1/27/2006

Juu ya Vuguvugu la Creative Commons

Majuzi niliandika kuhusu Tanzania kukubaliwa rasmi kuanzisha tawi la Creative Commons na kuwa Paul Kihwelo, mkuu wa kitivo cha sheria, Chuo Kikuu Huria, ndiye mwongoza mradi upande wa kisheria. Baadaye tunatakiwa kutafuta mwongoza mradi upande wa uhamasishaji. Kama hukusoma niliyoandika siku hiyo, bonyeza hapa. Ukisoma sehemu ya maoni utaona kuwa Mark Msaki ameongelea suala moja ambalo kwa muda mrefu limekuwa lilibishaniwa katika duru za wanazuoni wa masuala ya sheria, sayansi ya jamii, uchumi, na falsafa. Hoja yenyewe ni kuwa sheria ya hatimiliki inachochea ubunifu na ugunduzi. Na kuwa kama kama hakuna faida za kiuchumi/kifedha, watu hawatabuni au kujihusisha na kazi za ugunduzi. Kwahiyo vuguvugu kama la Creative Commons ambalo linachochea watu kuachilia huru kazi zao (iwe ni vitabu, muziki, sinema, n.k.) na kuondoa ukiritimba wa maarifa na elimu, linaweza (vuguvugu hilo) kuondoa msukumo wa kubuni, kutunga, kugundua, n.k.

Hoja hii ina mapengo mengi sana. Mfumo wa hatimiliki una kazi zake. Tunaounga mkono vuguvugu la Creative Commons hatusemi kuwa mfumo wa hatimiliki uondolewe kabisa. Tunasema kuwa mfumo huu unahitaji kufanyiwa mageuzi ili kuendana na upepo wa wakati, teknolojia zilizopo leo hii, na kukidhi matakwa ya umma. Tunachosema ni kuwa tunaweza kutumia itikadi ya ujamaa kwenye kazi ambazo zimekuwa zikifungwa pingu na sheria ya hatimiliki ambayo inakidhi mahitaji ya msukumo wa soko. Msukumo wa soko, kama apendavyo kusema Desmond Tutu, sio mungu. Sio mwanzo na mwisho wa kila kitu.

Zipo faida mbalimbali kwa umma iwapo mfumo wa hatimiliki uliopo (duniani kwa ujumla) utafanyiwa marekebisho. Kwa mfano, tazama suala la dawa za kuongeza maisha ya wenye Ukimwi. Dawa hizi zimegunduliwa (makampuni mengi ya madawa huiba elimu ya jadi ya dawa toka nchi za Kusini) na makampuni ya Magharibi. Dawa zao ni ghali sana kiasi ambacho watu wachache sana wenye ugonjwa huu katika nchi za Kusini wana uwezo wa kuzinunua. Makampuni ya Brazili, India na kwingineko yanatengeneza dawa-chapa kama hizo kwa bei nafuu zaidi. Kutokana na sheria ya hatimikili kitendo cha kampuni hizi kutengeneza dawa hizo bila ruhusa ya makampuni ya Magharibi yaliyozigundua ni kosa. Kitendo cha dawa-chapa hizi kuwa za bei ambayo masikini wengi wanaweza kuimudu kuliko ile ya makampuni ya Kimagharibi hakina nafasi kwenye mjadala. Suala kuu ni hatimiliki na haki ya makampuni haya kufaidi kwanza kwa maiaka kadhaa kabla makampuni mengine hayajaruhusiwa kuzitengeneza. Kwahiyo kumekuwa na kesi mbalimbali ingawa makampuni ya Magharibi yanarudi nyuma kwakuwa yameona kuwa dunia inayaona kama wanyama vile kwa kutaka kuzuia masikini wasio na kipato kupata dawa wanazoweza kununua.

Mfano mzuri wa umuhimu wa vuguvugu la Creative Commons ni huu: Shirika la Habari la BBC linaruhusu Muingereza yoyote kutumia bure chochote BBC walichohifadhi. Kama kuna Muingereza anatengeneza filamu, katika filamu hiyo akawa anahitahi sauti ya simba au tembo au akawa anahitaji video ya mbuga fulani ya wanyama, badala ya kufunga safari kutafuta wanyama hao anaweza kutumia video za BBC. Bure. Kila Muingereza hulipa kodi ya kuendesha BBC. Kwahiyo kila Muingereza ana haki ya kufaidika na kazi za BBC. BBC wakifuata mfumo wa hatimiliki uliopo itabidi wazuie Waingereza ambao ndio hasa wanaoipa uhai BBC kufaidi. Ni sawa na Tanzania. Redio Tanzania inaendeshwa kwa fedha zetu. Je hatimiliki ya kazi zake na rekodi zake zote ni za Watanzania wote? Vuguvugu la Creative Commons linasukuma Redio kama Redio Tanzania kupanua hatimiliki ya kazi zake kuwa ya Watanzania wote ambao kodi yao ndio uhai wa redio hiyo. Bonyeza hapa usome kuhusu BBC kuamua kuweka kazi zao zote chini ya Creative Commons. Unaambiwa kuwa ili umaliza kutazama video walizonazo, unapaswa kutazama video hizo kwa miala 68, usiku na mchana (masaa 24)!

Kuna mtazamo kuwa hatimiliki husaidia sana wagunduzi, watunzi, wanamuziki, n.k. Sio mara zote. Tazama kwenye muziki. Wanamuziki wengi wanapata hela zao sio kwenye kuuza CD bali kwenye maonyesho ya hadharani, matangazo, n.k. Wanaofaidi hasa kazi za wanamuziki ni makampuni ya kurekodi. Utashangaa kuwa makampuni haya ndio huwa yanamikili haki za nyimbo za wanamuziki. Na ndio huchukua sehemu kubwa ya pato linalotokana na kuuza CD. Sasa katika mwelekeo wa ki-Creative Commons, imekuja kampuni inaitwa Magnatune. Kampuni hii inauza CD. Asilimia 50 inakwenda kwa mwanamuziki (hakuna kampuni inayompa mwanamuziki asilimia 50. Hata wanamuziki unaowaona matajiri wanapunjwa wote). Zaidi ya mwanamuziki kupata asilimia 50, mwanamuziki huyo ndiye anayemiliki haki za muziki wake na sio kampuni hiyo. Bonyeza hapa uone kampuni hiyo.

Profesa Kembrew ni mtu wa utani sana. Yeye ni kati ya wanazuoni wanaoandika sana kuhusu mapungufu ya mfumo wa hatimiliki uliopo hivi sasa. Katika kuonyesha mapungufu yake, Profesa Kembrew aliamu kusajili msemo wa kiingereza,"Freedom of Expression." Baada ya kuusajili msemo huu amepewa haki ya kuweka nembo ya "haki zote zimehifadhiwa". Yaani hivi: Freedom of Expression©. Kwahiyo hivi sasa yeye ndiye anayemiliki msemo huo. Bonyeza hapa usome kihoja hicho kwa undani.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com