1/07/2006

Kwanzaa: Meza ya Umoja (na kanga za Mnazi Mmoja!)
















Nadhani baadhi mnafahamu kuwa mimi husherehekea sikukuu ya Kwanzaa. Moja ya mambo yanayofanywa wakati wa kusherehekea sikukuu hii inayoenzi maadili ya Kiafrika ni kuandaa meza ya Kwanzaa inayojumuisha vyakula, mishumaa, kikombe cha umoja, n.k. Unaona mwenye kwenye picha hii. Unaweza kuwa uliwahi kuona kanga hizi zikiuzwa pale Mnazi Mmoja. Meza hii niliandaa kwenye mhadhara ambao nilifundisha watoto weusi juu ya sikukuu hii na umuhimu wake kwao kama watu wenye asili ya Afrika. Baada ya tambiko, mafundisho, na ngoma, tulijumuika katika karamu. Neno karamu (ambalo liko katika wimbo wa Lionel Richie wa All Night Long) ndio hutumika wakati wa sikukuu ya Kwanzaa. Pia wakati wa sikukuu hii wamarekani weusi wanaojali Uafrika wao husalimiana "habari gani." Kutegemea na maadili ya siku hiyo (yako saba) mtu atajibu. Kama ni siku ya ujima, ukimsalimu atajibu, "Ujima."
Bonyeza hapa usome zaidi kuhusu Kwanzaa.
Bonyeza juu ya picha ili uzione vizuri zaidi.

3 Maoni Yako:

At 1/09/2006 04:27:00 PM, Anonymous Anonymous said...

Ebana nimefurahi kuwapa Waafrika wenzetu ufahamu wa Sikukuu ya Kwanzaa maana kwa wengine waliopo kwenye "utumwa wa kiroho" kuanzia wa Kimagharibi na wa Mashariki ya kati hawajawahi kusikia hiki kitu, na dini zao zinatumia silaha mbaya ya lugha ya kukashifu tamaduni zetu Waafrika. Kitu ambacho kinawafanya hawawezi kutoka "utumwani". Nadhani hii ni mbinu tu ya "slave masters" ya kujua wapi pa kuwabana "watumwa" wake wasikimbie kuwa huru kifikra, kitamaduni, kiroho, ... Mapinduzi Daima!

 
At 1/10/2006 04:08:00 AM, Blogger mloyi said...

Hongera kwa kuazimisha kwanzaa, Hii ni sikukuu muhimu kwa waafrika! Ila tunashindwa kushiriki wote, unajua maisha yetu yalivyo magumu!, sijui huwa tunakumbuka vipi siku ya krisimasi na kusahau kuanza kwa kwanzaa?
Ni sikukuu ya waafrika inabidi tulioafrika tuiteke na iwe na nguvu sana huku kwetu kuliko ilivyo huko. Hii itaashiria kuukubali umoja na wenzetu wa huko.
Jikomboe ipo inajitahidi kutukomboa ingawa wengi hatutaki kukombolewa, lakini bado inahitajika kutupa habari motomoto kuhusu kwanzaa, macho na akili yangu iko hapa kujua zaidi kuhusu kwanzaa.

 
At 1/15/2006 08:53:00 AM, Blogger Ndesanjo Macha said...

Asanteni Masawe na Mloyi. Masawe umetumia neno zito sana: utumwa wa kiroho. Mara nyingi huwa nasema utumwa wa kiakili lakini nadhani utumwa tulio nao ni mkubwa zaidi. Umeingia ndani zaidi. Ni wa kiroho. Kama tatizo ni la kiroho, jibu lake si linapaswa kuwa la kiroho?

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com