1/25/2006

Karibu Sana Pambazuka

Baada ya kimya cha muda mrefu ambacho kilinifanya nitake kuunda tume au kutumia makachero wa FBI kumtafuta, mwanablogu Nkya wa Pambazuka amerudi. Tena kwa kishindo na kasi mpya. Sijui hii kasi mpya kaambukizwa na Kikwete na wana mtandao? Ukienda katiba blogu yake utakuta ameandika juu ya madakitari ambao serikali iliwafukuza. Madakitari hawa walikuwa wakidai waongezewe mshahara na serikali ilikuwa ikisema, kama ilivyozoea, kuwa inashughulikia suala hilo. Sijui serikali yetu huwa inatumia miaka mingapi kushughulikia tatizo kama hilo. Toka tupate uhuru, kwa mfano, sirikali imekuwa ikishughulikia tatizo la mshahara usiotosheleza wa walimu. Hadi leo bado inashughulikia. Huenda ndio maana Sumaye alikuwa akituambia kila mara kuwa sirikali yetu hufanya kazi usiku na mchana. Sirikali mpya nayo sijui kama hufanya kazi usiku kucha. Nkya anasema kuwa kitendo cha kufukuza madakitari ni sawa na taifa kupoteza miaka 3,800 ya elimu. Kwa taifa kama Tanzania, kupoteza miaka yote hii sio jambo la mzaha. Bonyeza hapa uone alivyopata miaka hiyo. Nkya anatamani jambo moja: lini kipindupindu kitapiga hodi ikulu? Bonyeza hapa utajua kwanini. Nkya aliwahi kutoa msamiati mmoja. Aliita demokrasia "mkumbokrasia." Mfumo wa siasa na jamii ambapo wananchi wanashiriki kama washabiki. Sasa katika mambo mapya aliyoandika nimekuta ameviita vyama tuviitavyo vya upinzani, "vyama vya ushindani." Nadhani anamaanisha kuwa katika mfumo wa vyama vingi, kazi kubwa ya vyama ni kushindana (zaidi ya kupingana) kuweza kushawishi umma kuwa vina uwezo na mipango bora zaidi ya kuongoza nchi.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com