3/22/2005

BARUA YA EDUMEDUS NYONYI KWA PADRI KARUGENDO

Mwanafunzi wa Mlimani, Edumedus Nyonyi kamwandikia Padri Karugendo waraka wenye kichwa hiki: Ujumbe Toka Makaburini. Karugendo kasoma ujumbe huo na kutumia marafiki zake. Nami nimeusoma na kuamua kuuweka ndani ya blogu nanyi muusome.
Mpendwa Padri shikamoo.
Mwezi januari nilibahatika kutembelea eneo la mazimbu Morogoro yalipo makaburi ya wapigania uhuru wa Afrika ya Kusini. Hakika baada ya kutoka huko naona sina raha maishani mwangu. Hata hivyo nimeonelea nikushirikishe sauti hii niliyoisikia hata kama huenda ulishawahi kufika na kushuhudia mwenyewe nakuhakikishia mwangwi wake umebadilika.
Baada ya kufika makaburini ambayo yanatunzwa vema kuliko ya ndugu zetu wanaozikwa Kinondoni au Mburahati, niliona kibao chenye ujumbe ambao umeweka alama katika maisha yangu. Maneno haya yalisomeka hivi"Ours was not for grory nor personal distinction but it was due for the noble cause of our time and the liberation of humanity of the entire community of South Afrika."
Wakati bado nimepigwa ganzi na ujumbe huo huku nisijue la kufanya, wenzangu niliokuwa nao yapata kama ishirini hiv,i wao walikuwa wanashughulika na kupiga picha za ukumbusho. Nilidhani labda mimi ni mjinga kushughulika na kisicho na maana badala ya kuweka kumbukumbu ili nije nikawaonyeshe watu kwamba nani nilishawahi kutembea.
Hata hivyo nilihitimisha kuwa mtu mwenye akili hawezi kushughulika na mambo mengine na kuacha ujumbe wa kutisha, wa kijasiri wa kizalendo, wa kujitoa mhanga kama huo. Basi nilijua ndio elimu yetu ya siku hizi maana imekaa kiutandawazi.
Kumbe vifo vyao havikuwa ili waandikwe kwenye majina ya vitabu vya historia waka kutungwa kwenye nyimbo huku wakisifiwa kila mara! Kumbe kufungwa kwa mandela hakukuwa kukuza jina la ukoo. Bila shaka walijua wazi kuwa wanacho kipigania wanaweza wasikifaidi lakini kwa utu wao na vizazi vijavyo walilala mistuni kama wanyama.
Swali lilinijia kuwa Je ukombozi wa utu wa mwanadamu sasa umekwisha.Uliondoka na kuisha kwa ubaguzi?. La hasha bado tu watumwa wa wageni na hata ndugu zetu. Ndipo nikaenda mbali kuwa watu wanalala darasani ili wapate madgrii wawe maprofesa kwa ajili ya kukomboa wenzao au kukuza jina tu. Na rais na wabunge wanataka nafasi hiyo kama ujumbe wa makaburi ulivyo au ni "for grory and personal distinction".
Niliwahi kukuandikia kuwa nataka kuingia kwenye siasa. Na sababu ni hicho kilio cha makaburi. Nataka nione kama walau elimu yangu naweza kuitumia kuukomboa utu wa mwanadamu tena bila kujulikana kama ikibidi. Nilipanga mwaka huu kugombea udiwani Kanyigo au hata popote ambapo wangelinikaribisha. Niliwaandikia ndugu zangu waanze maandalizi wakadhani nimechanganyikiwa. Hivyo kwa mwaka huu na shughuliza kumalizia masomo naona nitakwama. Wasalaam Nyonyi.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com