3/29/2005

PROFESA MWANAMKE AENDESHA SALA YA KIISLAMU

Profesa Amina Wadud wa chuo kikuu cha Virginia Commoweath amegusa hisia za baadhi ya waislamu baada ya kuendesha sala ya kiislamu ndani ya kanisa na bila kutenganisha wanaume na wanawake. Ulinzi katika chuo hicho umeimairishwa kutokana na vitisho kufuatia sala hiyo. Kosa lake kubwa ni 1. kuendesha sala ya kiislamu kanisani 2. kuendesha sala wakati yeye ni mwanamke 3. kutotenganisha wanawake na wanaume. Soma habari zaidi hapa.

UNAFAHAMU "OURMEDIA.ORG"?

Tovuti hii ni muhimu sana kwa waandishi wa habari, wapiga picha, watengeneza filamu, na wale wanaotafiti maendeleo ya teknolojia ya mawasiliano na habari. Bonyeza hapa.

WANAVIITA VITA VYA KITAMADUNI...

Wanasema hivi ni vita vya kitamaduni kati ya Wafaransa na lugha ya kiingereza inayotawala katika mtandao wa tarakilishi. Soma maamuzi ya rais wa Ufaransa yaliyofanya watu wadai kuwa katangaza vita. Hapa.

3/28/2005

MAAJABU YA WACHOMEAJI WALEMAVU TANZANIA

Tanzania na bara la Afrika kwa ujumla kumejaa watu wenye vipaji na uwezo wa juu sana katika mambo mbalimbali. Tatizo ni mazingira ya kisiasa, kiuchumi, kielimu, na kijamii. Sera za kuwezesha watu wenye mitaji midogo zimebaki kwenye pambaja za midomo za watawala wa bara la Afrika. Soma habari hii ya walemavu hawa na maajabu yao ya kazi ya kuchomea vyuma. Hapa. Picha za kazi zao ziko hapa.

KWA WAPENDA SOKA

Wale wapenda soka au gozi la ng'ombe, nendeni hapa. Kuna mechi za moja kwa moja, picha, ratiba, na mengineyo. Nenda hapa usome habari za fujo za washabiki wa soka nchini Mali.

Kwanini haiwezekani?
Wananiambia kuwa haiwezekani. Kwanini?
Eti wananiambia kuwa haiwezekani ukawa hauko CCM na ukawa hauko upande wa upinzani.
Haiwezekani. Lazima uwe na upande. Lazima uwe kushoto au kulia. Ukiikosoa CCM wanakuja juu na kusema, "Wewe unashabikia upinzani." Ukikosoa upinzani wanakuja juu, "Umetumwa na CCM." Ukikosoa upinzani na CCM kwa pamoja wabaki mdomo wazi. Wanasema, "Haiwezekani!"

Jambo gani gumu kuelewa? Nawauliza.
Kwani ni kosa kutokuwa upande wowote? Naendelea kuwauliza.

Wananiambia lazima nichague shetani mwenye afadhali. Lazima nitafute mwivi na muongo mwenye afadhali. Lazima nichague shetani mmoja kati ya wawili.
Kwanini kuwe na ulazima huo? Naendelea kuuliza.

Mimi sitaki shetani wa upande wa kuume wala shetani wa upande wa kushoto. Awe ni shetani mwenye afadhali au shetani asiyefaa kabisa. Sitaki muongo au mwivi bora zaidi ya mwingine.


Inawezekana.

DINI INAKUZUIA USIMJUE MUNGU WAKO

Watakujia juu, "Haiwezekani!"
Haiwezekani. Kivipi. Hawatakubali. Mishipa itawatoka. Maswali watakurushia. Utashangaa, iweje hawaelewi jambo rahisi namna hii?
"Haiwezekani mtu asiwe na dini!" Watakwambia huku wakijiweka tayari kwa ubishi. Ubishi. Wanabisha jambo linalohusu nafsi yako. Wewe unawaambia kuwa nafsini mwako huamini kitu kinachoitwa dini. Na huna dini, sio muislamu wala mkristo (maana dini kwao ni hizi mbili tu).
Wanakataa. Haiwezekani. Kila binadamu ana dini.
"Hawezekani kivipi wakati mimi ni binadamu na sina dini?" Unawauliza.
Wanajibu, "Acha kutuhadaa, kila binadamu ana dini. Ina maana huamini kuwa kuna mungu?"
Wakiuliza swali hili lazima nicheke kwanza. Hapo wanakuwa wamekwenda ninapotaka. Ndipo ukombozi wa akili toka kwenye mtazamo ulioletwa na dini za kuja unapotakiwa kuanza. Watu wengi wanadhani kuwa ukiwa huna dini basi humwamini mungu.
Mahesabu yake:
binadamu+ dini = imani juu ya mungu (yaani mungu yupo)
binadamu- dini = mungu hayupo
Hawajui kuna tofauti kubwa sana kati ya dini na kumwamini mungu. Wakati wengi wetu tunadhani kuwa dini kazi yake ni kutufanya tumjue mungu, kumwamini na kumtii, ukweli ni kuwa dini nyingi zinatuwekea ukuta wa chuma usionekana ambao unatuzuia tusimjue mungu. Ukiwa hutaki kumjua mungu, nitakushauri uwe na dini. Ukiwa unataka kumjua mungu, acha nazo. Najua sentenso hiyo ya mwisho inaweza kukufanya ujiulize kama "zimenitoka" au bado "zipo."
Dini inakufanya umjue mungu kupitia mawazo na mitazamo ya watu wengine (karibu wote ni wanaume) ambao wanavaa kanzu na majoho wakiongea kwa utaratibu ili uone kuwa wana tofauti sana na wewe na kuwa wana ukaribu na mungu. Werngine hudiriki kutuambia kuwa huongea na mungu. Ila ukiwaambia wakuite saa wanaongea naye ili usikilize au kushiriki, watakwambia kuwa kama huna roho safi huwezi kuongea naye. Lakini ninaposoma busara za Yeshua (Yesu/Isa) nakuta akisema kuwa mungu anatafuta wale waliopotea. Na ndio maana Yeshua alikuwa akishinda vijiweni na wacheza kamari na wachakaramu wengine. Miyahudi ikamjia juu, "He, wewe mbona unajumika na wenye dhambi?" Unajua aliwajibu nini? Kasome kitabu unachoamini kuwa ndio ramani na dira yako hapa dunini ingawa kinakusanya vumbi. Kila siku unahangaika na magazeti ya ushambenga lakini kitabu unachodai kimeandikwa na mungu mwenyewe hukisomi...turudi kwenye hoja ya msingi.
Kwahiyo unachojua kuhusu dini ni mawazo ya viongozi wa dini yako. Mawazo yao hayo ndio yanakuwa dira yako wewe ambaye una akili na uwezo wa kujitafutia ukweli mwenyewe. Dini inakufanya uwe mvivu. Hutasoma biblia au kurani kwasababu kuna viongozi wa dini yako ambao kazi yao ni kusoma vitabu hivyo na kukutafsiria mara moja kwa juma. Au wakati mwingine mara moja kwa mwaka...kama wewe ni wale wanaoenda kanisani misa ya usiku au siku ya krisimasi.
Dini inakufanya udhani kuwa kuna mashindano kati yako wewe mkristo wa kilutheri na mkristo wa kiangikana, au shahidi wa yehova dhidi ya mkatoliki, au mashindano kati ya muislamu wa sunni na yule wa shia, au mashindano kati ya muislamu na mkristo...mashindano ya kwenda mbinguni. Dini inakufanya uamini kuwa watu wote wasio na imani kama yako watakwenda unakoita motoni. Wewe na wenzako ndio mnajua hiyo njia nyembamba iliyozungukwa na malaika weupe (ndio malaika weupe, hakuna mweusi) wenye mavazi meupe ya kuelekea kwenye uzima wa milele. Pengine ndio maana tunajichubua ili tufanane na hao malaika.
Kuna watu ambao huniambia kuwa dini huleta amani. Jamani, hivi Rwanda watu hawana dini? Je Sudan? Je Kashmir? Je Iraki? Serikali ya Marekani inayopenda vita kama sijui nini inaongozwa na watu wasio na dini? Tuache nchi hizo, twende kule zilikozaliwa dini zinazoitwa "kuu" duniani: uislamu, ukristo, na uyahudi. Twende kule walikotokea manabii wa dini hizi. Kule walikotembea na kufundisha. Twende kule mnakotumia mamilioni kwenda kuhiji. Twenda Mashariki ya Kati. Twende Palestina. Twende Yerusalemu. Huko kila mtu ana dini. Kama sio mkristo, basi ni muislamu, kama sio muislamu basi ni myahudi.
Dini moja inafundisha amani (uislamu), nyingine upendo (ukristo) na nyingine kushika amri kumi. Twende huko tutazame jinsi ambavyo dini inaleta amani!
Nyooshea kidole nchi yenye amani kutokana na watu wake kuwa na dini. Tazama Indonesia, nchi inayoongoza kwa idadi kubwa ya waislamu, je inaoongoza pia kwa amani? Tazama Ufilipino, karibu kila mtu ni mkatoliki, je wanaongoza kwa upendo aliohubiri Yesu? Hivi Kongo hawana dini? Kama dini inaleta amani, nchi zenye watu wachache wenye dini zingekuwa zinaongoza kwa vita. Lakini ajabu ni kuwa nchi zenye watu wachache wanaojihusisha na mambo ya dini zinaonekana kuwa na amani zaidi ya nchi ambazo karibu wananchi wake wote wana dini. Au tuseme wanajifanya wana hiki kitu kiitwacho dini.
Kwahiyo watu wengi wanaamini kuwa kama binadamu wasingekuwa na dini, wangekuwa watu wabaya na waovu sana. Mimi hujiuliza, binadamu anaweza kuwa mwovu zaidi ya alivyo sasa? Kuna uovu gani uliobakia? Au mnadhani yanayotokea Palestina, Iraki, Sudani, Kongo, yaliyotokea Rwanda, Cambodia, Vietnam, Aghanistan, Ujerumani ya Hitler ni hadithi? Maovu makubwa kabisa kwenye historia tunayoijua yametokea katika kipindi ambacho wanadamu wana hiki kitu mnaiita dini.
Biashara ya utumwa ya Atlantiki miaka zaidi ya 400. Ile ya waarabu ilichukua miaka mingi zaidi maana ilianza kabla hii ya Atlantiki. Mauaji ya wayahudi na Hitler. Bomu la atomiki huko Japani. Ubaguzi wa rangi Marekani na Afrika Kusini. Vita vya Wazungu vya Kwanza na vya Pili (wengine mnaviita vita vya dunia...wazungu (na baadhi ya waasia) vita vyao wanataka kubebesha lawama dunia nzima kwa kuiita vita vya dunia. Nanyi mnakubali. Yaani hawataki tugawane mali waliyotuibia bali tugawane historia ya damu.) Mauaji ya halaiki Rwanda. Ukoloni. Yote haya yamefanyika katika kipindi ambacho wanadamu wengi wanasema kuwa wana dini.
Hivi wezi wanaoiba sirikalini na wengine kuuza nchi hawana dini? Wananchi wenye hasira kali wanaoua binadamu wenzao bila huruma kwa kuwa wamedaiwa kuwa wezi, hawana dini? Wala rushwa na wana magendo, hawana dini?
Najua moja ya hoja inayotolewa ninaposema mambo haya ni hii, "Vita na maovu hayo hayajaletwa na dini." Nakubaliana kwa kiasi fulani. Nasema kwa kiasi fulani kwakuwa historia iko wazi juu ya maovu yaliyoletwa na dini. Ila hata kama maovu hayo hayakuletwa na dini, tunaweza kujiuliza: kama dini inaleta amani iweje mambo hayo yote yanayoharibu amani yatokee?
Tukichimba zaidi hoja hii tunaweza kwenda kwenye hoja nyingine ambayo sitaiingilia kwa undani. Hoja hiyo ni kuwa huenda watu "wenye dini" ukweli ni kuwa "hawana dini."
Kwa upande mwingine unapochunguza sana kitu tunachoita dini unagundua kuwa dini ni pazia. Linakuzuia usimjue mungu wako wala manabii zako. Hapa ninazungumzia Waafrika.
Hivi wewe na akili zako zote unadhani Afrika nzima haijawahi kuwa na manabii?
Kwanini sina dini? Kama wewe ni mwafrika, huhitaji dini. Uafrika ni utamaduni. Utamaduni huu unatupa mwongozo kwa kila jambo, yakiwemo masuala ya kiroho. Wewe unaweza kuyaita dini. Kwahiyo uafrika una misingi na falsafa yake kuhusu mungu unayedhani kuwa simwamini kwakuwa nasema kuwa sina dini. Falsafa na miongozo kuhusu mungu iliyoko katika utamaduni wa Mwafrika, kwa mtazamo wangu, vinatosheleza. Hakuna kitu kipya ambacho uislamu, ukristo au uyahudi unaweza kunifundisha. Kwanza amri kumi ambazo ni msingi wa dini hizi zinazoonekana kuwa ni "bora" zaidi ya nyingine zilikuwa Afrika miaka mingi kabla Musa, aliyesema kuwa kapewa mlimani na yehova, hajazaliwa. Ngoja nirudie ili usidhani nimekosea: NINASEMA KUWA AMRI KUMI "ZA MUSA" ZILIKUWEPO AFRIKA KABLA MUSA HAJAZALIWA! Ni kati ya amri 147 zilizokuwa zikitawala maisha ya Waafrika katika bonde la mto Nile (Misri ya zamani, Nubia, Ethiopia, n.k.).
Soma historia. Sio ile unayodanganywa shuleni na walimu waliodanganywa shuleni kama wewe na vyuo vya ualimu. Tafuta historia yeu.
Wakati dini yako inakupa amri isemayo, "Mpende jirani yako kama nafsi yako," utamaduni wa Afrika unakupa falsafa hii: Mtu sio mtu bila watu (Kwa Ki-Xhosa, "Umtu Ngumtu Ngabantu). Kwa maneno mengine tunaambiwa tupendane. Falasafa hiyo ndio inakupa ujamaa, harambee, n.k. Marasta wao wanakuja na dhana kama hiyo wanaposema, "I and I."
Unadhani kanuni ya mtu sio mtu bila watu imetoka kwa shetani?

MAKALA MPYA: MAPINDUZI BILA DAMU WALA WAFADHILI

Nimeweka makala mpya iitwayo: Mapinduzi bila damu wala wafadhili. Bonyeza hapa uisome. Makala nyingine ziko upande wa kuume katika kona ya makala zangu.

MASAHIBU YA WALIMU NA ELIMU TANZANIA

Kuna habari katika inayosikitisha sana kuhusu walimu na elimu nchini Tanzania. Mengi yaliyosemwa katika habari hii sio mapya. Ninafahamiana na walimu wengi, marafiki na ndugu. Ninajua mtazamo wa sirikali ya Tanzania katika masuala ya elimu kwa wote. Kama tunataka nchi yetu iondoke katika orodha ya nchi fukara zisizo na mbele wala nyuma duniani lazima turekebishe mfumo wa elimu na kuwapa walimu heshima zaidi na kuwapa ujira halali kwa kazi kubwa wanayofanya. Soma habari yenyewe hapa. Unaweza pia kutembelea tovuti ya shirika lisilo la kisirikali, HakiElimu, linalojihusisha na masuala ya sera na mfumo wa elimu Tanzania. Hapa. Taarifa nilizonazo ni kuwa kazi ya shirika hili inahitaji pongezi. Nawapa pongezi zangu. Lakini sitaacha kuzungumzia suala hili: utaona kuwa tovuti yao ina tatizo lile ninalozungumzia kila kukicha. Wakati dhumuni kubwa la Hakielimu ni kuhimiza ushirikishwaji wa umma katika uendeshaji wa sekta ya elimu, tovuti yao ni ya kiingereza. Lugha inayotumiwa kila siku na huo "umma" katika mabasi, baa, makanisani na misikitini, majumbani, ndotoni, mikutano ya hadhara ya kisiasa, vijiweni, n.k. ni Kiswahili. Sijui kuna ugumu gani wa wanaharakati wetu kuelewa jambo hili rahisi namna hii: Watanzania wanaelewa Kiswahili zaidi ya kiingereza. Kwisha! Sisemi kuwa kiingereza ni lugha isiyofaa, hata kidogo. Hii ni lugha tunaweza kutumia tunapokuwa na maingiliano na wengine wasiojua Kiswahili. Ila tunapokuwa tunaongea sisi kwa sisi, kuna ugumu gani wa kutumia Kiswahili? Kuna hoja kuwa lugha ya kiingereza inatumiwa katika tovuti nyingi Tanzania (kama ya bunge, ikulu, ofisi ya waziri mkuu, KKKT, n.k.) maana watu wanaotumia teknolojia ya mtandao wa tarakilishi (intaneti) wengi ni wasomi wanaojua kiingereza. Hii ni sawa na kusema kuwa kwakuwa Wafaransa wengi wanaotumia mtandao wa tarakilishi wanajua kiingereza, kwahiyo tovuti ya serikali na bunge la Ufaransa na kila kitu nchini humo viwe kwa lugha ya kiingereza! Hoja hii (ya kuwa Watanzania wanaotumia mtandao huu wanajua kiingereza ndio maana tovuti ni za kiingereza) tuiweke kiporo kwa sasa, nitaikabili kichwa kichwa hivi karibuni.

3/26/2005

PADRI KARUGENDO: DAKTA SALMIN SEMA UKWELI

Kuna makala mpya nzuri sana ya Padri Karugendo iitwayo: Dakta Salim, Sema Ukweli. Makala nyingine za Karugendo zinapatikana kwenye kona yake hapa bloguni iitwayo Kalamu Ya Padri Karugendo. Kongoli hapa usome makala yake hiyo mpya.

3/25/2005

"UONGO HUO" - JHIKO MAN

Rafiki yangu Da' (unajijua) umenitajia Jhiko Manyika. Nimemsikiliza sana leo. Kuna nyimbo zake mbili nadhani lazima azirekodi tena. Hasa wimbo wa Uongo huo. Leo nimeusikiliza vizuri sana. Nitawapigieni hapa siku moja. Ngoja niwapeni maneno ya wimbo huo. Kabla sijawapa, kwa wasiomjua, Jhiko Manyika ni mwanamuziki wa Rege nchini Tanzania. Tazama picha yake hapa.

UONGO HUO

Uongo huo, uongo huo, uongo huo,
Tusisumbukie uongo
Tuijue kweli na hiyo kweli
Itatuweka huru

Wale Waafrika tusio makini
Tumedanganyika,
Wakati ndugu zetu wanadai utu wetu
Sisi tunalalamika,
Wale Waafrika tusio makini
Tumedanganyika,
Wakati ndugu zetu wanadai utu wetu
Sisi tunakasirika

Tamaduni zetu
Tunasema ni za kishenzi,
Wazee wa kuwapa heshima
Tunasema ni wachawi wanatuua

Uongo huo, uongo huo, uongo huo,
Tusisumbukie uongo
Tuijue kweli na hiyo kweli
Itatuweka huru


Wale Waafrika tusio makini
Tumedanganyika,
Wakati ndugu zetu wanadai utu wetu
Sisi tunalalama,
Wale Waafrika tusio makini
Tumedanganyika,
Wakati ndugu zetu wanadai utu wetu
Sisi tunalalamika


Tunathamini vitu
Tunasahau utu

Uongo huo, uongo huo...

3/24/2005

MAPINDUZI YA UMMA AU ?

Kwa sasa siwezi kujua kama haya ni mapinduzi ya umma kwa faida ya umma au ni mchezo wa kuondoa wezi hawa na kuingiza wezi wale. Imetokea leo hii huko Kyrgyzstani. Historia ya mapinduzi kama haya ni ndefu. Kwa miaka ya karibuni tuna mifano michache. Yalitokea kule Jojia. Kongoli hapa. Kisha tukasikia Ukraine nako. Hapa. Halafu ikaja zamu ya Lebanoni. Hapa. Na sasa imetokea Kyrgyzstani. Hapa. Baadaye itakuwa wapi? Swali ninalojiuliza ni hili: mapinduzi haya ni kwa faida ya nani? Kitendo cha Marekani kushabikia mapinduzi ya Ukraine na kule Lebanoni kinafanya watu wengi wasite kufurahia kuwa umma umetwaa madaraka toka mikononi mwa wezi wachache. Tuna macho, tuna akili, tusubiri. Jambo la kushukuru katika yote haya ni kuwa hakuna watu walionyanyua silaha na kuingia msituni.

3/23/2005

WAKOLONI NA JINA LANGU JIPYA

Rafiki yangu mmoja kanikumbusha jina langu jipya nililopewa na Mloyi katika maandalizi ya kurudisha tawala za kikoloni barani Afrika. Jina hilo ni: Nesto McChair. Unaona karibu linafanana na Ndesanjo Macha. Kuna ukaribu fulani.

Maandalizi ya kurudisha tawala za kikoloni yanaendelea vizuri. Tenda ya ujenzi wa kiwanda cha dawa za kujichubua imeshatangazwa na sirikali ya Tanzania. Tayari tumeshapata washauri kuhusu kujichubua toka (zamani iliitwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo) Jamhuri ya Kidemokrasia Iliyo Katika Vita Vya Wenyewe kwa Wenyewe ya Kongo. Pia sirikali imeamua kuwa itamchagua mwanamuziki Maiko Jakisoni kuwa waziri wa nchi wa masuala ya kuondoa nuksi ya rangi nyeusi. Kumbuka shetani rangi yake ni nyeusi, na kamwe binadamu mwenye akili zake hawezi kukubali kuwa na rangi moja na shetani.

Halafu ule mradi wa kuandika biblia upya ili kuweka habari za mashirika yanayofanya kazi inayoendana na ule mfano wa Yesu wa Msamaria Mwema, yaani Benki ya Dunia na Shirika la Fedha Duniani unaendelea vizuri. Pia ili majina ya nabii Musa wa zama hizi, Tony Blair, anayetaka kuwakomboa wana wa Israeli huko Zimbabwe toka katika mikono ya Farao Mugabe yaingia kwenye kitabu hiki kitakatifu. Pia jina la Joji Kichaka ambaye ni Musa wa karne hii anayewasaidia Wairaki kuelekea kwenye zama za asali. Mradi huu unaenda polepole kutokana na ukweli kuwa aya zinashushwa taratibu sana. Sijui ni tatizo la mitambo ya mawasiliano au ni nini.

Kabla sijasahau, ile barabara mliyoiita Barabara ya Nyerere tuko mbioni kuibadili jina. Lazima Nyerere tumwondoe kwenye historia yetu kwa jinsi "alivyotulostisha." Kimbelembele chake cha kugombea uhuru kimetuletea umasikini mtupu. Napandwa na hasira. Siwezi kuendelea kuandika. Ngoja nilie kwanza halafu nitafute picha yake niliyonayo niichanechane. Na nikisikia mtu anasema, "Ujamaa ni kujitegemea ndio njia pekee ya kujenga jamii ya watu walio sawa na huru" huyo mtu ajue tutakosana. Zitakunjwa. Ama zangu, ama zake. Ngoja nikanywe maji nipunguze ghadhabu niliyonayo dhidi ya Maumau, Nkrumah, Neto, Toure, n.k. kwa kimbelembele chao cha kudai uhuru.
Tazama Mwalimu Nyerere alivyotufanya tukawa tunakimbia mchakamchaka huku tukiimba Kaburu matata iya! Tulikuwa na nyimbo kibao za kuwasakama na kuwabeza makaburu. Sasa hivi majuzi tumekuja kujua kuwa kumbe ni watu wazuri sana. Tena wacha mungu. Halafu hawana kinyongo na sisi hata kidogo. Nadhani wanafuata mafundisho ya biblia yasemayo, "Samehe hata mara saba u sabini." Wamatusamehe na kuamua kuja nchini kwetu kutusaidia kuchimba madini ya Tanzanite kwa faida yetu!

3/22/2005

MIZIMU YAO ILITOKA WAPI?

Wanasema hatuwezi kupiga hatua kuthaminiwa wala kutambuliwa,
Eti sababu sisi ni watu weusi Eeeh!
Ulimwenguni tumepewa laana,
Usiseme hivyo hebu acha kukufuru,
Kwani aliyetuumba hapendezwi hivyo.
Bob Marley naye Peter Tosh, niambie mizimu yao ilitoka wapi?
Mwalimu Nyerere, Nelson Mandela, niambie mizimu yao ilitokea wapi?
Kwame Nkrumah na Haile Selasie, niambie mizimu yao ilitoka wapi?
Martin Luther King na Marcus Garvey, niambie mizimu yao ilitokea wapi?
Kaza moyo ndugu Eeeh bado safari ni ndefu...
- Marehemu Justin Kalikawa katika wimbo wa Mizimu.

KICHAA MWENYE UPARA

Tunawajengea magereza,
Tunajenga shule zenu,
Mnatupa elimu ya kutupumbaza,
Mnatutuza chuki kwa upendo wetu
Mkitusimulia juu ya mungu wenu aliye mbinguni...
- Bob Marley katika wimbo wa Crazy BaldHead

MWANAHARAKATI WA MTANDAO WA KOMPYUTA AFARIKI

Mwanaharakati wa haki za binadamu na uhuru wa vyombo vya habari anayetumia mtandao wa kompyuta (cyber-dissident) wa nchini Tunisia, Zouhair Yahyaoui (36), amefariki dunia hivi karibuni. Aliaga dunia tarehe 13 mwezi huu kwa ugonjwa wa moyo. Yahyaoui atakumbukwa kwa mchango wake katika kupigania haki na uhuru wa habari nchini Tunisia. Yeye ndiye mwanzilishi wa webu ya tunezine.com. Yahyaoui alikuwa ndiye mtu wa kwanza kushinda tuzo mpya ya Cyber-Freedom mwaka juzi. Tuzo hii hutolewa na shirika la Waandishi Wasio na Mipaka (Reporters sans frontières ). Ukibonyeza hapa utaona webu mbalimbali zenye habari zaidi juu ya wanaharakati wanaotumia teknolojia ya kompyuta na nguvu za dola zinazotumiwa dhidi yao.

BARUA YA EDUMEDUS NYONYI KWA PADRI KARUGENDO

Mwanafunzi wa Mlimani, Edumedus Nyonyi kamwandikia Padri Karugendo waraka wenye kichwa hiki: Ujumbe Toka Makaburini. Karugendo kasoma ujumbe huo na kutumia marafiki zake. Nami nimeusoma na kuamua kuuweka ndani ya blogu nanyi muusome.
Mpendwa Padri shikamoo.
Mwezi januari nilibahatika kutembelea eneo la mazimbu Morogoro yalipo makaburi ya wapigania uhuru wa Afrika ya Kusini. Hakika baada ya kutoka huko naona sina raha maishani mwangu. Hata hivyo nimeonelea nikushirikishe sauti hii niliyoisikia hata kama huenda ulishawahi kufika na kushuhudia mwenyewe nakuhakikishia mwangwi wake umebadilika.
Baada ya kufika makaburini ambayo yanatunzwa vema kuliko ya ndugu zetu wanaozikwa Kinondoni au Mburahati, niliona kibao chenye ujumbe ambao umeweka alama katika maisha yangu. Maneno haya yalisomeka hivi"Ours was not for grory nor personal distinction but it was due for the noble cause of our time and the liberation of humanity of the entire community of South Afrika."
Wakati bado nimepigwa ganzi na ujumbe huo huku nisijue la kufanya, wenzangu niliokuwa nao yapata kama ishirini hiv,i wao walikuwa wanashughulika na kupiga picha za ukumbusho. Nilidhani labda mimi ni mjinga kushughulika na kisicho na maana badala ya kuweka kumbukumbu ili nije nikawaonyeshe watu kwamba nani nilishawahi kutembea.
Hata hivyo nilihitimisha kuwa mtu mwenye akili hawezi kushughulika na mambo mengine na kuacha ujumbe wa kutisha, wa kijasiri wa kizalendo, wa kujitoa mhanga kama huo. Basi nilijua ndio elimu yetu ya siku hizi maana imekaa kiutandawazi.
Kumbe vifo vyao havikuwa ili waandikwe kwenye majina ya vitabu vya historia waka kutungwa kwenye nyimbo huku wakisifiwa kila mara! Kumbe kufungwa kwa mandela hakukuwa kukuza jina la ukoo. Bila shaka walijua wazi kuwa wanacho kipigania wanaweza wasikifaidi lakini kwa utu wao na vizazi vijavyo walilala mistuni kama wanyama.
Swali lilinijia kuwa Je ukombozi wa utu wa mwanadamu sasa umekwisha.Uliondoka na kuisha kwa ubaguzi?. La hasha bado tu watumwa wa wageni na hata ndugu zetu. Ndipo nikaenda mbali kuwa watu wanalala darasani ili wapate madgrii wawe maprofesa kwa ajili ya kukomboa wenzao au kukuza jina tu. Na rais na wabunge wanataka nafasi hiyo kama ujumbe wa makaburi ulivyo au ni "for grory and personal distinction".
Niliwahi kukuandikia kuwa nataka kuingia kwenye siasa. Na sababu ni hicho kilio cha makaburi. Nataka nione kama walau elimu yangu naweza kuitumia kuukomboa utu wa mwanadamu tena bila kujulikana kama ikibidi. Nilipanga mwaka huu kugombea udiwani Kanyigo au hata popote ambapo wangelinikaribisha. Niliwaandikia ndugu zangu waanze maandalizi wakadhani nimechanganyikiwa. Hivyo kwa mwaka huu na shughuliza kumalizia masomo naona nitakwama. Wasalaam Nyonyi.

PADRI KARUGENDO: BURIANI JUSTIN KALIKAWE

Nimeweka makala mpya ya Padri Privatus Karugendo. Makala hii iliandikwa baada ya kufariki kwa mwanamuziki wa Rege, Justin Kalikawe. Alifariki Agosti 12, 2003. Ingawa makala ni ya muda mrefu, ujumbe wake una uhai hadi leo. Nakumbuka mara ya kwanza kumsikiliza Kalikawe, ilikuwa ni 1991/92 nikiwa Ilboru. Nadhani Tunga ndiye alikuwa na kanda moja yenye nyimbo zake ambazo sijui kama alikuja kuzirekodi rasmi. Nilijua kuwa nyota mpya ya Rege Tanzania inachomoza. Wimbo wake wa Mizimu ambao Padri Karugendo kauzungumzia unaweza ni wimbo wake ninaoupenda kuliko zote. Wimbo wake wa Machinga nakumbuka ulipigwa sana katika mitaa ya jiji la Dasalama. Na wimbo wa MV Bukoba ulitukumbusha msiba mkubwa wa taifa uliotokea kwenye lile ziwa lenye jina la Malikia wa Uingereza, Vikitoria (au Vikii kwa kifupi). Bonyeza hapa usome makala hiyo ya Kalikawe. Bonyeza hapa usikilize baadhi ya nyimbo zake. Ukifika kwenye webu ya Mzibo, bonyeza juu ya picha ya Kalikawe. Kumbuka makala nyingine za Karugendo ziko kwenye safu yake hapa bloguni iitwayo Kalamu ya Karugendo.

3/21/2005

WAMISIONARI HAWAKUELEWA WAAFRIKA

Wamisionari walipofika Afrika walitakiwa kwanza wakae chini waelimishwe. Hakutuelewa hata kidogo. Tatizo lao kubwa lilikuwa ni wanatumia tamaduni zao kama kipimo cha ukweli, ustaarabu, na ubinadamu. Kutokana na kutumia tamaduni zao karibu kila jambo toka katika tamaduni zetu lilionekana kuwa ni la kishenzi. Wakatuita wapagani. Wakasema mungu wa kweli hatumjui wao ndio wanamjua. Wakatuambia tumfuate huyo mungu wanayemwabudu wao. Laiti wangejishusha na kuamua kujifunza tamaduni zetu, falsafa, na mantiki zake, toka kwetu.
Kwa mfano walidhani kuwa Waafrika wote wanaabudu miungu wengi. Waliposikia tunasema kuwa kuna mungu wa uzazi, mungu wa mvua, mungu wa mazao, mungu wa maji, mungu wa jua, n.k. wakadhani tuna miungu kibao, pengine isiyohesabika. Kumbe Waafrika wengi tunaposema mungu wa hiki na mungu wa kile tunamzungumzia mungu mmoja. Mungu ni mmoja ila sifa na kazi zake ni nyingi. Tunaamini kuwa nguvu tunayoiita mungu ni vigumu sana kuielewa kwa fikra za kibinadamu. Hatuwezi kabisa kuielewa nguvu hii kwa kufikiria tu na kuunda taswira fulani kichwani huku nguvu yenyewe hatujaiona kwa macho. Kutokana na ugumu huu, Mwafrika anajaribu kumwelewa mungu kupitia kazi zake mbalimbali kama vile uumbaji (hapo ndio unakutana na mungu wa maji, uzazi, mazao, mito, n.k.) Tuliamini kuwa yeye ndiye anatupa maji. Kutokana na kazi yake hiyo tunamwita mungu wa maji. Yeye ndiye katupa mbegu, hapo tukamwita mungu wa mazao. Lakini ni mungu huyo huyo mmoja. Kwahiyo mungu kwetu ni muumbaji na kazi zake za uumbaji tunaziona na hapo ndipo tunamwona yeye. Kwahiyo Waafrika tunamjua mungu kupitia kazi zake mbalimbali, lakini mungu huyo ni mmoja.

Wamisionari waliposikia kuwa tuna mungu wa maji, na uzazi, na mavuno walituambia tuachane na imani hizo maana kuamini mungu zaidi ya mmoja ni kinyume na amri yake. Wakadai kuwa huko ni kuvunja amri ya kwanza. Ajabu ni kuwa baada ya kutuambia tuachane na mungu wa maji, mungu wa uzazi, na mungu wa mazao walitupa mungu baba, mungu mwana, mungu roho mtakatifu wakatuambia kuwa huyo ni mmoja. Kama falsafa yetu ya mungu wa uzazi, mungu wa maji, na mungu wa mazao, haimaanishi mungu mmoja, iweje mungu baba, mungu mwana, mungu roho mtakatifu awe ni mungu mmoja? Halafu tulipofungua kitabu cha Mwanzo katika biblia tukakuta inasema: "Na tuumbe mtu kwa mfano wetu." Inakuwaje mungu mmoja anasema "... kwa mfano wetu?" Wetu wangapi? Mmoja? Waulize swali hili wafuasi wao. Ninajua watakavyokujibu,
Ukiwavalia njuga suala la mungu baba, mungu mwana, na mungu roho mtakatifu kuwa mmoja (lakini mungu wa uzazi, mazao, na maji sio mungu mmoja) watakuambia kuwa hiyo ni siri. Ni fumbo. Wanaita fumbo la utatu. Kwa ufupi, wamisionari walikuwa na uelewa finyu sana na dharau. Kazi tulionayo sasa ni kuelimisha wale walioamua kufuata falsafa, na teolojia zao.

TUNAJIGAWIA KAZI

Binadamu tusipofanya kazi kwa kujiwagia au kugawana kazi kama siafu au mchwa, tunaweza kujikuta wote tunafanya kazi moja. Kwahiyo katika nchi wote tukiwa waimba mapambio na nyimbo za chipukizi za kusifu watawala mapambia na nyimbo hizo vitakuwa ni kelele. Jamani, wote msijiunge na kwaya au chipukizi. Wengine mkikimbia mchakamchaka msiibe. Tukiimba wote hatutasikilizana. Wengine waimbe, wangine wasikilize, wengine waongee, wengine waandike, wengine wapime, wengine wakosoe, wengine wapinge, wengine watazama tu...
Kwa mfano, kuna wanaosifia jinsi Tanzania "inavyokwenda mbele." Soma gazeti la uhuru na sikiliza hotuba za viongozi kama unataka kusikia jinsi Tanzania inaelekea kukamilisha Dira ya Kitaifa Ya Maendeleo ya 2020. Waombe watu wanaowandikia hotuba zao wawe wanakutumia nakala za hotuba zao. Kwahiyo viongozi hawa na gazeti kama Uhuru wanafanya kazi nzuri ya kusifu. Sasa kuna wengine kazi yao sio kusifu bali kuzungumzia ile asilimia nyingine ambayo watawala na wanasiasa huwa hawasemi. Kawaida wanatuambia mambo yanayowahakikishia nafasi walizonazo. Ile asilimia wasiyotaka ujue, pale wanapotaka uamini kabisa kuwa nchi yako inakwenda mbele kwa kasi, inatolewa na wengine. Hawa wanaifurahia sana kazi hiyo na inapokuwa mshale wa moto kuwaingia wale wanaoamini wimbo wa "Tanzania inapiga hatua za maendeleo" ndio wanafurahi zaidi maana ndio moja ya kazi zao. Watu hawa lazima tuwachome kwa mshale wa moto. Pambio la Tanzania kuendelea limewaingia katika nafasi zao kiasi ambacho wakisikia mtu anasema kuwa Watanzania wana haki ya kuwa daraja la juu zaidi ya walipo wanaona kama vile wametukanwa. Inakuwa ni kinyume na imani waliyojengewa. Mbaya zaidi ni pale mtu huyo huyo anakuwa anapata mishale unapoongelea sio siasa tu bali dini. Anapata tabu sana. Anapata ghadhabu. Hajui afanye nini. Anaandamwa hadi kwenye imani ya nafsini mwake. Inavunjwavunjwa. Teolojia yake inahojiwa. Inarushwa huku na kule. Kitabu chake anakuta kumbe wala hakijui sawasawa. Anashtuka pia kujua kuwa hatuogopi kuwasema viongozi wake wa dini kuwa ni waongo. Au wanakandamiza wanawake. Kama ni mkatoliki unamuuliza, "Kuna kosa gani mwanamke akiwa Padri?" Mtazame atakavyojilambala mdomo. Kama ni muislamu mwambie, "Kurani inasema mwanamke akikosea una mambo matatu ya kufanya: 1.kataa kulala naye kitanda kimoja 2. muonye 3. mpige." Hiyo namba tatu ndio ninaipenda sana. Muulize, "Je mwanaume akikosea kwenye uislamu anafanywe nini?"
Nimeamua kuwa nitaanza kutafuta kipaji cha kusifia. Ingawa kipaji hiki sikipendi sana, nitakitafuta ili niridhishe kila upande.

WEWE MWANAMKE MWANAHARAKATI

Katika waraka wa awali (kabla ya huu) nilianza kuongelea vyombo vya habari, nikarukia mengine. Kuna raha wakati fulani kuandika tu bila kujua hasa unakwenda wapi na utaishia wapi. Waraka uliopita nilikuwa naongelea wanaharakati wanaotaka kubadili nchi kabla hawajabadili mtu mmoja mtaani kwao.
Hii inanikumbusha wanaharakati wanawake wanaounda vyama, mitandao, na kufanya mikutano na makongamano ili kuondoa udhalimu wa mfumo dume. Wanaharakati hawa wanaisukuma sirikali ili iweke mazingira ya kisheria na kisera ambayo yatatoa nafasi sawa kwa wanawake na wanaume. Wanawake hawa wanaharakati wanawashauri, wanawahimiza, na kuwaunga mkono wanawake wenzao wanaogombea nafasi mbalimbali za uongozi.
Swali kubwa hapa ni hili: ni kitu gani kinawafanya wanaharakati hawa wagombee haki za kisiasa na kiuchumi lakini sio za kidini na kiimani? Wanawezaje kuitaka sirikali kuhakikisha kuwa wanawake wanapewa nafasi sawa katika jamii lakini hawataki dini zao kutoa nafasi hiyo sawa? Unakuwa mwanaharakati wa jinsia na wakati huo huo dini yako ni Ukatoliki wa Roma ambao haumpia mwanamke huyo unayemtetea haki sawa? Kwanini unataka wanawake wawe viongozi kwenye shughuli za siasa, uchumi, na utawala ila sio kwenye dini? Ni lini wanawake watakuwa mapapa na maaskofu? Ni lini wataruhusiwa kuhubiri mbele ya umma wa wakatoliki au waislamu? Ni lini tutawaona wakiwa kwenye uongozi wa juu wa Bakwata au jimbo? Kama hawana haki ya kuwa na uongozi kwenye mambo ya maana kama ya mungu, kwanini wawe na uwezo wa kuongoza kwenye mambo ya kibinadamu? Kwanini sirikali inayoongozwa na wanadamu iwape haki sawa wakati dini inayoongozwa na mungu (kwa mujibu wa wafuasi wa dini yenyewe) haiwapi hizo haki? Je wanadamu tukisema kuwa mfumo dume ni mfumo tunaoiga toka kwa mungu tutakuwa tumekosea? Kama mungu hataki waongoze mambo yake au wahubiri juu yake, kwanini sisi tuwachague? Kama mwanamke hawezi kuwa kiongozi wa juu wa wakristo au waislamu, kwanini apewe uongozi wa juu wa nchi? Kama mungu hataki wanawake wawe mashehe, maimamu, mapadri, maaskofu, n.k. kwanini sisi tung'ang'anie kuwa na viongozi wanawake?
Haki ya mwanamke inayodaiwa kwenye ulingo wa siasa ni haki hiyo hiyo ambayo inapaswa kudaiwa katika dini zinazoongozwa na wanaume wanaojichukulia kuwa ni bora zaidi.
Mwanaharakati yeyote wa jinsia, awe mwanaume au mwanamke, lazima apambane na mfumo dume ulioundiwa mistari ya unabii ili kumbagua, kumdhalilisha, na kumkandamiza mwanamke.

MAENDELEO YA VYOMBO VYA HABARI

Vyombo vya habari vya Marekani vimeendelea sana kama vile vya Tanzania. Habari za vyombo hivi ni za muhimu sana kwa maisha ya binadamu. Kawaida, maendeleo ya vyombo vya habari yanapimwa kwa vigezo vingi sana, kimojawapo ni kutazama umuhimu wa habari zinazotolewa katika maisha ya binadamu kwa ujumla. Tazama habari kwenye gazeti kisha jiulize, hivi habari hii ndio iliyotusaidia tukajenga shule ya Mapinduzi ambayo jiwe lake la msingi limewekwa juzi? Je habari hiyo kama hatuna tutashindwa kupambana na rushwa kikamilifu? Je habari hiyo inasaidia binadamu waweze kuishi kwa utu zaidi?
Ukipima kwa kipimo hicho utajua kuwa vyombo hivi katika nchi za Marekani na Tanzania vimeendelea sana. Kwa mfano, dakika 35 zilizopita vyombo vya habari hapa Marekani vimetupa habari nzito kuliko zote katika siku hii ya leo. Habari hii ni muhimu mno. Umuhimu wake ndio umenifanya niseme ninayosema. Nimeamua nikugawie na wewe habari yenyewe kwani itakusaidia sana katika harakati zako za kupata elimu, kazi, huduma bora za afya, kutaka barabara nzuri hadi vijijini, na kudai uwajibikaji. Usipoipata, vyombo vya habari hapa vinatuambia, utakuwa umekosa jambo moja kubwa sana maishani. Vyombo hivi na vile vya Tanzania ni kama pacha. Sijui nani kajifunza kwa mwenzie.
Kila mtu nchi nzima (yaani Tanzania) anajifanya kuwa ni mfuasi wa hizi dini za kuja. Anajifanya kuwa anatii Amri Kumi za huyo mungu wake. Lakini Mtu huyo huyo habari anazopenda sana kuzisoma ni zile zinazohusu watu wanaovunja amri za mungu wake kuliko habari za watu wanaotii amri za huyo mungu. Ndio maana nikisema kuwa Tanzania watu hawana dini wengine mnanijia juu. Nadhani kuna faida fulani ya waislamu na wakristo kutokutii amri kumi wanazodai kuzifuata. Kama wangetii amri hizo nani, kwa mfano, angeua wezi? Wezi wangetumaliza maana wasingekuwa na woga. Hivi sasa wanaiba kwa woga maana wanajua kuwa mkiwakamata, ingawa dini zenu zinakataza msiue, lazima mtawaua. Mtawapiga hata kama hamna ushahidi. Mtawachoma moto. Kisha mtaondoka zenu kuelekea kwenye mazoezi ya kwaya, misa ya jioni, au sala ya alasiri. Mkifika huko mnadai mungu anasema katika Amri ya sita: Usiue.
Nadhani kuna mistari ilifutika kidogo katika amri hiyo. Labda karatasi ililoana. Mistari iliyofutika inasema, "Usiue labda awe kijana masikini mwizi wa elfu kumi. Wale wezi wa mamilioni, kwa jina langu, muwasamehe na kuwafanya wawe viongozi wenu. Wanayofanya ni mambo mazuri sana kiasi kwamba mnataka wao watangulie nyie mtawafuata. Wao ndio wanajua njia.
Na ile Amri ya Nane isemayo usiibe nasikia kuna maneno yaliyofutika pia. Ilikuwa inasema, "Iba ili mradi usikamatwe. Na ukishaiba usisahau kunijengea mimi bwana wa majeshi makanisa na misikiti kwa fedha hizo za wizi."
Mkristo au muislamu akienda kununua magazeti, kukawa na gazeti moja linasema, "Fahamu kurani na biblia inasemaje kuhusu vyakula vifaavyo kutunza hekalu (mwili) la bwana," na jingine linasema, "Kondomu zinazoongeza raha kwa mwanamke zagunduliwa." Unadhani watanunua gazeti jipi? Najua kwakuwa ni waumini wa dini mbili "kuu duniani" watachagua lile gazeti la mambo ya mungu wao. Je kama kuna habari kuhusu mjadala wa wabunge kuhusu muswada wa marekebisho ya katiba na gazeti jingine lina habari ya mbunge aliyekuwa amelala wakati wa mjadala huo, unadhani Watanzania wengi watanunua lipi? Acha kudharau Watanzania, yaani unafikiri wengi watanunua lenye habari ya mbunge kulala? Una maana pia kuwa hawatanunua habari kuhusu kurani au biblia bali habari kuhusu kondomu? Nakataa.
Narudi Marekani. Nilisema kuwa kuna habari imetokea dakika 35 zilizopita ambayo ndio namba moja kwa siku. Sitaki uikose. Nayo ni hii: MAIKO JAKISONI AMECHELEWA KWENDA MAHAKAMANI.
Huoni nisingekwambia maisha yako yangeharibika? Ndio kuendelea kwa vyombo vya habari.
Tafuta maana ya yote niliyosema. Au kulalamika. Kuna jamaa wanasema kuwa eti mimi napenda kulalamika na sio kuchambua. Tunatakiwa kulalamika. Tukilalamika wote itakuwa kelele. Kelele hiyo itamtoa chatu pangoni kwa woga. Kulalamika ni kupinga. Kulalamika ninakozungumzia hakuna maana ya kulia kama mtoto. Kulalamika kwa kuelimisha na kuamsha. Kwa kila lalamiko, maarifa. Kila lalamiko, historia. Kila lalamiko, ukweli. Kila lalamiko, falsafa. Kila lalamiko upinzani wa kitamaduni. Kila lalamiko, utaifa. Kila lalamiko, uafrika. Kila lalamiko, mwamko. Mapinduzi. Ya dhati.
Kila ninapoandika neno mapinduzi kuna watu akili zao zinakimbilia kwenye silaha. Sijui kwanini baadhi ya watu ni rahisi kufikiria silaha na vita namna hiyo. Yaani tutumie vita, tuangamize uhai, kwa ajili ya kutetea uhai? Mbona wanadamu tuna akili na maarifa tele ya kuondoa udhalimu wa njia na mikakati isiyohitaji silaha? Fungua vitabu vya historia. Fuata nyayo za waliokutangulia.
Wengine wakisikia neno mapinduzu wanaanza kufikiria idadi ya watu. Wanajiuliza, "Mapinduzi hayo ni lini wakati kila mtu amepotea? Itachukua muda gani watu wote kufumbua macho?" Usithubutu kufiria namna hiyo. Mabadiliko makubwa ya jamii huletwa na watu wachache ambao wanakuwa kama vile wa ugonjwa wa kuambukiza. Isitoshe kuna kanuni ambazo ni za wazi kuhusu jinsi ya kuleta mabadilikobila kumwaga damu, kuhitaji pesa, kuhitaji nguvu za dola, vyombo vya habari, n.k.
Wanaharakati wengi ninaoshauriana nao wanalalamika kuwa hawana uwezo wa kuwa na vyombo vya habari. Wanataka wapate chombo cha kuwasiliana na taifa zima. Ninawauliza mifano ya vyombo wanavyozungumzia, wanataja magazeti, redio, luninga, webu, n.k. Nawauliza, "Kuna chombo cha habari kikubwa kuliko mdomo? Kwa siku unasoma maneno mangapi na mangapi unasikia toka kinywani mwa mtu?" Nawaambia kuwa midomo yao na midomo ya wengine kama wao ndio vyombo vya habari.
Wengine wananiuliza, "Unajua kaka mimi nina mawazo mengi napenda wananchi wenzangu wayajue lakini sina upenyo wa kuyatoa. Unaweza kunisaidia nipate safu kwenye gazeti lolote?" Nawauliza kama wamehawai kuandika hayo mawazo yao yakasomwa na marafiki zao wa karibu, majirani, vijana wenzie kijiweni, wanafunzi wenzake, waumini, ndugu zake na hata wazazi wake. Wanasema kuwa hao watu watawasomaje wasipotolewa gazetini. Nawauliza, "Je masomo shuleni unaandika wapi?" Wanasema kwenye daftari. Hapo ndio tunakuwa tumefika kwenye kilele cha mazungumzo. Kama mtu anaweza kuandika mambo kwenye daftari na yakasomeka, kwanini asitafute daftari zuri akaandika hayo anayotaka kuandika magazetini ili waliomzunguka waelimike? Kwanini asubiri hadi apewe safu gazetini? Asipopewa safu mawazo yake ndio yanapotea? Je kila mwelimishaji lazima awe na safu ili mawazo yake yawe na faida kwa binadamu?
Anzisha safu ya mtaani kwenu. Kanunue daftari dukani. Andika, wape watu wasome. Mabadiliko ya nchi hayatokei ghafla. Ni mabadiliko yanayoanzia mtaani ndio yanayobadili taifa. Ni kitu gani kinakuzuia kufanya unayotaka kufanya kwa Watanzania wote kwa wakazi wa mtaani kwenu? Kwanini unataka kuanza na nchi? Taifa letu lina mtazamo wa ajabu kabisa wa maendeleo. Unaona tuliowachagua ndio huwa wanaamua maendeleo ni kitu gani. Sio tunawachagua ili watekeleze kile sisi tunachoamini kuwa ni njia ya kuleta maendeleo. Wanataka sisi ndio tutekeleze wanachoona kuwa ndio njia ya kumkomboa Mtanzania. Hii ni demokrasia ya kushushwa kama aya za manabii wanazotuambia wameshushiwa. Demokrasia ya kweli inaanza chini inakwenda juu. Ni pale mimi na wewe tunapoweza kufanya mwenyekiti wa mtaa atimize wajibu wake. Na aogope nguvu ya wana mtaa maana anajua kuwa asipotimiza kazi zake hatachaguliwa tena. Mkiweza kuwa na serikali ya mtaa inayofanana na sirikali kuu mnayoitaka, hapo ndipo mnaweza kuanza kuzungumzia kubadili mfumo wa sirikali kuu. Lakini kama mwenyekiti wa mtaa ni mzembe, mwongo, mbadhirifu, na mla rushwa na mnaendelea kumchagua maana anawapa pilau, usitarajie utaweza kuleta mabadiliko huko juu.
Nitaendelea...

KUOA MZUNGU

Jana nilimzungumzia yule bwana aliyeniandikia akisema kuwa watu wanaooa wazungu wanasahau Uafrika wao. Alikuwa akinishitumu pengine kwa kudhani kuwa nimeoa mzungu. Rafiki yangu mmoja kaniandikia akijibu tuhuma ya huyu bwana ambaye anataka tuamini kuwa aliyeoa Mwafrika hana Uafrika kama aliyeoa Mwafrika mwenziye. Ninaibandika barua yake hapo chini muisome:

Hali gani?

Vipi mjomba, naona unaamsha hisia za watu mbalimbali.
Haya, kuna jambo linatatiza. Hivi kuoa mtu mweupe au mchina ni kusahau uafrika? mbona Agostino Neto wa Angola alikuwa na mke mtu mweupe wakati Mobutu alikuwa na mke mweusi ti, yupi mwafrika sana Mobutu au Neto? Sina hakika, Gamal Nkrumah si mtoto wa Nkrumah mwanamapinduzi tunaemuenzi.. mama yake si ana asili ya kiarabu..wakati washenzi wengi wengi wengine akina Abacha wana wake weusi. Wezi wote tanzania wameoa waarabu? Utu wa mtu, au Uafrika wa Mwafrika si pambo la kuvaa au kito cha kuonesha..au kwa mahusiano ya unyumba tu.
Nawaona wengi wenye siasa za kushutumu watu weupe kwenye vilabu huku ughaibuni, ikesha mwisho wa usiku utawaona hao wanachukua vimada weupe kwenda kufanya zinaa mbele huko.

Kesho yake utawasikia tena wakicheka fulani kaoa mweupe, kwenye kiza vipembeni haoooo! nao wanashiriki weupe.
Nafikiri suala kubwa hivi sasa ni hili - Je tunafanya nini kwa Afrika. Mchango wetu ni upi. katika siasa watu wanao ogopa ukweli siku zote hutaka kumuua tarishi, kumtusi tarishi ili ujumbe wake udharauliwe. tukitizama vita ya kichaka huko umangani... watu wote waliotaka kusema kweli wako wapi... utu wao na kazi zao vyote vilitiwa dosari ili ukweli juu ya vita usitoke.

Basi twende mbele na turudi nyuma, tutahadhari na mambo ya binafsi, huyu anakula makdonad basi si mzalendo, huyu kavaa tai basi si mwafrika safi, huyu kaoa mchina basi si mwafrika safi...

Kwaheri.
***********************************************************************************

3/20/2005

TUNAWASUBIRI WAKOLONI...WAJE HARAKA!

Tarehe 15 mwezi huu nilipata barua ya kusisimua sana toka kwa msomaji wangu ambaye pia ni rafiki yangu, ndugu Mloyi. Aliniandikia baada ya kuandika makala kuhusu kurudisha wakoloni nchini Tanzania. Nilipoisoma nilimtumia rafiki yangu mwingine mpambanaji akaisoma. Akaniambia kuwa nilipoandika makala kuhusu kurudisha wakoloni, nilikuwa natoa dira. Na ndugu Mloyi katika barua yake anatoa mikakati ya utekelezaji. Kwa ruhusa yake ninaanika barua yake wazi muisome:

Ndugu Ndesanjo,
Kabla sijasahau kukuambia, jina langu jipya litakuwa Molly Newman...Je watalipenda? Ninaanza kujitambilisha kwa jina hilo hata kama nitafika miaka sabini bado nitakuwa Newman, New mpaka lini? Labda wapinzani wawaondoe (wakoloni) kwa ujinga wao. Wakoloni watalipenda sana jina hilo, nitatubu mbele kwamba sikujipa jina la zamani, nilipewa na wazazi wangu na watanisamehe kama walivyomsamehe Adam kwa makosa ya Eva au Samsoni kwa makosa ya Delila. Hawawezi kuniadhibu ambaye sikutenda kosa.

Nitakaa nao mbele ya mungu mpya, watajali mama yangu anakula nini. Najua wapigania uhuru waliwafukuza wakoloni kwa sababu walifungwa na nguvu za giza, wao lilileta nuru mpya waliikataa.Utakuwa kiongozi wetu wa maisha, mgombea uraisi wa maisha kwani chama chetu kitakuwa na nguvu ya kugombea uraisi miaka yote. Uhakikishe wakija wasitoke tena, ila ndugu zao wanaowategemea wabaki hukohuko ili waweze kuwatumia fedha kidogo toka kwenye ikulu yetu, maana tutakuwa tumeiga ukarimu wao. Hujui na sisi pia tutakuwa tunawapa misaada zaidi ya wanayotupa wao, kuliko tunavyowapa sasa?

Tutakuwa binadamu wapya wastaarabu na gentle. Tutakuwa tunajiandaa kuwa weupe kama theluji, dhambi zetu zitatakaswa ili tuingie mbinguni. Weupe sio kwa mkorogo bali kwa utakaso wa neno lililo jipya kuliko la wana wa Farao tuliokuwa tunawapenda. Nimejua sasa kwanini nchi hii bendera yake haina rangi nyekundu. Ni mpango wa mungu mkuu. Unajua Mkwawa , Mangi na wengine walimpinga mungu mkuu ndiyo maana walilaaniwa wasikumbukwe kwenye bendera yetu, na wote watakaopinga mpango wetu watasahaulika kama manyani ya porini yanavyosahaulika.

Ndesanjo, lakini jina lako litatutia doa kwanini usiwe Nesto McChair utakuwa na jina linalotamkika hata raisi mpya hata pata tabu kulitamka. Nimeanza mazoezi ya kusahau kiswahili, nimeanza kusahau kuandika maneno ya kiswahili, juzy niliposoma makaler yako ya pili niliona una waopposer wengi sana. Ila ulimi wangu unanitia aibu kila nikijaribu kuongea kama yule buruda wa sunday school, naona niuchonge kabla siku haijafika na weusi uminizidi, nitapata taabu sana kusema mimi ni coloured sio chotara. Nimenunua suti ila joto linanisumbua sana , ila inanibidi nivumilie tu maana najua ninachotaka. Usijali sana tutafanikiwa tu.

Unajua sisi wenyewe bila hawa ndugu zetu hatuwezi kufanya kitu, hata wote tukisoma darasa moja kuanzia nursery hadi college bado tunakuwa na mapungufu, sio wao. Si unaona? Mkapa ana degrii na Schwazeneggar hana lakini uongozi wa Schwaznegger si mzuri kuliko wa Mkapa? Nani anampinga Schwaznegger kama sio uroho wa madaraka tu? Utandawazi utakuwa mzuri kwetu siku hizo sio kama sasa, angalia wazungu waliompinga Bush, na wenye kumuita Kichaka wakome kabla sijawashtaki. Wote sasa wanamuunga mkono, Iraq inajengwa, Iran itakuwa civilized kuliko wote na sisi sasa tutatolewa kwenye viota tufundiswe kuishi kwenye nyumba za kisasa zenye viyoyozi na matanuru ya kuingiza joto, sio utani tunahitaji joto hapa Dar.

Unajua wakija hawa sasa tutapata vitu kwa bei nafuu sana kama bure, angalia kwao maisha yalivyo rahisi sio kama sisi, tutaendelea sana. Tunawasubiri waje watufumbue macho tumechoka kuishi kwenye vibanda. Wapinzani wakijua niko mstari wa mbele kuwapinga si watanitafuta waniue mpaka niombe msamaha na kujiunga nao! Je wewe hautakuwa karibu kunisaidia nisijeingia kwenye laana kuu ya kukataa weupe? Nao watakubali niteseke wakati ni mtu mzuri kwao? Je watakuja na mabinti zao? Tutawaoa kama wao watakavyooa wetu , si unaona South Africa, tutapata jamii ya machotara.

Watoto wangu watakuwa weupe kama theluji hawatahitaji kutubu dhambi maana hawatakuwa nazo kama babu zao upande wa mama yao. Watakuwa na huruma ya hali ya juu, kamwe hawatavumilia kuona watu wanateseka, wengine wanatupwa kwenye bahari waliwe na papa au wengine kwenye minyororo wanapelekwa kufanyishwa kazi. Dunia yetu itakuwa nzuri sana. Hakutakuwa na dhambi, hata malaya hawatakuwapo tena maana watakuwa wamepewa jina jipya zuri. Watanipenda sana hata kama nitapata ajali nikiwahi kufanya ngono nje ya ndoa watasema nilikuwa nakimbia paparazzi kama Diana.
Kwaheri.
***************************************XXX****************************************

Hapo ndipo ukawa mwisho wa barua ya Mloyi.

MSOMAJI KANIAMBIA: YOU ARE A LEGEND "ON" YOUR OWN EYES

Kati ya wanaonirushia mishale ya sumu kuna bwana mmoja ambaye kama wengine anajificha nyuma ya mbuyu: hatoi jina lake halisi. Huyu bwana kaniachia ujumbe mara mbili kwenye kitabu changu cha wageni. Sijui kwanini kila mara anakuja kwenye blogu hii wakati anadai kuwa ninamkumbusha mwanafunzi wa kidato cha tano ambaye ndio wa kwanza kijijini kwao kwenda kidato cha tano na sita. Huyu bwana katumia Kiswahili na Kiingereza kunirushia mishale hiyo. Huenda alitaka kuonyesha kuwa naye yumo. Ndio wale wale. Unakuja kwenye blogu ya kiswahili, unaniandikia ujumbe mimi ninayeongea kiswahili unaingiza kiingereza cha hapa na pale. Labda alikuwa anaweka msisitizo maana kuna wanaodhani kuwa jambo likizungumziwa kwa kiingereza linakuwa na nguvu zaidi. Lakini jambo nisiloelewa ni hili: huyu bwana hiki kiingereza chenyewe kinampa tabu lakini bado anaking'ang'ania. Jamani, kwanini Waafrika tuko hivi? Ngoja niweke sentensi zake za kiingereza alizoniandikia na kumfundisha jinsi hii lugha ya watu wasiomthamini inavyotumiwa.
Maneno yake: You consider yourselves as legends, but you are legends on your own eyes.You reminds me of those form five students who were the first from their village to attend high school, and thterefore thought the journey ends there.
Uchambuzi wangu: kama ananizungumzia mimi basi hana haja ya kusema "yourselves" au kusema "legends." Pia sio sahihi kusema "you reminds," hakuna haja ya kuweka "s" kwenye neno "remind." Angeweka "s" kama angetumia He/She au It. Hii ni sawa na mtu kusema, "You goes to school." Halafu ni vyema kusema, "...a legend in your own eyes," yaani angetumia "in" badala ya "on," pale aliposema, "...legends on your own eyes."
Kama ningekuwa na anuani yake ningemwandikia ili iwe siri yake. Lakini kwakuwa sina anuani yake inabidi niweke hapa maana najua atarudi. Na pia kwakuwa hajaacha jina, hakuna atakayejua anayekosolewa ni nani. Kwahiyo huyo mtu asijisikie vibaya. Ningekuwa na anuani yake ningempa somo zaidi la lugha hii kutokana na makosa mengine kwenye ujumbe wake ambayo sina muda wa kuyajadili.
Kingine alichonishangaza huyu bwana ajifichaye nyuma ya mbuyu ni kuwa ameanza ujumbe wake kwa kusema, "Inaonekana waafrika wakioa wazungu au waarabu wanasahau uafrika wao." Nimeshindwa kuelewa anamzungumzia nani hapo. Kama ananizungumzia mimi basi nitapenda kumfahamisha kuwa mimi sijaoa mzungu au mwarabu. Kuhusu Waafrika kusahau Uafrika wao, kusahu huko kunaanza pale unapowasiliana na Mwafrika mwenzako ambaye mnazungumza lugha moja (Kiswahili), lakini unakimbilia Uingereza kwenda kuokota maneno ya kiingereza ya kuwasiliana na nduguyo.
Nitapenda kurudia kusema kuwa watu wanaonirushia mikuki ya sumu nimewapa uwanja. Badala ya kuweka mistari miwili, mitatu kwenye kitabu cha wageni au kwenye anuani yangu ya barua pepe, waandike kwa mapana na marefu hoja zao. Mpambano wa fikra ni mtamu sana. Hasa tunapokuwa tunazungumzia masuala ya nchi yetu na bara letu, utaifa, uzawa, utamaduni wa Mwafrika, ukoloni mamboleo, dini za uongo za kuja, ubeberu, umuhimu wa Kiswahili, haki za binadamu, n.k.

NIMERUDI: MAENDELEO NI SAYANSI

Nilipotea kidogo bila taarifa. Nilikabiliwa na mambo mbalimbali (safari, mikutano, ulezi, n.k.). Sasa nimerudi. Nina makala zaidi toka kwa Freddy Macha, Padri Karugendo na zangu. Nitaziweka. Pia kuna barua kadhaa toka kwa wasomaji ambazo nitaziweka hapa mzisome. Kuna mengi mapya, mishale ya sumu bado ninaikwepa. Waafrika tumepoteza kabisa nafsi zetu kiasi ambacho akitokea mtu kutuonyesha njia anaonekana kuwa ni adui. Tunataka kunyanyua mapanga kutetea manabii toka nchi za mbali huku tukiwa hatujui hata manabii toka kwenye vijiji vyetu. Kwanza huu ugonjwa wa akili lazima tuutafutie dawa. Ugonjwa wa kudhani kwamba Afrika nzima hakuna manabii. Manabii wanatoka tu Uyahudini na Uarabuni. Ugonjwa wa kudhani kuwa Afrika nzima haina maeneo "matakatifu" ndio maana watu wanatumia mamilioni kwenda kubusu jiwe Uarabuni au kuhiji Yerusalemu au Roma. Ugonjwa wa kudhani Abdalah ni jina la Kiislamu na George (ambaye huitwa Joji) ni jina la Kikristo. Ugonjwa wa kuamini hekaya za Kiyahudi kuwa dunia ilianza kati ya miaka 5000 - 7000 iliyopita. Lazima tukomeshe gonjwa hili baya kabisa linaloharibu akili na nafsi za Waafrika ambao hadi leo tumeshindwa kabisa kujitawala kutokana na kutojijua. Sirikali zetu zimejaa wezi. Wanachojua ni kuomba. Wanaita "misaada." Hivi sasa Afrika nzima viongozi wamejiunga na kwaya inayoimba pambio la "utandawizi" na "soko holela." Hawa nao lazima waondolewe. Bara limejaa huzuni. Ukimwi unatumaliza. Ujinga unaongezeka. Mauaji yasiyo na mbele wala nyuma yanasikika kila kukicha. Visima vinakauka. Watoto hawaendi shule kwa kukosa ada. Vifo vya magonjwa yanayotibika vinaongezeka. Umri wa kuishi unazidi kupungua. Ni tabu tupu. Ni kilio. Yote haya lazima yakome. Wako wanaodhani kuwa Afrika haitakaa iende mbele. Hawa ni wale wanaodhani kuwa maendeleo ni muujiza. Sio muujiza. Ni sayansi. Sayansi hii inaanza kwa kusafisha fikra zetu na kusafisha viambaza vya utawala vilivyojaa wezi ndani ya suti na majina ya kuazima. Kazi hii ni yangu na yako.

NIMERUDI

Nilipotea kidogo bila taarifa. Nilikabiliwa na mambo mbalimbali (safari, mikutano, ulezi, n.k.). Sasa nimerudi. Nina makala zaidi toka kwa Freddy Macha, Padri Karugendo na zangu. Nitaziweka. Pia kuna barua kadhaa toka kwa wasomaji ambazo nitaziweka hapa mzisome. Kuna mengi mapya, mishale ya sumu bado ninaikwepa. Waafrika tumepoteza kabisa nafsi zetu kiasi ambacho akitokea mtu kutuonyesha njia anaonekana kuwa ni adui. Tunataka kunyanyua mapanga kutetea manabii toka nchi za mbali huku tukiwa hatujui hata manabii toka kwenye vijiji vyetu. Kwanza huu ugonjwa wa akili lazima tuutafutie dawa. Ugonjwa wa kudhani kwamba Afrika nzima hakuna manabii. Manabii wanatoka tu Uyahudini na Uarabuni. Ugonjwa wa kudhani kuwa Afrika nzima haina maeneo "matakatifu" ndio maana watu wanatumia mamilioni kwenda kubusu jiwe Uarabuni au kuhiji Yerusalemu au Roma. Ugonjwa wa kudhani Abdalah ni jina la Kiislamu na George (ambaye huitwa Joji) ni jina la Kikristo. Ugonjwa wa kuamini hekaya za Kiyahudi kuwa dunia ilianza kati ya miaka 5000 - 7000 iliyopita. Lazima tukomeshe gonjwa hili baya kabisa linaloharibu akili na nafsi za Waafrika ambao hadi leo tumeshindwa kabisa kujitawala kutokana na kutojijua. Sirikali zetu zimejaa wezi. Wanachojua ni kuomba. Wanaita "misaada." Hivi sasa Afrika nzima viongozi wamejiunga na kwaya inayoimba pambio la "utandawizi" na "soko holela." Hawa nao lazima waondolewe. Bara limejaa huzuni. Ukimwi unatumaliza. Ujinga unaongezeka. Mauaji yasiyo na mbele wala nyuma yanasikika kila kukicha. Visima vinakauka. Watoto hawaendi shule kwa kukosa ada. Vifo vya magonjwa yanayotibika vinaongezeka. Umri wa kuishi unazidi kupungua. Ni tabu tupu. Ni kilio. Yote haya lazima yakome. Wako wanaodhani kuwa Afrika haitakaa iende mbele. Hawa ni wale wanaodhani kuwa maendeleo ni muujiza. Sio muujiza. Ni sayansi. Sayansi hii inaanza kwa kusafisha fikra zetu na kusafisha viambaza vya utawala vilivyojaa wezi ndani ya suti na majina ya kuazima. Kazi hii ni yangu na yako.

3/16/2005

WIZI WA URITHI WA AFRIKA

Waafrika bado wanapambana kurudisha mali na urithi wao ulioibwa na wakoloni na wavamizi miaka mingi iliyopita. Wezi hawa ambao wanajiita wakristo na dini yao ina amri isemayo usiibe (au ukiiba ikitokea umekamatwa basi rudisha) walipoingia afrika waliiba kila walichoona kinawafaa. Sasa chuo kikuu chenye heshima cha Edinburgh kimekataa kuachia vitabu vilivyoibwa toka Ethiopia. Waethiopia wamekuja juu wanataka mali zao, mijaa hii inakatalia. Naona itabidi tumfuate Joji Kichaka ili tuvamie nchi zenye mali zetu na kuzitwaa. Kongoli hapa usome habari hiyo. Habari zaidi za urithi wa Ethiopia ulioporwa hapa.

KWANINI WATANZANIA HAWAFUNGI MIKANDA?

Ninapokutana na wakoloni wanaokwenda Tanzania kutembelea wanyama...(ndio, sio kutembelea binadamu. Wanyama wa Afrika wanapendwa zaidi ya Waafrika), katika mambo ambayo hawaelewi ni tendo la madereva kuendesha magari bila kufunga mikanda. Watalii wana akili fupi sana. Kitu gani wanashindwa kuelewa? Hawajui kufunga mkanda ukiwa ndani ya gari ni kujitakia kifo? Ndio maana mimi hadi leo sifungi mkanda. Polisi wakinisimamisha ninawasomesha. Nawaambia kwenye utamaduni wetu usalama ni kutokufunga mkanda.
Wananiuliza, "Kuna sababu gani ya msingi inayowafanya msifunge mikanda?" Nawaambia jibu ni rahisi sana: Ukifunga mkanda wakati wa ajali utashindwa kuruka! Full Stop!

3/13/2005

PADRI KARUGENDO NA MIAKA 10 YA ULINGO WA BEIJING

Nimeweka makala mpya ya Padri Privatus Karugendo iitwayo Miaka 10 ya Ulingo wa Beijing. Makala hii ambayo inauliza maswali ya msingi kuhusu masuala ya jinsia inapatikana kwa kubonyeza hapa. Kumbuka kuwa makala zake nyingine ziko katika safu yake, Kalamu ya Padri Karugendo, iliyoko chini ya kona ya makala zangu na Freddy Macha zilizoko upande katika blogu hii.

LAZIMA NGOZI NYEUPE IINGIE IKULU

Nimeweka makala mpya ambayo niliandika kwa ajili ya safu yangu katika gazeti la Mwanchi nchini Tanzania. Makala hii inazidi kujenga hoja yangu kuwa tuhahitaji wakoloni kwa mara ya pili na ya mwisho (ya mwisho maana safari hii wakishaingia hawatatoka tena). Inaitwa: Lazima Ngozi Nyeupe Iingie Ikulu. Bonyeza hapa uisome. Makala zangu nyingine ziko katika kona ya makala zangu, upande wa kulia wa blogu hii, chini ya picha yangu.

ONYESHO LA "EYES WIDE OPEN"

Onyesho la "Eyes Wide Open" linaloendeshwa na American Friends Service Committe ni aina fulani ya sanaa iliyochanganyika na harakati za kupinga vita na matumizi ya nguvu katika kusuluhisha migogoro duniani. Bonyeza hapa utazame habari na picha za onyesho hilo. Ukifika hapo bonyeza kidude cha "Watch the Movie" ili kutazama filamu fupi ya gharama ya vita.

ALIBADIRI

Bwana mmoja kaniandikia. Anasema kuwa madai kuwa "watumishi" wa Mungu huwa wanaombea watu wanaowasimanga au kupinga imani zao hayana msingi wowote. Akasema kuwa mbona viongozi wa nchi za Kiislamu wanaomchukia Joji Kichaka wasimsomee alibadiri awe kichaa? Mimi nami nikaongeza, mbona Wapalestina wasiwasomee Waisraeli na kiongozi wao Sharon alibadiri ili wote wawe vichaa na wao (Wapalestina) waweze kutwaa nchi yao?

3/11/2005

KARUGENDO: UKRISTO UMEWAPOTOSHA WAAFRIKA

Nimeweka makala mpya mbili za Padri Privatus Karugendo. Makala zake kama mnavyojua zinapiga msasa fikra zetu. Makala ya kwanza inasema: Ukristo Umepotosha Waafrika. Bonyeza hapa uisome. Na ya pili inasema: Huu Sio U-Tanzania. Bonyeza hapa uisome. Makala zake nyingine ziko katika kona yake iitwayo Kalamu ya Karugendo iliyoko mkono wa kulia chini ya makala zangu na za Freddy Macha.

KISWAHILI CHA KENYA KATIKA KISA CHA JAFARI

Nimeweka kisa kimoja kitamu sana toka kwenye mkusanyiko wa hadithi wa Freddy Macha utakaochapwa hivi karibuni nchini Tanzania uitwao Mpe Maneno Yake. Kisa hiki kinaitwa Kisa cha Jafari. Kisa hiki kinasimuliwa kupitia wazungumzaji ambao wametoka Kenya na wanaishi nchini Uingereza. Kisome ujifunze kiswahili cha Kenya. Bonyeza hapa. Kazi zaidi za Freddy ziko katika kona yake hapa ndani, upande wa kulia, chini ya makala zangu.

UNAFAHAMU AFROGEEKS?

Wale wafuatiliaji wa masuala ya teknolojia mpya za mawasiliano: Tazama Afrogeeks 2004 hapa. Na Afrogeeks 2005 hapa.

NUKUU YA MWIZI MOBUTU SESE SEKO

Rafiki yangu kanitumia nukuu ya mwizi aliyekuwa akishirikiana na nchi zinazojiita za kidemokrasia kama Marekani katika wizi wake wa mali ya Wakongo, Mobutu Sese Seko:

"If you steal, do not steal too much at a time. You maybe arrested. Steal cleverly (yiba na mayele), littleby little." -- President Mobutu Sese Seko of Zaire inan address to party regulars in 1991.

MANENO YA WOLE SOYINKA

Rafiki yangu kanitumua maneno haya toka kwenye kalamu ya Wole Soyinka.

"All symbols of military authority must be removed from ourmidst. Those arrogant photographs that desecrate public spaces, schools, hospitals, offices, even courts of justice. Street names, also, change them all. Remove them. Remove them by stealth, remove them openly, by cunning, remove them by bribery, remove them forcibly, remove them tactfully, use whatever method is appropriate, but remove them. I call on all who are resolved to play a role in our mutual liberation to participate in this exercise of psychological release, or mental cleansing and preparedness..." - Wole Soyinka (1996)

NAKUBALIANA NAWE KITURURU

Kitururu (sifahamu jina lako la kwanza) wa Tanganyika (kama ulivyoeleza mwenyewe) ninakubaliana kabisa na maneno yako. Umenitumia ujumbe huu hapa chini ukinukuu maneno niliyoandika hapa bloguni juzi:

Nimependa sana blog yako. Lakini katika maandiko yako hakuna hoja dhaifu ulioiandika kama hii hapa (chini hapo ananukuu maneno yangu):
Rafiki yangu wa karibu kanionya niache kuandama "watumishi" wa mungu maana wanaweza kuniombe! Naona anaweza kuwa anasema kweli. Itabidi nipunguze kidogo. Kidoooooogo. Sitawagonga sana.

+++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++++

Ninakubaliana nawe. Na kwa msingi huo nitapambana kisawasawa na watu wanaojiita "watumishi" wa mungu. Hasa wale wanaotuhadaa kwa kutuambia kuwa tukubali kuteseka hapa duniani chini ya sirikali za kidhalimu kwani tutapata raha ya milele tukifa. Wanakubali tubebe chakula kichwani huku tunalia njaa. Tunaweza kuanza kupata hiyo raha ya ahera hapa duniani kama wanavyoipata wao. Kwahiyo, ndugu Kitururu. Sitapunguza hata kidogo.

NINAKWEPA MIKUKI YA SUMU

Kuna mikuki ya sumu inarushwa kunielekea. Wako wanaorusha kwenye anuani yangu binafsi na wengine wanarusha kupitia kitabu cha wageni. Nadhani kuna hoja ninazotoa ambazo zinawaiingia baadhi yetu kama kisu cha machinjioni. Na kama ni hivyo, basi wajue hiyo ndio gharama ya kujikomboa. Ushauri ambao naweza kuwapa kwa sasa ili wasiwe na ghadhabu kama mkizi, ni huu: Kama kuna jambo hukubaliani nalo, jibu kwa hoja. Hoja kwa hoja. Hoja bin hoja. Nguvu ya hoja. Nipe nikupe. Hakuna mtu yeyote ambaye atanitumia chochote alichoandika kupinga au kusahihisha jambo lolote ninalosema nami niache kuweka wazi kila mtu asome. Kaa chini, andika, nitumie. Nitaweka hapa kila mtu asome. Nawapa uwanja. Kipenga kimelia. Kama kuna haja ya kujibu nitakujibu. Ninaheshimu uhuru wa mtu kutoa maoni. Awe anakubaliana nami au hakubaliani. Sitakutukana, au kutupa kazi yako uliyonitumia jalalani, au kukuita majina ya ajabu ajabu eti kwakuwa sikubaliani na unayosema. Nguvu ninayotumia sio ya misuli, sio ya matusi, sio ya vitisho, bali hoja. Hoja, falsafa, maarifa, elimu, historia...Nawe pambana nami kwa hoja, falsafa, historia, n.k. na sio vitisho au kutukana. Vitisho na maneno machafu ndio naita mikuki ya sumu. Hii nimeikwepa. Changamoto ninayotoa ni hii: usijifiche katika majina ya uongo na mistari miwili, mitatu ya vitisho au maneno machafu kwenye kitabu cha wageni au anuani yangu. Toka nyuma ya mbuyu tupambane kwa hoja. Toka nyuma ya pazia. Kama nimesema 1+1= 5, ukibisha usiseme tu: "Hujui unalosema. Funga mdomo." Hapo unakuwa unapoteza muda muhimu sana maishani. Kaa chini useme kwanini 1+1 sio 5. MMENIELEWA NINYI AKINA NANI HII? Kama mmetumwa, basi waambieni hao wanaowatuma wajipange tena vizuri. Nimeandika haya machache ila mnajua kuwa barua nilizowajibu nimeandika mengi zaidi.
Kuna baadhi ambao wameudhika kwa sababu ya hoja zangu za kisiasa. Hawa tuwaache kwanza. Kuna hawa wameudhika kutokana na maoni yangu kuhusu dini. Hawa ndio wana ghadhabu zaidi. Usiudhike. Bado hujasikia kitu. Ndio mwanzo tu. Kule Moshi enzi za kwenda sinema ukumbi wa Plaza pale Moshi mjini tulikuwa tukiwa na msemo huu, "Hiyo ni trela. Bado picha." Nami nawaambia ndugu zangu waumini wa dini za kuja. Nyie mnapotuita sisi tunaohubiri dini za asili au tusio na dini kabisa kuwa ni wapagani, makafiri na majina mengine ya ajabu, kwani tunawatishia au kuwatukana? Tunajipanga na kuja na hoja. Mnapohubiri na kusema kuwa watu wasioamini hivyo vitabu vyenu viwili watakwenda... sijui mnaita motoni, mbona hatupandishi jinamizi la hasira?
Salman Rushdie alipotumia haki yake ya kutoa maoni yake, mzee mmoja kule Iran akatangaza fatwa. Auawe! Kufuru hiyo! Baadhi ya waislamu Tanzania wakashangilia. Wakataka kitabu kipigwe marufuku kuingia nchini. Kikapigwa marufuku (ingawa kiliingia kwa njia za panya na nilikisoma wakati ule kilipotoka). Lakini sirikali ilipoamua kupiga marufuku kitabu cha Hamza Mustapha Njozi kiitwacho Mwembechai Killings and the Political Future of Tanzania (bonyeza hapa ukisome), waislamu hao hao walioshangilia kutolewa kwa amri ya kuuawa kwa Salman Rushdie na kupigwa marufuku kwa kitabu chake kuingizwa Tanzania, walinyanyuka wakitaka sirikali iruhusu kitabu hiki kuingizwa nchini na kuuzwa. Mkuki kwa nguruwe? Yaani kama kitabu kinaandikwa kinatetea dini yako unakuja juu na kutaka haki za binadamu na kikatiba ziheshimiwe, lakini kitabu kikiandikwa kikiwa na dalili za kupinga imani yako unakuja juu kutaka haki hizo zikanyagwe. Huu ndio tunaita unafiki wahedi. Lazima ukome. Tutaukomesha. Mtusomee ile mistari yenu mnayotumia kutishia watu au mkatusalie huko kwenye majumba ya ibada za unafiki...mfanye lolote. Hatutanyamaza. Kwenye wimbo wa Ride Natty Ride, kuna mstari Bob Marley anasema, "moto unawaka na hakuna wa kuuzima." Ndio kinachotokea hivi sasa. Vijana wanaamka. Wanafungua vitabu vya historia. Wanaongea na mababu zao kabla hawajaaga dunia na kuondoka na hazina ya maarifa. Wanatafiti. Wanaandika. Wanaimba. Wanatunga. Wanaongea. Kwenye wimbo mwingine wa Bob Marley wa Talking Blues anasema, "...sasa tunajua kuwa mhubiri anadanganya." Kweli tunajua hilo. Tunajua, kwa mfano, Kakobe alidanganya nchi nzima mwaka 2000 kuwa kaongea na Mungu. Tunajua mashehe ni waongo. Wanashika tasbihi na kuvaa kanzu na kupaka ndevu hina...wanachanganya uislamu na Uarabu. Uislamu ni unyenyekevu mbele za mungu, hauna maana ya kuiga utamaduni wa Kiarabu. Kuchukua majina yao, staili ya ya mavazi, n.k. Wote hawa wajue moto unawaka na hakuna wa kuuzima. Kwenye wimbo mwingine wa Jah Lives Bob Marley anasema kuwa uongo unaweza kuwa kosa la jinai ila sio dhambi. Kwahiyo mnaweza kwenda kule kwenye mchezo wa kuigiza katika ukumbi wa maonyesho kabambe uitwao bunge, mkaandika sheria za kufanya kusema ukweli ikawa ni kosa la jinai. Lakini mnaweza kuandika sheria ya kufanya ukweli kuwa ni dhambi?
Mimi nasema kitabu cha Salman Rushdie kisomwe na mtu yeyote. Kiuzwe kokote kule. Kitabu cha Njozi kisomwe na yeyote. Kiuzwe Tanzania nzima na hata dunia. Hakuna sababu ya kuzuia vitabu hivi viwili. Bonyeza hapa usome kitabu cha njozi.
Kwahiyo kuna watu hawajazoea kupingwa kwa hoja. Wanataka tu watangaze "ukweli" wao, wakisikia ukweli tofauti na ule wao ulioletwa na majambia na bunduki wanakuja juu. Tuwapa hoja mishipa inawatoka kwa hasira. Tulieni. Ndio mwanzo wa safari ya ukombozi. Kuna watakaolia, kuna watakaoacha midomo wazi kwa mshangao, kuna watakaoshangilia, kuna watakaogutuka, n.k. Tutambue kuwa ukombozi wa nchi na bara letu, iwe ni kwenye nyanja ya uchumi, siasa, michezo, elimu, jamii, sanaa, n.k. lazima uanze kwanza kwenye fikra. Usiende mbali sana. Usianzane na mimi. Usikimbilie kwenye vitabu sijui vitakatifu na vitukufu. Anza kwenye fikra. Anza na wewe binafsi. Fikiria nje ya kasha. Fungua kasha, toka nje. Weka matundu, chungulia nje. Kasha halina kufuli. Mlango uko wazi, wewe tu hutaki kutoka. Kwanini unang'ang'ania kukaa ndani? Ukweli sio ukweli kwakuwa eti watu wengi wanaufuata. Ukweli ni uweli. Hata kama hakuna binadamu yeyote duniani anayeufuata, ukweli unabaki kuwa ukweli. Usiogope kuhoji mambo. Hoji kila kitu. Hoji kila mtu. Hoji dini. Hoji itikadi. Hoji elimu. Hoji historia. Hoji maandiko. Hoji. Ndani ya kasha mmebanana sana. Huoni tabu ya kuhema? Toka nje, jinyooshe, tazama jua, Uko huru. Huu ni wakati wa fikra sahihi. Mtazamo sahihi. Matendo sahihi. Bila fikra sahihi mwili wako unakuwa tu kama gurudumu la gari ambalo linakwenda kule mwendesha gari anakotaka.
Kwa wale wanaoniandama kutokana na makala zangu za hivi karibuni za siasa, nina maneno machache ya kuwaambia: Ujumbe ninaoutoa katika hoja yangu ya kutaka Tanzania itawaliwe tena ni sawa na msemo wa Yesu aliposema, "Nimekuja ili wawe na macho ila wasione. Wawe na masikio, wasisikie..." Hoja yangu hii ya kutaka wakoloni ni fumbo. Werevu wameshafumbua siku nyiiiingi.

3/10/2005

UTAKUWA WAPI MACHI 15 MWAKA HUU?

Kuna filamu ya kwenye mtandao wa kompyuta inakuja na kitu kinaitwa "webisodic" (kama kwenye episodic). Hapo Machi 15 filamu hii itaonyeshwa kwa mara ya kwanza na siku hiyo itakuwa bure (baada ya hapo utapaswa kulipa senti 99 kwa kila "webisode"). Bonyeza Hapa. Barua ya watengeneza filamu kwa vyombo vya habari iko hapa.

3/09/2005

VIDEO KUHUSU WANABLOGU LUNINGA YA ABC

Katika kipindi chake cha Nightline jana usiku, kituo cha luninga cha ABC kilikuwa na habari kuhusu wanablogu (Inside the Life of Bloggers). Bonyeza hapa utazame video ya kipindi hicho. Tazama upande wa juu kulia utaona kiunganishi cha video hiyo.

CITEULIKE.ORG: KWA WANATAALUMA

Watu walioko vyuoni, walimu, na wengine wanaosoma majarida ya kitaaluma wanaweza kuwa na maktaba yao katika webu nzuri sana ya CITEULIKE.ORG. Katika tovuti hii sio tu unaweza kuweka machapisho ya kitaaluma kwenye maktaba yako mwenyewe, tena bure, bali pia unaweza kutembelea maktaba za wengine kuona wanasoma nini. Nimeipenda mno. Bonyeza hapa.

URAIS SIO KUBEBA ZEGE

Bwana John Malecela amewajia juu wale wote wanaodai kuwa amezeeka hivyo hafai kuwa rais. Anasema acheni kumwandama kwani, "Urais sio kubeba zege!"

KESI KUHUSU BLOGU

Kuna kesi ninayoifuatilia kuhusu wanablogu ambayo inazua maswali kuhusu uhusiano wanablogu na taaluma ya uandishi wa habari. Soma hapa.

NIMEPEWA ONYO

Rafiki yangu wa karibu kanionya niache kuandama "watumishi" wa mungu maana wanaweza kuniombe! Naona anaweza kuwa anasema kweli. Itabidi nipunguze kidogo. Kidoooooogo. Sitawagonga sana.

NIMTUME NANI? - II

Huu ni muendelezo wa Nimtume Nani sehemu ya kwanza ambayo sikuimaliza maana nilirukia kwenye mambo mengine. Nilikuwa nauliza kwa niaba ya mungu: Nimtume Nani? Swali hili linasubiri majibu huko mbinguni. Mwaka 2000 alitumwa Kakobe. Alitumwa na mungu wake anayempa uwezo wa kuponyesha watu ila hampi busara za kwenda kuponyesha mahospitalini badala ya kuwasubiri waende kanisani kwake, ambako pia hupeleka sadaka. Tena ili sadaka ziwe nyingi, waumini wake hawatakiwi kupanda mabasi maana nauli itapunguza mshiko wa mungu.
Unajua zamani nilikuwa nikiamini kuwa ni kweli sadaka zinakwenda kwa mungu. Eti wanasema, "Mtolee Bwana." Wewe nani kakwambia mungu anataka pesa? Kama mungu alikuwa anachukua hizo pesa vitambi na magari ya kifahari ya "watumishi" wa mungu vingepatikanaje? Bila kusahau misalaba mikubwa mikubwa wanayovaa shingoni...sijui inauzwa wapi. Nami nataka wangu. Si tuliambiwa kila mtu atabeba msalaba wake mwenyewe? Kuna walioelewa kuwa Yesu alimaanisha ubebaji wa msalaba ndani ya nafsi zetu, na wengine wakadhani ni kubeba misalaba juu ya kifua. Wahubiri misalaba yao ni mikubwa zaidi ya waumini kumaanisha kuwa wao ni wateule wa mungu.
Nimtume Nani? Mungu wa Waisraeli auliza.
Kwanza, hivi Watanzania wanahangaika na nini na Mungu anayesema kuwa wateule wake ni Waisraeli? Au wewe ndugu yangu Mbena, Mnyaturu, Mmasai, Mkinga, Msukuma, Mchagga, Mzanaki, n.k. umeshakuwa Muisraeli? Kwani si tunaambiwa kuwa Waisraeli hawa wana makabila 12 tu ambayo ndio yenye viti mbinguni na idadi yake, 144,000, imetajwa kabisa kwa mujibu wa kitabu kisichoeleweka vizuri cha Ufunuo? Usishangae idadi ya wateule kuwa ndogo hivyo, njia ya kwenda kule tumeambiwa na watu ambao hawajawahi kufika huko na hawatafika kuwa ni nyembamba! Hivi wewe kabila lako katika 12 ya wateule wa mungu ni lipi? Lazima utakuwa na makabila mawili, la kuzaliwa na hili la kujipenyeza.
Najua Tanzania kuna makabila zaidi ya 120, mbinguni viti ni vya makabila 12...mbona kutakuwa na kasheshe hapo? Mambo ya kuingilia miungu wa wengine na kumtupa wako yatatutokea puani. Amri ya kwanza inasema usiwe na miungu wengine ila mimi. Haiishii hapo. Sababu ya kuwa na mungu huyo na sio wengine inatolewa: "... maana nilikutoa utumwani Misri...."
Huyo mungu hapo haongeni nami maana ninajua historia ya watu wangu. Hatujawahi kuwa utumwani Misri. Lazima anaongea na watu wengine. Jamani, Wachagga tumewahi kuwa utumwani Misri kisha Yehova akatupeleka nchi ya ahadi? Labda makabila mengine Tanzania. Ila Wachagga nimesoma historia yao hatujawahi kuwa na mtu anaitwa Musa. Kwanza jina hilo sio la Kichagga.
Nimtume Nani? Mungu wa wayahudi anauliza. Mwaka 2000 alimtuma Kakobe kutuambia kuwa Mrema atakuwa rais. Uchaguzi ukafanyika Mrema akashindwa vibaya sana. Ahadi ya mungu kupitisha mtumishi wake aendeshaye gari la kifahari huku waumini wake wakitakiwa kutembea kwa miguu haikutimia. Huenda shetani aliingiza mkono wake kwenye uchaguzi. Ndio hoja ya baadhi ya watu. Wanasema, "Shetani anafanya kazi usiku na mchana kuharibu kazi ya mungu." Kwahiyo shetani alitumia wezi wa kura kuharibu unabii wake. Kama nitakubaliana na hoja hii, itabidi nikubali kuwa shetani ana nguvu kushinda mungu maana anaweza kuzuia ukamilisho wa ahadi/unabii wa mungu kwa wanadamu.
Mwaka huu atatumwa nani? Pengo? Sidhani. Pengo anaongoza kanisa linalodai kuwa bikira Maria alikuwa bikira maisha yake yote wakati alizaa watoto (nduguze Yesu). Hawezi kutuma waongo. Pengo yuko kwenye kanisa linalokataza wanawake kuhubiri. Hawezi kutuma wabaguzi wa kijinsia. Pengo yuko kwenye kanisa linalokataza wanaume kuoa na kuwaacha waharibu watoto wadogo wanaopamba mimbara za kanisa. Hawezi kutuma wanaoshindana na kanuni za maumbile na baiolojia.
Au atatumia kanisa la Kiluteri? Majuzi maaskofu wa Kiluteri wametwangana makonde. Kanisa liko kwenye mgogoro mkubwa kuhusu uongozi, mali, teolojia, n.k. Hakuna mtu mwenye nafasi ya kutumwa. Kanisa la Kiluteri linadai kuwa kuna kitu kinaitwa dhambi ya asili...uongo mkubwa huu.
Au labda safari hii atatumwa Muislamu.
Jamaa mmoja kaniambia kuwa tayari mtu keshatumwa. Tena Shekhe. Shekhe Yahya Hussein. Mtabiri mkuu Afrika Mashariki na Kati. Kasema rais mpya atakuwa ni binadamu. Atakuwa na upele (alimaanisha chunisi?). Atachaguliwa Oktoba mwaka huu. Atakuwa na nywele. Atazunguka nchi nzima kupiga kampeni. Atakuwa anajua kusoma na kuandika (basi hatakuwa Mrema!). Atakuwa anapenda kuvaa vizuri....utabiri mkali kweli huu!
Shekhe Yahya huwa ananifurahisha pale anaposema, "Kutakuwa na migogoro ya kisiasa huko Mashariki ya Kati." Jamani, kama huo ni utabiri basi hata mimi basi ninaweza kuwa mtabiri. Ngoja nitabiri: Waafrika wengi watakufa kwa ukimwi, kutakuwa na mgogoro wa kisiasa Lebanoni, Tanzania itafanya uchaguzi mwaka huu, Zanzibar kutakuwa na ghasia za hapa na pale, Marekani itaendelea kuikalia Iraki, Irani na Marekani zitagombana, uhusiano wa Korea ya Kaskazini na Marekani hautakuwa mzuri, "Babu" wa Mlingotini atakuwa na wageni wengi kabla ya Oktoba, wakulima Tanzania wataendelea kutumia jembe la mkono mwakani, Tanzania, Kenya, na Nigeria zitatawaliwa na rushwa...
Swali letu: Nani atatumwa mwaka huu? Kakobe ameshasema akitumwa tena hakubali. Hataki tena kurudia aibu ile ya 2000.

MAHESABU YA MWIZI WA TANZANIA OKTOBA MWAKA HUU

Rafiki yangu wa karibu ambaye ni mwana uchumi, baada ya kusoma makala yangu hii hapa iitwayo TUBINAFSISHE IKULU, ameamua kunipa mahesabu yatakayosaidia kupata rais au mwizi (kutegemea na mtazamo wako) kupitia moja ya mapendekezo niliyotoa kwenye makala hiyo. Huu hapa chini ndio ujumbe wake:
Baada ya kusoma makala yako ya kubinafsisha ikulu nimeona kwamba pendekezo ambalo litafanyika ni lakwanza; yaani kuwa na rais mwislamu na mkristo. Litafanya kazi kama hivi: Rais akiwa Mwislamu makamu wake ni Mkristo. Sasa mahesabu ni kama ifuatavyo:
1. Mwislamu+Mwislamu = haiwezekani
2. Mkristo +Mkristo = Haiwezekani
3. Mwislamu+ Mkristo= Inawezekana.

Sasa hesabu zitafanya kazi kama hivi:Kwa vile Kikatiba ni lazima Rais akitoka bara makamu atoke Zanzibar; Kama Rais atatoka Bara ni Lazima awe Mkristo kwa vile Zanzinbar hapatakuwa na Mkristo wakuwa makamu wa Rais. Kama Rais atatoka Zanzibar ambapo ni mwislamu basi makamu toka bara ni lazima awe Mkristo. Kwa mantiki hiyo basi kuna uwezekano kuwa mgombea yeyote kutokaBara atakuwa Mkristo ili mgombea mwenza toka Zanzibar awe mwislamu. Kama atatoka wa urais visiwani basi makamu toka bara ni mkristo.
Huu ndio uwezekano kwa majina: Kikwete Nje Kwa mantiki ya uislamu. Siyo rais wala makamu. Salim A. Salim ana nafasi kwa mantiki hii ya dini. Nikuchefue zaidi Sumaye na Malecela wanaweza kuwa na nafasi katika mantiki hii. Nimefikiria haya mahesabu usiku nikaona nikushirikishe unipe maoni yako kwa mantiki hii finyu ya udini.

3/07/2005

NIMTUME NANI?

Mwaka 2000 alitumwa Mhubiri Kakobe. Hatujui kilichotokea. Hatujui kama mungu alibadili mawazo akasahau kumwambia Kakobe au kutuma mtumishi mwingine. Hatujui kama Kakobe hakusikiliza ujumbe kwa makini. Tunachojua kwa uhakika wa asilimia 600 ni kuwa Augustine Lyatonga Mrema hakuwa rais wa Tanzania.

Nakumbuka nilikutana na wananchama wa TLP wakaniambia kuwa Mrema atakuwa rais. Nikawauliza, "Mmejejuaje?" Wakasema kuwa Kakobe ametangaza. Na kwa kuwa Kakobe ni mtumishi wa mungu mwenye miujiza mingi, lazima ana mawasiliano ya moja kwa moja na mungu. Na mungu huyo ambaye anaponyesha wagonjwa pale Mwenge, jijini Dasalama huku wagonjwa wa matatizo ya akili wakiteseka Muhimbili...wagonjwa hawa kwakuwa wanaumwa akili hawawezi kuamua kwenda kwa Kakobe. Kwanza wengi wao wanaamini kuwa sio wagonjwa. Sasa unawategemea watafunga safari hadi Mwenge kutibiwa? Kutibiwa nini wakati wanajua kuwa ni wazima?

Unajua hawa watu wanaojifanya kuponyesha kwa miujiza wananishangaza sana. Mhubiri anatoka Marekani hadi Tanzania kuponyesha wagonjwa. Anakwenda kufanya miujiza hiyo Dasalama. Badala ya kwenda hospitali ya barabara ya baharini (Ocean Road) ambako kuna wenzetu wanaumwa kansa na wanasubiri kuaga dunia. Anakwenda ukumbi wa Diamond Jubilee utafikiri kuna onyesho la Twanga Pepeta.

Badala ya kwenda muhimbili ambako wagonjwa wanateseka bila dawa, anakwenda viwanja vya Jangwani wakati muhimbili ni mwendo wa dakika kumi kwa miguu mwendo wa haraka toka Jangwani. Anatoka nchi ya mbali anaenda kuhubiri kwenye kiwanja ambacho wengi waliokwenda hapo hawahitaji kuponywa magonjwa.

Najua hoja wanayotumia kujibu hili, wanasema kuwa mtu akiwa na imani atakwenda katika eneo kwenye miujiza. Imani inayowapeleka hapo ndio inawaponyesha.

Kuna majibu mawili ya haraka ya hoja hii. Kwanza, kama mtu anaponywa na imani yake hahitaji mtu kutoka Marekani kumponyesha maana dawa ni imani yake mwenyewe na sio ya mtu mwingine. Na imani yake haiko mikononi mwa huyu mhubiri anayejifanya kuponyesha. Imani anayo nafsini mwake. Kwahiyo mponyaji wake hatoki Marekani bali moyoni mwake.

Hoja yangu ya pili ni kuwa kama mtu mwenye imani ndio anaponyeshwa, je kichaa anaweza kuponyeshwa kwa jina la Bwana? Kwani kichaa anaweza kuelewa maana ya kuwa na imani? Anaweza kuelewa maana ya kuombewa? Kwanza kitendo cha kuwa kichaa kinamfanya asijue kuwa anaumwa.

Na watoto je? Watoto wachanga walioko hospitali wanatakiwa kuamka kwenda viwanja vya Jangwani? Au kama wazazi wao hawana imani basi watoto hao wanatakiwa wabaki na magonjwa yao na kuteseka kwa makosa ya wazazi? Lakini Bwana anayeponyesha sio ndio alituambia kuwa kama hatuna imani kama watoto hatutaingia ufalme wake? Si yeye alisema kuwa ufalme wa Bwana ni kwa ajili ya watoto? Sasa mhubiri anapokwenda Tanzania toka nchi ya mbali kama Marekani kisha anaacha kwenda kuponyesha watoto katika wodi za watoto zisizo na dawa za kidunia, tumwelewe vipi? Kwani Jangwani kuna nini? Wagonjwa si wako hospitali? Wameshaomba ruhusu toka serikalini kwenda kuponyesha mahospitalini wakakataliwa? Kwanza wahubiri wanatoa huduma za "kiroho" hospitalini. Kwahiyo haitakuwa mara ya kwanza kwao kwenda kuombea wagonjwa kule waliko.

Tunataka tuamke siku moja tuone kwenye vichwa vya habari vya magazeti:
1. WAGONJWA WODI YA VICHAA WAPONYWA WOTE KWA UWEZO WA MUNGU
2. WODI YA WATOTO YABAKI TUPU: NI BAADA YA MHUBIRI TOKA MAREKANI KUWAOMBEA KWA JINA LA BWANA ALIYE MKUU

Nilikuwa nauliza juu ya atakayetumwa mwaka huu. Nimerukia mambo kibao. Naona nikae chini niandike kabisa makala ndefu juu ya hoja ninazojenga hapa. Au mnaonaje?

TUWARUDISHE WAKOLONI

Jamani,
Mkiniona Bwagamoyo msishangae. Nitakuwa nafuatilia kizizi kwa "Babu." Unajua tena hii ndio ile miezi yenyewe. Toka sasa hadi Oktoba, "Babu" na watu wengine wanaojiita Masharifu watakuwa na kazi nzito sana. Ila "Babu" wa Mlingotini ndio ana kazi kubwa zaidi.

Kutokana na uchaguzi kukaribia, watu wengi wanakwenda kwa "Babu" Mlingotini ili wapate kizizi cha kushinda uchaguzi. Watu kama hawa wanakwenda kwa ajili ya faida zao binafsi. Mimi ninakwenda kwa sababu tofauti. Ninakwenda kwa faida ya umma. Ninakwenda kwa faida yako wewe Mtanzania. Ninakwenda ili kampeni yangu ya kubinafsisha ikulu na kurudisha wakoloni ifanikiwe. Hakuna kitu tunachohitaji Tanzania na Afrika kwa ujumla zaidi ya wazungu wa kututawala.

Tuamue tu kimoja iishe.

Unajua watu wengi hatujui faida za ukoloni. Ukoloni ulitusaidia sana. Uhuru wa nchi za Afrika ulikuwa ni kosa kubwa sana. Ngoja nikutajie faida za ukoloni: bila ukoloni usingekuwa na jina ulilonalo, bila ukoloni usingekuwa na dini uliyonayo, bila ukoloni usingejua kiingereza ambacho unakipenda sana kuliko hata lugha ya watu wako, n.k. Nadhani unaona mwenyewe.

Kama sio ukoloni usingekuwa unamjua mungu wa kweli hata kidogo. Ungekuwa bado unaamini imani za mababu zako ambazo ni za kishenzi. Kama sio za kishenzi lazima ungezifuata, na kama zimefichwa ungezitafuta. Si unaona huzifuati? Jibu sio gumu: imani hizo ndio za kishenzi na wewe hupendi mambo ya kishenzi. Imani za kuabudu mawe uhangaike nazo ya nini?.

Wakoloni lazima tuwashukuru sana. Daima. Bila wao ungekuwa una jina la ovyo kabisa. Jina lako linaloitwa la "kinyumbani" au "utoto" lingekuwa ndio jina lako rasmi. Si unakumbuka ulivyokuwa unalia au kutaka kupigana ukiitwa jina la "kinyumbani" au "utoto"? Bila wakoloni, ukipata mtoto ingekubidi umpe majina ya kishenzi waliokuachia waliokutangulia. Ungewapa heshima kubwa mababu zako kuliko mababu za wengine. Lakini kutokana na wingi wa rehema wa Wamisionari, walitushawishi hadi tukaamua kuenzi mababu zao vizazi hadi vizazi. Majina ya Kiarabu na Kiuropa ni majina ambayo wao wamerithi toka kwa mababu zao. Ila unajua mababu zao walikuwa wastaarabu na mababu zeti walikuwa washenzi sana.

Kwa ufupi, ukoloni unakupa nafasi ya kumpa mwanao jina zuri kabisa la Kiarabu.

Najua walitudanganya wakatuambia kuwa majina hayo ni ya kidini, yaani ya Kiuropa ni ya kikristo ingawa Yesu hakuwahi kuishi Uingereza, Italia, Ujerumani, Ureno, au Ufaransa. Wala hakuwa anaongea lugha ya nchi hizo.


Wakatuambia pia kuwa majina ya Kiarabu ni ya kiislamu wakati ambapo majina hayo yalikuwepo kabla hata Muhammad hajazaliwa. Kwahiyo Waarabu walikuwa na majina hayo hata kabla hawajaanza kuita jina la Allah. Kabla hakujawa na kitu kinaitwa Uislamu, kwa maana ya dini. Kurani ilikuwa "haijashushwa." Hakukuwa na watu ambao waliuita Uislamu tunaoujua leo kama dini yao, lakini walikuwa na majina ambayo leo unayaita ya kiislamu.
Lakini hakuna ubaya kudanganywa kama jambo lenyewe ni zuri. Mimi mtu akinidanganya lakini nikafaidika kwa namna moja au nyingine na uongo huo, sijisikii vibaya. Ndio maana nafurahi sana wakoloni walivyokuwa wanatundanganya kama watoto. Maadamu kulikuwa na faida za kukubali kudanganywa, naona walifanya jambo sahihi. Kwa mfano huu uongo kuhusu majina. Mimi naona majina yao ni mazuri sana. Yanatamkika vizuri, ladha mdomoni, na yana hadhi ya juu. Kwahiyo naona afadhali walitudanganya. Ndio maana ninawaambieni, tuwarudishe. Tena haraka sana. Tunawarudisha polepole mno hivi sasa.

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com