKE, ....Wakati tukiimba hivyo tutazame jirani yetu Kenya. Tumuombe Mwenyezi Mungu AWABARIKI VIONGOZI WAKE(kuna neno nimetaka kulisema lakini nimelimezea)."

12/08/2005

Tuzo ya Majimaji Yaenda kwa Jaji Mwalusanya

Jaji James Mwalusanya amepewa tuzo ya pekee ya Haki za Binadamu itolewayo na Kituo cha Haki za Binadamu Tanzania. Tuzo hiyo inaitwa Maji Maji Human Rights Award. Jaji Mwalusanya ni kati ya majaji ambao baadhi huwaita "majaji wanaharakati." Mwalusanya ni jaji ambaye masuala ya haki za binadamu yalikuwa yakimgusa sana na alijulikana kwa tabia yake ya kutoogopa kutoa maamuzi yanayoendana kinyume na matakwa ya serikali. Hii ndio sababu iliyokuwa ikipelekea mchungaji Christopher Mtikila kuwa na tabia ya kupeleka kesi zake Dodoma badala ya Dar Es Salaam. Jaji Mwalusanya alikuwa akifanya kazi Dodoma.
Moja ya kesi kubwa ambazo Mwalusanya aliwahi kutoa maamuzi yake ni ile ambayo alitamka kuwa hukumu ya kifo inayokubalika katika sheria za Tanzania ni kinyume na katiba na mikataba ya kimataifa ambayo Tanzania tumetia saini. Ni Mwalusanya huyu pia ambaye katika kesi iliyofunguliwa na Mtikila aliamua kuwa ni kinyume na katiba ya Tanzania kwa wananchi kutakiwa kuomba ruhusa kwa Mkuu wa Wilaya (yaani kinara wa CCM) na polisi (yaani mkono wa udhalimu wa wa-twawala) ili kufanya mkutano wa hadhara. Hukumu hiyo unaweza kuisoma kwa kubofya hapa. Ni Mwalusanya pia ambaye alitoa hukumu katika kesi nyingine ya Mtikila kuwa ni kinyume na katiba kwa Mtanzania kutumia pasipoti ili kutembelea Tanzania! (enzi zile za kutumia pasipoti kwenda Zanzibar). Pia ndiye aliyeamua kuwa ni halali na ni haki ya kikatiba kwa raia yeyote yule kugombea nafasi yoyote ya uongozi bila kuwa mwanachama wa chama chcochote. Hukumu hii iliwafanya watwawala kukimbilia bungeni kwenda kuipinga.
Pamoja na tangazo la tuzo hii na pia pongezi kwa Kituo cha Haki za Binadamu kutambua mchango wa Jaji Mwalusanya katika ujenzi wa demokrasia nchini Tanzania, ninatumia wasaa huu kuuliza swali ambalo linaweza kuwa limeshachosha baadhi yenu. Mimi halijanichosha. Kisa cha kuita tuzo hii Maji Maji Human Rights Award ni nini? Kwanini isingeitwa Tuzo ya Haki za Binadamu ya Majimaji? Au ikiitwa "award" ndio inakuwa na nguvu zaidi?
Dakika chache zilizopita nimetembelea tovuti ya Kituo cha Haki za Binadamu...kwanza jina lao hasa ni Center for Human Rights...nilitaka kutazama kama wamebadili lugha ya kigeni waliyokuwa wakiitumia. Wapi! Ugonjwa ule ule. Ukisoma malengo ya hawa wapigania haki (sijui kwanini hawapiganii haki za kitamaduni) utaona kuwa wanasema kuwa wanatetea na kuelimisha wanyonge na masikini kuhusu haki zao za msingi. Lakini wakati huo huo tovuti yao inatumia kiingereza tena cha mabomba makali makali. Wanafikiri Maimuna ataelewaje haki zake kama wanamwelimisha kwa lugha asiyoielewa? Halafu watabaki wakidai Watanzania hawajui haki zao...watazijuaje kama inabidi waende kwanza kwenye madarasa ya lugha za kigeni?
Pamoja na kuwaunga mkono katika jitihada zao za kutoa huduma za kisheria na elimu ya katiba kwa Watanzania, ningependa kuona wakitumia tovuti yao kuelimisha na kutoa msaada wa kisheria kwa Watanzania wa kawaida na sio Waingereza au Wakanada. Wafaye hivyo kwa kutumia lugha ambayo tunaitumia majumbani, mitaani, kwenye mabasi, sokoni, kwenye harusi, misiba, n.k. Lugha tunayoitumia asubuhi, mchana, jioni. Lugha hiyo ni Kiswahili.
Bofya hapa utembelee tovuti yao.

12/06/2005

Usidharau Nguvu ya Blogu Kuleta Mabadiliko

Pongeza za dhati zinamwendea mwanablogu Nkya wa Pambazuko. Hivi karibuni Nkya alitaka kujua bendera ya Uingereza inafanya nini kwenye tovuti ya Chadema? Wasomaji wake wakatoa maoni yao. Hazikupita siku mara bendera hiyo ikaondolewa. Bofya hapa usome aliyoandika na bofya hapa utazame tovuti hiyo ya Chadema bila bendera ya kule kwa Malikia Lizabeti.
Pongezi zinawaendea pia Chadema kwa kukubali mantiki na uzalendo vichukue nafasi.

12/03/2005

Nafasi ya Kazi Katika Mradi wa Sauti za Dunia

Kutokana na kupanuka kwa shughuli za mradi wa Sauti za Dunia, mradi huo umetangaza nafasi ya kazi ya mhariri mtendaji. Atakayeajiriwa kwa kazi hii hatahitajika kuhama anakoishi hivi sasa. Hii ni kazi utakayoifanya kupitia mtandao wa kompyuta. Bonyeza hapa usome wanatafuta mtu wa namna gani (kama unafahamu mtu atakayefaa unaweza kumtumia habari hii kwa kubonyeza kwenye picha ya bahasha pembeni mwa sehemu ya kutolea maoni).

Mkutano wa Wanablogu Uingereza Wiki Ijayo

Ule mkutano mkubwa wa mradi wa Sauti za Dunia unaofanyika nchini Uingereza katika makao makuu ya shirika la habari la Reuters umeiva. Nimepangwa kushiriki katika mjadala kuhusu blogu na uandishi wa habari. Bonyeza hapa kwa taarifa za kina kuhusu mkutano huo. Katika mkutano huu kutakuwa na wanablogu wawili toka Tanzania. Mwingine ni mwanablogu pekee wa Tanzania anayeishi na kusoma Uingereza ambaye unaweza kumsoma hapa. Orodha ya watu wote wanaohudhuria bonyeza hapa utaiona. Pia ukibonyeza hapa utaona sura za wanaohudhuria.
Kwa wale ambao hawahudhuria mkutano huu, unaweza kufuatilia kwa kupitia video ya mtandaoni (matangazo ya moja kwa moja). Unahitahiji kuwa na iTunes, au programu zenye mp3. Urushaji utaanza saa nne asubuhi kwa saa za London siku ya jumamosi tarehe 10. Bonyeza hapa ili uweze kujua saa hiyo ni saa ngapi hapo ulipo. Bonyeza hapa kwa anuani ya kufuatilia video ya mtandaoni ya mkutano huo moja kwa moja.
Kwa wale ambao hawatakuwepo London bado kuna uwezekano wa kushiriki katika mkutano huu kwa kupitia programu ya Internet Relay Chat (IRC). Kwa maelezo ya jinsi ya kushiriki kwa
Kumbuka pia nitablogu mkutano huo moja kwa moja kupitia hapa Jikomboe.
Kama nilivyosema hapo juu mimi nitashiriki katika mjadala kuhusu blogu na uandishi wa habari. Nabandika hapa chini maelezo ya mjadala wenyewe na watu ambao nitakuwa nimekaa nao kwenye kiti moto:
SESSION TWO 11:30-1:00
Best of both worlds
Much is made of the “blogging vs. journalism” argument. We believe there can and must be room for both in this world, and that the world will be better for having both.
Led by Rebecca MacKinnon, with input from Jeff Ooi (Malaysia), Ndesanjo Macha (Tanzania), Dina Mehta (India), Georgia Popplewell (Trinidad & Tobago), David Sasaki (Americas Editor), Onnik Krikorian (Armenia), Ben Parmann (Eurasia Blog), Lisa Goldman (Israel), and Dean Wright (Reuters)
Mkutano huu umedhaminiwa na Kituo cha Intaneti na Jamii cha Berkman cha Chuo Kikuu cha Harvard na Shirika la Habari la Reuters.

Mwanablogu Mpya: Dan, Umeishia wapi?

Dan Makundi ni mhandisi pale jijini Dasalama. Anablogu kwa kiingereza. Amekuwa kimya kidogo toka alivyoandika mara ya mwisho Novemba 8 mwaka huu. Bonyeza hapa umsome (ila tafuta kamusi kabisa kabisa!).

12/01/2005

Padri Karugengo: Mwafrika Ni Mnafiki au Mjinga?

Jana, katika barua pepe ambayo Mrisho Mpoto aliandika kwa watu kadhaa alisema kuwa Waafrika ni kama kituko vile. Tena ni wanafiki. Bonyeza hapa usome kuhusu barua hiyo kisha ndio uendelee na ujumbe wa leo toka kwa Padri Karugendo (ambaye makala zake zitarudi hapa kwenye blogu, pamoja na zangu, wiki hii).
Basi Padri Karugendo anauliza swali zuri sana. Soma waraka pepe wake aliotuma kwa watu wale wale Mrisho aliowatumia:
"Wanafiki au Wajinga. Mrisho Mpoto, anasema sisi niwanafiki, lakini mimi ninafikiri alitaka kusema sisini wajinga? Labda ninayaweka maneno haya midomonimwake, lakini ningeomba tujiulize juu ya unafiki naujinga - mnafiki na mjinga, ni nani wa kukwamisha maendeleo ya nchi yetu? Na kudai pesa mtu ili umjadili ni unafiki au ni ujinga? Mtu kuiuza nchi ni unafiki ama ni ujinga?"
Mbarikiwe,Padri Karugendo.

Siku ya "Umeme" Duniani

Leo ni siku ya Ukimwi duniani. Tunachofanya ni kutafakari kuhusu ugonjwa huu. Hivi Ukimwi ni nini? Ulitoka wapi? Mbona haukuwepo zamani? Au kama ulikuwepo mbona haukutumaliza? Je dawa yake itakujapatikana? Je kwanini hauna dawa? Au kama dawa ipo mbona wengi hatujui?

Basi katika kukumbuka hii siku, mwanablogu Sokari Ekine wa blogu ya Black Looks, ambaye pia ni mhariri wa blogu za Kusini mwa Afrika wa mradi wa Sauti Za Dunia, anachambua wanablogu walivyoikumbuka hii siku. Uchambuzi huo uko katika jarida la Pambazuka. Bonyeza hapa umsome.

Sokari Ekine mwenyewe bonyeza hapa umsome.

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com