3/20/2006

Anuani ya Makazi Mapya

Nyumba mpya ya blogu hii inapatikana kwenye anuani hii: http://jikomboe.com
Au unaweza kubonyeza hapa.
Blogu hii itaendelea kuwepo kama kumbukumbu ya blogu yangu ya kwanza.

2/11/2006

KWAHERINI...

Kwaherini ndugu zanguni.

Kwaheri hii sio ya kuacha kublogu. Sio kama ile ambayo Michuzi aliyotupa hivi majuzi.
Kwaheri hii ni ya kuhama nyumba. Sio kuacha kublogu. Naamini mnafahamu kuwa sitakaa niache kublogu hata kwa mtutu. Nimekuwa siandiki sana na pia hata barua pepe nyingi (za wasomaji na marafiki) sijazijibu. Nilikuwa katika ujenzi wa nyumba mpya. Ujenzi wenyewe bado unaendelea. Unajua ukihamia kwako hata kama madirisha hayana vioo huwa hakuna noma. Hata gunia au bati utaweka maana ni kwako.

Wakati huo huo nimeendelea kuandika ule mwongozo wa wanablogu. Mwongozo huu daima utakuwa unaendelea kuandikwa kutokana na mabadiliko ya haraka ya teknolojia na kutokea kwa mambo mapya. Mwongozo huu umerekebishwa kwani ule wa mwanzo ulikuwa na makosa mengi hasa katika kodi za "HTML." Niliuandika wakati naanza kujihusisha na haya mambo. Baadhi yenu mlinishtua juu ya makosa yaliyokuwepo. Nimesahihisha na kuongeza mambo kadhaa. Kazi yenyewe bado sana. Niliyoandika hivi sasa ni kama asilimia tano.

Ingawa mwongozo huu unalenga hasa wale ambao wana nia ya kuanza kublogu, kuna mambo kadhaa ambayo yanaweza kusaidia hata wale waliobobea. Kama sio mambo yaliyoko hivi sasa basi baadaye kutakuwa na mambo ambayo unaweza kufaidika. Bonyeza hapa usome mwongozo huo.

Haya, sasa nachukua nafasi hii kuwataka mkaribie kwenye makazi yangu mapya kwa chai. Makazi hayo ni.....

Bonyeza hapa uyaone mwenyewe.

2/07/2006

Mchezo wa kuigiza: Watanzania na Utanzania Wetu

Mti Mkubwa (ambaye Michuzi anamuiita Mti Mkubwa Mkavu) ni mwanablogu ingawa sio mwanablogu. Suala la Mti Mkubwa kuwa mwanablogu ingawa sio mwanablogu ni moja ya mifano ambayo mimi huitazama kama ni faida za teknolojia ya blogu. Je ni mara ngapi umeona maoni ya wasomaji kwenye magazeti yamewekwa ukurasa wa mbele? Mti Mkubwa ni msomaji mzuri sana wa blogu na mtoa maoni changamoto. Mara nyingi maoni yake huwa yanakuwa mazito sana kiasi ambacho wanablogu huyaweka ukurasa wa mbele badala ya kuyaacha kwenye kidirisha cha maoni. Hii ni sawa na mhariri wa gazeti kuchukua maoni ya msomaji na kuyaweka kwenye ukurasa wa mbele. Kwahiyo utaona kuwa kutokana na maoni na taarifa mbalimbali anazotoa Mti Mkubwa kuweka ukurasa wa mbele za blogu zetu, unaweza kusema kuwa Mti Mkavu ni mwanablogu (ingawa sio moja kwa moja, kwa maana ya yeye kufungua blogu yake mwenyewe).
Read more »

Michuzi...kisa ni nini hasa?

Matukio mengi yanayotokea duniani hii leo hii. Michuzi anataka kuacha kublogu katika blogu yake tuipendayo ya picha. Nakuomba umsihi abadili uamuzi wake. Ingawa kuamua kublogu au kutoblogu ni uamuzi wa mtu binafsi, unaweza kublogu ikafika wakati ambapo uamuzi wa kuendelea au kuacha unakuwa sio wako binafsi. Hasa inapokuwa ni mtu ambaye blogu yake ni sawa na jumba pepe la makumbusho ya taifa kwa picha. Ina maana kuwa tuna haki na kumhoji atupe sababu za msingi. Sababu aliyotoa kwenye blogu yake haijaniridhisha. Labda atufafanulie zaidi. Bonyeza hapa umsome. Iwapo kuna mtu anamuunga mkono uamuzi wake, mtu huyo ana haki pia ya kutoa maoni yake kwenye kidirisha cha maoni hapo kwenye blogu ya Michuzi. Mimi binafsi simuungi mkono na unaweza kusoma maoni yangu hapo kwenye blogu yake.

2/04/2006

Blogu Hadi Kasulu..

Kama mapinduzi ya uandishi pepe unaona kuwa ni utani, fikiria tena. Kasulu nako kuna blogu. Ndugu yetu Njili Mwakoba amekata shauri. Ameanza kublogu. Mtembelee umkaribishe. Bonyeza hapa.

2/01/2006

Natangaza Kuzaliwa Kwa....

Je una habari za kuzaliwa kwa blogu hizi? Nitaandika machache kutokana na ujio wa wanablogu hawa wapya (ukiacha blogu ya watoto ambao ni ukurasa wa pili wa Da Mija). Watembeeleeni tafadhali na kuwaunga mkono. Kuna ndugu Lubuva, bonyeza hapa. Halafu Kisima cha Weledi, bonyeza hapa. Kutana na Jungu Kuu (lina ukoko au halina?), bonyeza hapa. Na masuala ya watoto kupitia Da Mija, bonyeza hapa.

Kasri halali akitafuta kila mbinu za kuleta wanablogu wapya. Msome mwenyewe kwa kubonyeza hapa kuhusu juhudi zake hizo na matunda yake.

1/29/2006

Blogu Mpya, Nguvu za Teknolojia Mpya, na Kadhalika

Kasri la Mwanazuo katuletea mwanablogu mpya. Juhudi zake nazipongeza. Mwanablogu huyo ni Mustapha ambaye amekuja na Hotspot. Mkaribishe na uwe unamtembelea. Bonyeza hapa uende nyumbani kwake. Kuja kwa Mustapha kumetokea dakika chache kabla sijakaa chini kuandika kifupi juu ya masuala ya teknolojia na vyombo vya habari. Huwa sichoki "kuhubiri" juu ya masuala haya kwani mapinduzi ya teknolojia ya habari, mawasiliano, na maarifa yananikuna sana. Mapinduzi haya faida zake kwa nchi kama zetu unaweza usizione lakini ukiwa unatazama mbali na una uwezo wa kuona "picha kamili" utajua kuwa mapinduzi haya yatabadili mambo katika nchi zetu kwa kiasi kikubwa. Kama sio sasa, ni hapo baadaye kidogo.

Moja ya mambo ambayo yanabadilika kutokana na teknolojia mpya ni mahusiano kati ya magazeti na wasomaji. Mahusiano kati ya wahariri, waandishi, na wasomaji wao. Kwa miaka mingi magazeti yamekuwa ni chombo cha habari cha mstari mmoja ulioonyooka ambapo habari, maarifa, na elimu vinatoka katika vyombo hivyo na kwenda kwa wasomaji. Mahusiano kati ya magazeti na wasomaji ni mahusiano kati ya mtoaji na mpokeaji. Magazeti yanatoa habari na maarifa, sisi wasomaji tunapoke. Wasomaji ni walaji. Barua za wasomaji tunaweza kusema kuwa ndio njia kuu ya kufanya mahusiano kati ya magazeti na wasomaji kuwa ya nipe nikupe. Magazeti yanatuambia jambo nasi tunapata nafasi ya kujibu, kuhoji, kuuliza, kusahihisha, kupongeza, n.k kupitia barua za wasomaji. Pia tunaweza kuandika kukemea jambo au kumtaka kiongozi afanye au aache kufanya jambo fulani. Zaidi ya hapo wasomaji hatuna sauti. Sisi ni magolikipa.

Kama hujawahi kufanya kwenye magazeti hutajua kuwa ni barua chache sana ambazo wasomaji wanaandika zinapata nafasi ya kusomwa na wahariri na kuchapishwa gazetini. Nyingi huishia kapuni. Na wakati mwingine, "barua za wasomaji" huandikwa na waandishi wa habari wenyewe! Kuna mambo ya ajabu sana ndani ya vyombo vya habari (ndio maana wakati mwingine mimi huviita vyombo vya uongo). Unaweza kusoma habari isemayo, "wananchi wengi waliohojiwa na gazeti hili..." ukaamini kabisa kuwa wananchi wengi waliohojiwa kumbe "wananchi" hao wako kichwani mwa mwandishi. Hajaenda kokote, hajahoji mtu yeyote.

Tofauti na magazeti-jadi ambapo msomaji ni msomaji, mtandao wa tarakilishi (Intaneti) umeleta jambo jipya. Mtandao huu, baadhi ya watu wanauita: soma-andika. Mtandao wa tarakilishi umejengwa kwa namna ambayo inaruhusu mtu kusoma na pia kuandika. Kwa mfano, kama umesoma jambo hapa kwenye blogu ukawa hukubaliani nalo au hukuelewa unaweza kuandika kupinga au kutaka ufafanuzi. Walaji na wazalishaji wanakuwa kitu kimoja. Wasomaji wanakuwa waandishi, waandishi wanakuwa wasomaji (wanasoma yaliyoandikwa na wasomaji wao). Mahusiano ya vyombo vya habari mtandaoni na wasomaji yanabadilika na kuwa ya mistari miwili ya nipe nikupe.

Ngoja nikupe mfano mdogo wa jinsi teknolojia inabadili mambo. Nimekuwa nikiandika magazetini rasmi toka mwaka 1992/93. Toka wakati huo hadi majuzi nilikuwa siwezi kujua wasomaji wangu wanawaza nini, ukiachia mbali wale ambao nilikuwa nakutana nao ana kwa ana. Lakini nilipoanza kuweka anuani yangu kwenye makala zangu nikaanza kuwa na mahusiano ya moja kwa moja na wasomaji wangu. Wasomaji wananiuliza maswali kutaka ufafanuzi, wananipa mapendekezo ya makala za kuandika, wananiunga mkono, wananishushua, wananiponda, wananikumbusha ahadi nilizoweka za kuandika kuhusu jambo fulani, n.k. Nimeandika makala nyingi kutokana na mapendekezo ya wasomaji. Hili ni badiliko kubwa sana.

Blogu zinatuwezesha kwa kiasi kikubwa kufanya mambo ambayo yamekuwa hayawezekani katika magazeti-jadi ya kuuzwa mtaani. Huku bloguni tunaandika. Wasomaji wetu nao wanaandika. Mara yanatokea majadiliano. Sio mtu mmoja tu anawaambia wengine ambao wanasoma bila kuwa na uwezo wa kujibu, kuunga mkono, au kuuliza maswali. Hapana. Blogu inawezesha nyanja ya habari kutoka kwenye zama za wasomaji kuwa kama watu wasio na mawazo, habari, au fikra. Watu wanaopaswa kusoma tu, kupokea bila kutoa. Tunatoka kwenye zama hizo na kuingia kwenye zama ambazo nyanja ya habari inakuwa ni aina fulani ya majadiliano. Mazungumzo. Nipe, nikupe. Mzalishaji ni mlaji na mlaji ni mzalishaji. Kila mtu anakuwa mwanahabari. Hili ndio linafanya blogu kupata umaarufu kwa haraka. Siku hizi zinatolewa hadi skolashipu kwa ajili ya kublogu. Sio mchezo. Bonyeza hapa uione (lazima uwe mwanafunzi wa chuo kilichopo Marekani).

Katika kujaribu kubadili mahusiano kati yake na wasomaji, kwa kutumia teknolojia mpya, magazeti kadhaa yanafanya majaribio ya aina mbalimbali. Kwa mfano, gazeti la Wisconsin State Journal linatumia wasomaji wake kuamua habari zipi ziwekwe ukurasa wa mbele. Wasomaji wanapiga kura. Bonyeza hapa usome kuhusu jaribio hili. Mwaka jana gazeti la Seattle Post-Intelligencer lilianzisha jaribio ambalo tahariri inaandikwa na wahariri wa gazeti hilo na wasomaji wake. Kongoli hapa na hapa kwa undani. Kuna gazeti kama News and Record ambalo limeanzisha ukurasa uitwao Town Square katika tovuti yake ambapo wasomaji wanapewa nafasi ya kuandika habari wenyewe. Bofya hapa uwatazame. Magazeti mengi yanachofanya hivi sasa ni kuwa na waandishi wao ambao wanakuwa na blogu. Blogu hizo zinakuwa ni uwanja wa majadiliano kati ya gazeti na wasomaji wake. Ukiachilia mbali maagazeti hayo, teknolojia mpya zimezalisha miradi mipya kabisa kwenye nyanja ya habari. Kwa mfano, kuna Wikinews, mradi ambao habari zinaandikwa na wasomaji. Zinaandikwa na mtu yeyote. Tazama hapa. Halafu kuna jamaa walioanzisha mradi kabambe wa uandishi wa umma huko Korea ya Kusini, Ohmynews. Ohmynews ina habari ambazo zinaandikwa na wananchi. Wasomaji wakisoma habari wakaipenda wanaweza kumlipa aliyeandika habari hiyo. Bonyeza hapa utazama toleo la kiingereza la Ohmynews.

Kwa ufupi, nilikuwa namkaribisha Mustapha , kumpongeza Kasri kwa kutuletea huyu ndugu, na kusema kuwa tunalofanya kupitia katika blogu zetu hizi ni sehemu ya mapinduzi ambayo yanabadili kabisa mahusiano kati ya watoa habari na wapokeaji.

1/28/2006

Zaidi juu ya Creative Commons: kitabu cha bure na zoezi la pekee la kuhariri

Huu ni mmoja wa mifano ya faida za Creative Commons. Majuzi kimetolewa kitabu cha kufundisha watu wa nchi zinazoitwa "zinazoendelea" juu ya ujenzi wa mtandao usiwaya (wireless network kwa kimombo). Kitabu hiki kimetolewa chini ya nembo ya Creative Commons. Kinapatikana bure. Na kuwakuwa kiko chini ya Creative Commons, mtu yeyote yule anaruhusiwa kukitoa kitabu hiki katika lugha yoyote ile (na hata kuongeza mambo ambayo anaona ni muhimu ila hayako katika kitabu mama). Yote hii unaruhusiwa kufanya bila kuomba ruhusa kwa mtu yeyote kwa masharti kuwa kitabu hicho usikitoe kwa minajili ya kibiashara na pia lazima toleo lako liwe chini ya Creative Commons. Kitabu chenyewe ukibonyeza hapa utakipata. Hapa kuna ukurasawa wa "wiki" wa kitabu hicho.

Kuna mfano mwingine wa mabadiliko makubwa yanayojitokeza kutokana na teknolojia mpya na vuguvugu kama la Creative Commons. Mwaka 1999, Larry Lessig, mwanzilishi wa vuguvugu hili, alitoa kitabu kizuri sana kiitwacho Code and Other Laws of Cyberspace. Hili lilikuwa ni toleo la kwanza. Toleo la pili, yaani Code v. 2, ni muendelezo na upanuaji wa hoja na uchambuzi ulioko katika toleo la kwanza. Kwa staili ya ki-Creative Commons, toleo hili la pili badala ya kuandikwa na Larry Lessig peke yake kama ilivyo kawaida katika nyanja ya vitabu, toleo hili linaandikwa/linahaririwa na watu mbalimbali. Ina maana kuwa hata wewe unaweza kushiriki katika kuandika toleo la pili la kitabu hiki. Bonyeza hapa uone zoezi hili la kipekee.

Mawaziri Kuapa kwa Biblia na Kurani: Imani tumezibebabeba tu?

Wiki iliyopita, kwa ajili ya ukurasa wangu katika gazeti la Mwananchi, niliandika makala kuhusu mawaziri wapya kuapa kwa kutumia kitabu "kitukufu" na "kitakatifu" baada ya kuteuliwa. Soma baadhi ya hoja nilizotoa dhidi ya tendo la kuapa:

Baada ya rais mpya kuteua baraza jipya la mawaziri, kilichofuata kilikuwa ni tendo la kula kiapo. Tukio hili limezungumzwa sana mtaani hasa kutokana na kitendo cha Kingunge Ngombale Mwiru (nitampa zawadi ya jina zuri) kuapa kwa kunyoosha mkono bila kushika kitabu "kitukufu" au "kitakatifu" (kurani au biblia) kama wengine walivyofanya.

Wakati ambapo kwa watu wengi kuapa bila kutumia kitabu cha dini ilikuwa ni habari kubwa, kwangu mimi kitendo cha wafuasi wa Isa/Yesu kuapa ndio ilikuwa habari kubwa kabisa. Ni habari ya binadamu kuwa na tabia ya kufanya mambo kutokana na mazoea bila kutafiti kwa kina juu ya usahihi wa jambo lenyewe. Ni tabia inayotokana na utamaduni wa kuiga mifumo ya sheria, utawala, na demokrasia ya nchi nyingine tukidharau uwezo wetu wa kuunda mfumo wetu wenyewe.

Tendo la mawaziri kuapa wakitumia kitabu kitakatifu au kitukufu hatujaanzisha sisi. Utamaduni wa mashahidi kuapa mahakamani kwa kutumia vitabu hivyo hatujauanzisha sisi. Tumeiga toka kwa wengine kama ambavyo tumeiga karibu kila kitu.

Kwanini habari kwangu sio Kingunge kuapa mikono mitupu bali Wakristo na Waislamu kuapa? Jibu la swali hili liko katika kitabu cha Matayo, mlango wa 5, aya ya 33 hadi 37. Katika aya ya 34 Yesu/Isa anakataza wafuasi wake (Waislamu na Wakristo ni wafuasi wake) kuwa wasiape kamwe.

Hivi ndivyo asemavyo toka aya ya 33 hadi ya 37: "Tena mmesikia kuwa watu wa kale waliambiwa: `Usivunje kiapo chako, bali ni lazima utimize kiapo chako kwa Bwana. Lakini mimi nawaambieni, msiape kamwe; wala kwa mbingu, maana ni kiti cha enzi cha Mungu; wala kwa dunia, maana ni kiti chake cha kuwekea miguu; wala kwa Yerusalemu, maana ni mji wa Mfalme mkuu. Wala usiape kwa kichwa chako, maana huwezi kuufanya hata unywele mmoja kuwa mweupe au mweusi. Ukisema, `Ndiyo`, basi iwe `Ndiyo`; ukisema `Siyo`, basi iwe kweli `Siyo`. Chochote kinachozidi hayo hutoka kwa yule Mwovu."

Anasema kuwa ingawa huko nyuma kuna manabii waliwaambia wanadamu kuwa wanaweza kuapa, yeye anabadili na kusema kuwa usiape kamwe. Hii haikuwa kwa mara ya kwanza kwa Yesu/Isa kutengua mafundisho ya zamani. Unakumbuka, ingawa iliandikwa “jino kwa jino, jicho kwa jicho,” yeye alikuja na kusema geuza shavu. Mchukie adui yako akabadili kwa kutuambia kuwa tuwapende na tena tuwaombee. Aligeuza sheria ya kupiga mawe hadi kuwaua wanaokamatwa katika uzinzi. Alibadili sheria kuhusu talaka. Alibadili maana ya kuzini kwa kusema kuwa hata ukitamani umeshazini.

Nimetoa mifano hii kukupa picha kidogo ya baadhi ya mambo aliyobadili likiwemo suala la kiapo. Anatuambia kuwa kipimo cha ukweli wa kauli yetu isiwe ni kiapo. Anasema ukisema “ndiyo” iwe “ndiyo” na ukisema “hapana” iwe “hapana.” Ukisema utatii katiba na kutumikia wananchi, basi tii katiba na kutumikia wananchi. Hakuna la kuongeza wala kupunguza. Sema ukweli na simama kwenye hiyo kweli, usianze kuingiza jina la Mungu ili kutufanya tuone kuwa unayosema ni kweli.

Nimekuwa najiuliza kwanini wafuasi wa Mwalimu huyu wamekuwa hawafuati mafundisho yake? Je inawezekana kuwa ufuasi wao ni wa jina tu na sio imani ya dhati na uelewa wa mafundisho yake? Amesema waziwazi usiape. Wewe unaapa, tena kwa kutumia kitabu chenye maneno yake yanayokukataza. Je hili ni tatizo la kufuata tamaduni za wengine bila kuhoji? Au ni tatizo la kuwa wafuasi wa Isa/Yesu bila kusoma mafundisho yake?

Lakini tukiacha hoja hii ya kuwa Isa/Yesu amekataza wafuasi wake kuapa, kuna hoja nyingine ambayo niliwahi kuitoa huko nyuma. Nitairudia kwa kifupi. Haiwezekani kutumia Kurani au Biblia kuapa kuwa utalinda katiba ya nchi ukitegemea kuwa Mungu atakubariki na kukusaidia ili utimize kiapo hicho. Kwa sentensi chache sana nitakueleza ni kwanini kisha nitakuacha ili iwe tafakari yako siku hii ya mungu jua (ndio maana ya jumapili).

Kurani na Biblia zinasema kuwa Mungu ametoa amri kumi. Amri ya kwanza inasema, “Mimi ni Bwana Mungu wako usiwe na miungu wengine ila mimi.” Hili sio ombi. Inaitwa amri. Anasema wazi kuwa anataka umwamini na kumwabudu yeye tu. Yeye Yehova/Allah. Tuje kwenye katiba yetu: katiba yetu inatoa uhuru wa kuabudu. Ina maana kuwa unaweza kuabudu Mungu mmoja au miungu 10, hutakuwa umevunja sheria ya nchi. Sio hivyo tu, unaweza pia kutokuwa na imani yoyote na usiwe umevunja sheria ya nchi.

Kwa maneno mengine, wakati Yehova/Allah anakwambia, “Niabudu mimi” katiba inasema “Abudu chochote kile.” Je Mungu aliyekupa AMRI ya kumwabudu yeye tu, anaweza kukubariki ili uendeleze katiba inayosema abudu chochote kile? Yaani Mungu atakuwa anakubariki ili uendeleze mwongozo ambao unawapa wanadamu ruhusa ya kuvunja amri yake ya kwanza. Tena amri hii sio ya kumi bali ni ya kwanza. Kama katiba ingesema mwamini mungu mmoja ambaye ni Yehova/Allah, basi nisingeshangaa iwapo waumini wa Kikristo na Kiislamu wangekuwa wanamuomba mungu awasaidie kuilinda hiyo katiba. Lakini katiba haisemi hivyo. Inapingana kabisa na mafundisho ya Allha na Yehova. "Usiwe na miungu mingine ila mimi" sio sawa na kusema kila mtu ana haki na uhuru wa kuamini atakacho.

Kwahiyo kitendo cha kutumia kitabu kinachokutaka uwe na Mungu mmoja kuapa kuwa utalinda katiba inayokuruhusu uwe na mungu yoyote, mmoja au miungu wengi, au hata usiwe na imani kabisa, n.k. kinaonyesha kuwa huenda imani zetu tumezibebabeba tu. Au tumebebeshwa.

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com