1/18/2006

Karibu Ibrahim Bwire na Blogu Yako

Ni kweli kuwa bado blogu za Kiswahili ni chache ukilinganisha, kwa mfano, na blogu za Kiingereza za Wakenya. Ni kweli kuwa ni Watanzania wachache hivi sasa wenye uwezo, nafasi, na ujuzi wa kutumia tarakilishi na mtandao wa tarakilishi. Ninafurahi kuwa ukweli huu hauzuii wenye nia ya kublogu kufanya hivyo. Ukitazama historia ya magazeti, kwa mfano, nchini Tanzania utakuta kuwa kuna wakati kulikuwa na gazeti moja. Kuna wakati magazeti yalikuwa machache mno na tena hayakuwa yakisambazwa nchi nzima. Na tena yalikuwa yakisomwa na watu wachache sana. Na tena kulikuwa na watu wengi wasiojua kusoma. Lakini mambo yamekwenda hadi tumefika wakati ambapo huwezi kusoma magazeti yote yanayotolewa kwa siku. Na magazeti hayo yanafikia watu wengi zaidi. Blogu nazo kuna siku tutakaa na kusema, "unakumbuka enzi zile watu walikuwa hawajui blogu ni nini?" Utafika wakati huo. Jitihada zinafanyika. Kwa mfano, blogu zetu siku si nyingi zitaanza kusomwa asubuhi redioni na kwenye luninga kwenye vipindi vile wanavyosoma magazeti ya siku. Yaani kama wanavyosoma magazeti ya siku ndivyo watakuwa wanasoma blogu zetu, jambo ambalo litasaidia tunayoandika kufikia watu wengi zaidi. Tunajua kuwa redio ndio chombo cha habari kinachofikia watu wengi zaidi duniani hivi sasa. Tutaingia kwenye chombo hicho. Kwahiyo upo uwezekano wa kutumia vyombo vya habari vinavyofikia watu wengi kusambaza cheche tunazotoa kwenye blogu zetu.
Tararira yote hiyo nilitaka kumkaribisha mwanablogu mpya, ndugu Bwire (asante sana Kasri la Mwanazuo kwa kutuletea). Bwire anasema kuwa weka kila kitu kando, fikra ndio mambo yote. Bonyeza hapa umtembelee.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com