9/28/2004

WIZARA MPYA KENYA: CHEKA USIOGOPE!

Blogu ya Thinker's imeorodhesha wizara mpya ambazo Mzee Kibaki anazipika. Wizara zenyewe hizi hapa:

Minister of Miscellaneous Projects
Minister of Other Projects
Minister of Stuff
Ministry of Vitus, Details and Ma-somethings
Minister of Livestock (4 or more Legs)
Minister of Livestock (2 - 4 Legs)
Minister of Livestock (Less than two legs, excluding fish)
Ministry of Fish & Animals That Live In Water
Ministry of Ministries
Ministry of Drinking Water
Ministry of Any Other Water (except seas and oceans)
Ministry of Seas, Oceans and other water bodies
Ministry of Catering
Ministry of Highways
Ministry of Roads
Ministry of Lanes
Ministry of Footpaths
Ministry of Language
Meanistry of Hihger Edducation
Ministry of Middle Education
Ministry of Lower Education
Ministry of Committees, Workshops & Conferences
Ministry of Energy (Charcoal & Firewood)
Ministry of Energy (Oil & Petrol)
Ministry of Energy (Gas)
Ministry of Energy (Hot Air)
Ministry of Energy (Biogas)
Ministry of Sports With Balls (Except Pool, snooker, etc)
Ministry of Sports With Balls & Sticks (Pool, snooker, etc)
Ministry of Any Other Sports
Bonus Ministry

DARFUR YA MAREKANI

Wamarekani wanapenda sana kuuliza kwanini Waafrika wanauana katika vita kama vile hawana akili timamu? Wakati ambapo hapa Marekani hakuna mauaji ya halaiki (ya wazi wazi!!!) kama kule Sudan au Rwanda, kuna mauaji baina ya mtu na mtu yanayonifanya nitishike sana ninapoona mtu ananijia akiwa na mkono mfukoni. Bonyeza hapa usome kisa hiki kilichotokea jana huko Detroit. Visa kama hivi vinatokea kila kukicha. Jamaa anaweza kuwa ameudhiwa na mke wake anaamua mguu na njia na bunduki yake kutafuta watu wa kuwamwagia risasi.

IKO SIKU NITARUDI...

Kuna hii blogu inaitwa Aturi. Nimeitembelea muda mfupi uliopita. Jamaa mmoja kasema jambo ambalo limeniacha hoi. Kuna kitu kinaitwa The Myth of Return yaani kila mgeni aliyeko hapa ughaibuni huwa ana ndoto za kurudi makwao siku moja ila hakuna anayerudi! Hii imenikumbusha maneno ya Peter Tosh katika wimbo wake wa Equal Rights anaposema, "Kila mtu anatakwa kwenda mbinguni ila hakuna anayetaka kufa." Onaeli Mandambi (bado una kipindi cha Rege Radio One?). Kwa kumbukumbu ya "experience" za Moshi pale kwa Jere usiku tukimsikiliza Tosh akililia haki na Gregory Isaacs akilalama kwa tungo za mapenzi kama Night Nurse huku mchicha wa ugali ukichambuliwa. Kuna raha wakati mwingine kuogelea katika kumbukumbu za miaka ya nyuma.

Kuna bwana mmoja pale Moshi, sijui yuko wapi siku hizi, alikuwa akinikumbusha sana Peter Tosh. Nilikuwa nakutana naye kila jioni pale YMCA. Mrefu, mwembamba, mweusi, na ana sura ya ukaidi kama alivyokuwa Daktari Mitishamba (Bush Doctor) mzee wa "Ihalalishe" (Legalize It) Peter Tosh. Huyu bwana, jina nimemsahau, siku moja tumekaa pembeni ya bwawa la kuogelea la YMCA (Davis Mosha unakumbuka enzi zako na Nick Malisa pale bwawani? Mmoja wenu karibu azame. Hivi alikuwa ni nani vile??) basi huyu jamaa, ambaye ni rasta, alikuwa anasikiliza mhubiri aliyekuwa akiendesha ibada ukumbini. Rasta akamsikiliza wee....kisha akanitazama na kusema kwa kiingereza, "Church is big business." Akanyanyuka na kuondoka. Nilikuwa bwana mdogo wakati huo. "Kanisa ni dili?" Maneno haya niliyafikiria kwa miaka mingi iliyofuata kabla ya kuelewa kwa undani alichokuwa akisema.

Hivi nilikuwa nasema nini tena? Naona nimerukia mambo kibao hadi nimesahau nilichokuwa hasa nataka kusema. Hakuna ubaya. Haya, salimia nyumbani.

9/26/2004

NYUMBA ILIYOJENGWA KWA MATAIRI TANZANIA

Wakati wamasai wanatumia matairi kutengeneza malapa, bwana Charles Lugenga wa DSM amejenga nyumba ya aina yake. Nyumba hii kila kitu pamoja na zulia la ndani, viti, na meza vimetengenezwa kutoka kwenye matairi yaliyotumika! Lugenga anasema kuwa ujenzi wa kutumia matairi yaliyotupwa utasaidia katika kusafisha mazingira. Habari zaidi pamoja na picha za nyumba yenyewe kongoli (bonyeza) hapa.

9/23/2004

Soma Makala za Padri Karugendo

Nimemaliza kusoma makala za Padri Privatus Karegendo zinazotolewa katika gazeti la Rai nchini Tanzania. Kwa walioko nje ya Tanzania ambao hawapati makala zake, unaweza kusoma makala zake hizi tatu kwa kwenda hapa: http://kumekucha.com/Makala.php

9/21/2004

Ukiwa na Njaa Mtafuite Erick

Nimemtaja Erick kwenye makala yangu ya wiki iliyopita katika gazeti la Mwananchi. NIlikuwa nazungumzia suala la kujitolea kusaidia jamii na wanajamii. Erick hujitolea kushughulikia suala la maakuli. Ukienda kwenye tukio lolote lile la hadharani, iwe ni sinema, muziki, hotuba, maonyesho, n.k. ukakutana na Erick basi ujue kuna chakula cha bure. Kila ninapomwona lazima nicheke. Erick yeye ni mfuasi wa siasa za "kijani." Ni mtetezi wa mazingira. Anapenda sana kujitolea kusaidia. Kwa mfano, kila ijumaa lazima apike chakula kisha aende kituo kikuu cha mabasi hapa Toledo kugawa chakula hicho bure. Mpango huu wa kugawa chakula bure kituo cha basi unaitwa "Chakula, sio Mabomu" (kwa tafsiri ya kiswahili). Kawaida huwa anakwenda kwenye maduka ya vyakula vya asili (yaani visivyo na kemikali za sumu) ambako huwa anapewa chakula bure. Ikifika ijumaa anapika kisha huyoooo...kituo kikuu cha cha mabasi.

Ikitokea ukamuona Erick ukiwa na njaa, tuliza akili maana muda si mrefu utakula. Leo nilikwenda kutazama sinema ya bure iitwayo The Carlyle Connection kwenye kanisa la Central United Methodist mtaa wa Central. Sinema hii inaonyesha jinsi ambavyo familia ya Bush imekuwa na uhusiano wa muda mrefu wa kibiashara na kirafiki na familia ya Usama Bin Laden. NIlikuwa nimechelewa kidogo kwenye hiyo sinema. Nilipoingia tu nikamuona Erick ameketi. Njaa ilikuwa imenikamata kweli, lakini nilipomuona ilikuwa kama nimeshashiba. Baada ya kuketi dakika tano hivi nilinyanyuka kuelekea upande alioko Erick. Kawaida huketi au kusimama pembeni ya chakula chake. Kila anayeenda kuchukua chakula anapewa somo fupi kuhusu chakula chenyewe. "Leo hii asithubutu kuja kunipa hutba." Nilijisemea wakati nikielekea kwenye meza iliyoshehena vyakula vya nguvu.

Baada ya kula na kushiba vilivyo, Erick alinijia, "Ukitaka chakula zaidi unaweza kuchukua upeleke nyumbani." Huyu ndio Erick mwenyewe. Lazima ukishakula akushawishi uchukue chakula nyumbani.

Huyo ni Erick. Nikimtazama simmalizi. Sijui muda wa kupika vyakula vyote hivi kila kukiwa na tukio anapata wapi. Pamoja na kuwa ni mwanafunzi, Erick akizuka kwenye tukio lolote lazima awe na mikoba ya chakula. Imefika wakati ukiongea naye unaona kama vile unaongea na hoteli.

Erick na chakula chake. Kuna wakati nikimwaza nikiwa peke yangu ninabaki kucheka. Sio muongeaji sana. Anapenda kutazama huku akitabasamu. Akiongea itakuwa kuhusu chakula!
Jambo la ajabu ni kuwa sijawahi kumuona Erick akila!!

9/19/2004

MDUARA WA NGOMA

Mwendo wa kama dakika tano kwa miguu toka nilipohamia hivi karibuni, Old West End, kuna kituo cha sanaa, Collingwood Art Center. Kundi la ngoma za Kiafrika na Karibiani la Alma Dance Experience limetoa ukumbi wake wa mazoezi kwa ajili ya watu wanaopenda kupiga ngoma. Kwahiyo kila jumapili kuanzia saa saba na nusu watu wanajimwaga hapo na ngoma zao.

Kinachofanyika hapo kiingereza kinaitwa Drum Circle. Watu hutengeneza mduara kisha wanaanza kupiga ngoma. Hakuna anayeongoza. Hakuna kuongozwa. Upigaji unatokana na hisia ya mtu. Kila mtu anapiga ngoma, awe anajua au hajui. Ngoma zinapigwa wee hadi watu wanasuuzika roho zao.

Nilikwenda kwenye mduara wa ngoma kwenye kituo hiki kwa mara ya kwanza. Kulikuwa na watoto, familia, vijana, watu wa makamo, n.k. Watu wengi wanaohudhuria mduara wa ngoma huamini kuwa ngoma/muziki ni aina ya dawa. Ni dawa nzuri sana hasa kwa watu wanaoishi kwenye mfumo wa maisha ambao watu wanafanyishwa kazi kama punda ili kujenga ubepari. Bwana mmoja, kwa mfano, amesafiri umbali saa moja ili kuja kupiga ngoma.

Niliulizwa kama Afrika kila mtu anajua kupiga ngoma au kama Tanzania watu wanapenda kukaa pamoja na kupiga ngoma. Jibu nililowapa liliwashangaza sana. Ngoma tulizokuwa tukitumia zimetoka Afrika. Ngoma yangu kwa mfano imetoka Senegal. Wengi walikuwa na ngoma iitwayo Djembe ambayo ni maarufu sana. Ngoma aina ya Djembe haihitaji kuchomwa moto kama ngoma nyingine ili itoe mlio mzuri. Ngoma hii ina kamba ambazo unazikaza kwahiyo hakuna haja ya kutafuta kuni na kiberiti kila mnapotaka kupata magoma kitakita.

Ni kitu gani kinafanya wenzetu kupenda sana utamaduni wetu wa asili wakati sisi tunauponda? Kundi la Alma Dance Experience kwa mfano linajulikana hapa Toledo kwa ngoma za asili toka Afrika. Kundi hili limeundwa na watu weupe.

Nakumbuka nilipokuwa jimbo la Washington nilikwenda kanisa la Universal Church kwenye sherehe moja. Utashangaa kuwa makanisa ambayo waumini wake wengi ni weupe kama hili la Universal Church upigaji wa ngoma za asili za Kiafrika ni sehemu ya ibada. Ukienda makanisa ya watu weusi wa hapa Marekani au hata yale ya weusi waliohamia toka Afrika huwezi kukuta hata siku moja wakipiga ngoma.

Ukienda kwenye "mduara wa ngoma" popote pale utakutana na watu weupe na weusi wachache sana. Waotunza na kutukuza utamaduni wetu ni kizazi cha wale waliochangia katika kuuharibu. Lakini sisi kwanini hatuoni uzuri wa tulichonacho?

Ninasikia njaa. Ngoja nikatie ndani. Jana jamani nilishiba kama sijui nini. Nilikwenda kwa rafiki yangu toka Sierra Leone, Amira Alghali, ambaye alikuwa amepika ubwabwa wa kisamvu cha mawese. We! Nashangaa sikujing'ata ulimi. Haya ngoja nikale.

Kabla sijasahau. Yule jirani yangu anayefuatilia vifo na majeruhi huko Iraki anaendelea na kazi yake. Namba zilizoko kwenye mabango matatu mbele ya nyumba yake zimebadilika. Leo yapata mwendo wa saa kumi takwimu zilikuwa hivi:
WAIRAKI WALIOKUFA = 12,778
WAMAREKANI WALIOJERUHIWA = 7,230
WAMAREKANI WALIOKUFA = 1,032

Hiyo demokrasia ambayo rais mwizi wa kura Joji Kichaka (george bush) anadai kuwa inajengwa nchini Iraki iko wapi? Si tuliambiwa kuwa Wairaki wanamchukia sana Saddam kiasi ambacho askari wa Marekani watapokelewa kwa shangwe, vifijo, nderemo, na maua? Maua na nderemo vinaweza kusababisha vifo vya askari 1,032 na kujeruhi 7,230? Ngoja nikale.

9/18/2004

NIJIITE X???

Ninaanza kuchoka kumfunza kila ninayekutana naye jinsi ya kutamka jina langu: ndesanjo. Wengine wanasema, "Basi nitakuita Macha." Lakini nawaambia kuwa Macha ni jina la familia/ukoo. Macha sio jina langu. Mimi ni Ndesanjo! N'takuzaba kibao mimi...

Wengine wanapata tabu kulitamka kiasi ambacho utadhani kuwa wanaweza kuvunja jino! Tuache utani, ninaanza kukerwa. Sina muda wa kufundisha kila ninayekutana naye. Ninakutana na watu kibao kila siku. Kuna mambo mawili naweza kufanya: nianze kutoza kodi (si ndio ubepari wenyewe huu?) kila ninapofundisha mtu au nikate mzizi wa fitina na kufuata nyayo za Malcolm X kwa kujiita X!

MALCOLM X

Wale wanaofuatilia kwa karibu mambo yanayomhusu Malcolm X (El Haj Malik El Shabaz) unaweza kwenda kwenye webu hii inayoendeshwa na Dr. Abdul AlKalimat wa chuo Kikuu cha Toledo. Hapa utakuta hotuba zake. Unaweza kuzirekodi kwenye CD. Bonyeza hapa.

SARAH SHADRACK

Tafadhali Sarah Shadrack nipe anuani yako. Umeaniachia ujumbe bila anuani. Asante.

9/15/2004

KWA TAARIFA YAKO...

Kwa taarifa yako...
Hakuna kitabu chochote katika Biblia ambacho kimeandikwa na nabii Musa. Kanisa lilinidanganya kwa miaka mingi sana nikadhani kuwa ni kweli vitabu hivi viliandikwa na Musa. Musa hakuandika kitabu hata kimoja.

Kama vitabu vitano vya mwanzo vya Biblia vimeandikwa na Musa kwanini aandike, "...Mungu akamwambia Musa..." badala ya kuandika "Mungu akaniambia..." Mtu akikwambia jambo huwa hatusemi, "Fulani akamwambia..." bali tunasema, "Fulani aliniambia..."

Na iweje Musa aandike hadi kifo chake mwenyewe? Kitabu cha Kumbukumbu la Torati: 34:7 kinasema: Musa alikufa akiwa na miaka 120...
Inawezekana mstari huu Musa aliuandika kabala hajafa! Au aliuandika kimiujiza baada ya kufa?

Uongo mwingine ni kuwa vitabu vya Injili ya Matayo, Marko, na Luka vimeandikwa na wanafunzi wa Yesu. Hawa mabwana hawakuwa wanafunzi wa Yesu. Yote waliyoandika waliandika kutokana na mambo waliyoyasikia toka kwa wale waliomuona Yesu! Tatizo ni kuwa hata mahakamani ushahidi wa mambo uliyosikia (hearsay) hauna nguvu!

MAARIFA NA VITA

Leo asubuhi nilikuwa katikati ya jiji. Ujumbe ulioandikwa katika ukuta wa maktaba kuu ya jiji la Toledo iliyopoa katika makutano ya barabara ya Adams na North Michigan nimeupenda: MAARIFA YAMEKOMBOA WATU WENGI DUNIANI KULIKO VITA VYOTE VILIVYOWAHI KUPIGANIWA KATIKA HISTORIA.

MABANGO YA KISIASA NJE YA NYUMBA

Jumba la nne mtaa wa Robinwood, karibu na makutano ya Robinwood na Bancroft ni uwanja wa siasa. Nje ya jumba hilo kuna bendera ya Marekani na ya Umoja wa Mataifa zinapepea. Kitendo cha kuweka bendera ya Umoja wa Mataifa kinanifanya nitambue kuwa mwenye jumba hili lilojengwa miaka mingi iliyopita ni mtu wa siasa za mrengo wa kushoto. Watu wenye siasa za mrengo wa kulia wanauponda sana Umoja wa Mataifa. Hawaoni sababu ya maana ya MArekani kuwa mwanachama wa Umoja huu. Wananchi wa siasa za kushoto kama huyu bwana wanaona kuwa umoja huu pamoja na matatizo yake mengu bado una manufaa kwa taifa na dunia kwa ujumla.

Jana jioni nikiwa narudi toka mizungukoni na rafiki yangu Malaika jamaa alikuwa nje ya nyumba yake akiwa amemaliza kuweka mabango matatu meupe yaliyoandikwa kwa rangi nyekundu. Yameandikwa hivi kwa herufi kubwa:
WAIRAKI WALIOKUFA: 12, 721
WAMAREKANI WALIOKUFA: 1, 014
WAMAREKANI WALIOJERUHIWA: 7, 032

Hizi ni takwimu zinazotokana na uvamizi wa kigaidi wa Marekani dhidi ya Iraki. Kila siku atakuwa anabadili takwimu hizi kuendana na yanayotokea huko Iraki.

Hii tabia ya watu wa mtaa huu wa Old West End kuweka mabango ya kisiasa nje ya nyumba zao unanifurahisha sana. Nitapiga picha baadhi ya mabango haya na kuweka ndani ya blogu hii.

9/12/2004

Pilikapilika

Niko katika pilikapilika za kuhama. Ninahama toka mtaa wa Leitchworth kuelekea mtaa wa Old West End hapa hapa Toledo, Ohio. Old West End ni mtaa wenye nyumba za kizamani zilizojengwa kwa mtindo uitwao Victorian. Majirani naona wameanza kunitazama kiajabuajabu. Mimi mweusi na mtaa umejaa ngozi nyeupe. Wengine wameanza kuniuliza, "Unafanya kazi gani?" Wanataka kujua kama wamepata jirani asiye na mbele wala nyuma atakayehatarisha usalama wao. Huu ni mtaa wa watu wanaokaa barazani jioni wakinywa mvinyo na kusoma magazeti kama Mother Jones, The Nation, na Village Voice . Wengi wameweka "sticker" za kumponda Bush kwenye magari yao au nje ya nyumba zao wameweka mabango yanayosema, "Rudisha majeshi nyumbani" wakionyesha kutokuunga mkono uvamizi wa kigaidi na kidhalimu uliofanywa na Rais Joji Kichaka dhidhi ya Iraki.


"Jina lako gumu kweli kutamka. Itanichukua muda. Umesema unafanya kazi gani?"
"Nafundisha." Nawajibu.
"Umetoka wapi?" Wananiuliza kutokana na lafudhi yangu.

Asubuhi, mchana, jioni: Jina lako gumu kutamka. Unafanya kazi gani? Umetoka wapi?

Kuna kitu kinaitwa white flight: watu weupe wana tabia ya kuhama mtaa kama ukianza kujazana watu weusi. Najua hii haitatokea maana nikishawaambia ninapofundisha na kuwa nimetoka Tanzania najua hujisemea moyoni, "Huyu ni tofauti." Hii tabia ya kusema kuwa watu weusi tuliotoka nje ya Marekani ni "tofauti" wakimaanisha kuwa sisi ni bora zaidi ya weusi waliozaliwa hapa inaniudhi kishenzi.

Ukitaka kuona baadhi ya nyumba za Old West End kongoli hapa.

9/10/2004

KENYA: KOZI YA UANDISHI WA MTANDAO WA TARAKILISHI (kompyuta)

Kozi ya uandishi wa mtandaoni (online journalism) imeanza kutolewa nchini Kenya. Kozi hiyo inatolewa na United States International University jijini Nairobi. Kwa habari zaidi kongoli hapa.

JABALI AFRIKA (Sisi Tambala wa Kenya)

Kila ninapowasikiliza hawa jamaa wa Kenya wanaojiita Jabali Afrika ninakumbuka sana kundi la Sisi Tambala (bado wanafanya mazoezi pale nyumba ya sanaa?). Jabali Afrika wanaimba kiafrika na kupiga ngoma. Niliwasikia mara ya kwanza mwaka 2001 niliponunua kanda yao pale Nairoberry (Nairobi) nikitokea Kisumu. Ilikuwa ni kanda ya CD yao iitwayo Journey. CD yao ya mwisho kutoa, Rootsganza sijaipenda sana. Naona wameingiza vyombo kadhaa ambavyo vimeharibu kabisa ule utamu wa sauti zao na midundo ambayo inanikumbusha sana afrika. Ila Maumau Chant katika CD hiyo ni kiboko. Hatari tupu. Mshairi Cosmas Sindani (ninatafuta habri zake zaidi) ndio hasa amenikuna. Huku ngoma zikirindima kwa mtindo wa Nyanbinghi, Sindani anaghani kwa sauti iliyojaa hisia, "Mzungu arudi Ulaya, Mwafrika apate Tawala." Ninapanga kwenda Cleveland mwezi huu kwenye shoo yao. Tazama picha zao kwa kubonyeza hapa.

Baba Moi na Mzee Ruksa

Ni kitu gani kinafanya watawala wanapoachia madaraka wana wa nchi wanaanza kuwapenda hata kama hawakuwa viongozi wazuri? Ali Hassa Mwinyi, maarufu kwa jina la Mzee Ruksa, wakati akiwa madarakani nchini Tanzania aliandamwa sana kutokana na utumbo uliokuwa umetawala serikali. Hivi sasa hakuna kiongozi anayeshangiliwa kwenye dhifa za kitaifa kama yeye. Kenya nako, Baba Moi ambaye alikuwa madarakani toka mwaka 1978 hadi aliposhindwa mwaka jana, alikuwa akiandamwa kutokana na rushwa na uchafu mwingine mwingi. Hivi sasa kuna watu wanamuota.

KAMUSI PROJECT

Unaweza kushiriki katika mradi wa chuo kikuu cha Yale uitwao Kamusi Project ambapo mtu yeyote, toka popote, anaweza kuchangia katika kuandika kamusi ya Kiswahili. Bonyeza hapa.

9/09/2004

TUMA KWA YEYOTE

Kila ninapoandika lolote, mwishoni utaona kuna picha ya bahasha. Ukinbonyeza juu ya bahasha utaweza kumtumia yeyote jambo unalosoma. Kwahiyo ukisoma jambo lolote ukataka kuwashirikisha wengine, bonyeza juu ya bahasha ndogo mwishoni upande wa kulia, mtumie unayetaka.

9/06/2004

METHALI NA TOVUTI YA WIKI

METHALI: Konzo ya maji haifumbatiki.

Kiswahili hicho. Umejua maana yake?

Hii ni webu/tovuti yetu ya wiki: www.chezasalama.com

HipHop: Tazama Video

Kuna video hapa ya tamasha la hip hop kwa ajili ya Ukimwi lililofanyika Uholanzi mwaka 2002. Kati ya walioshiriki ni X Plastaz wa Tanzania na Baby Fatim wa Senegal. Tazama video zao hapa: http://www.baobabconnections.org/artikel.php?id=444

MAJALIWA YA WAKIMBIZI

Kuna sinema inayoonyesha majaliwa ya wakimbizi walioko ughaibuni. Filamu hii unaweza kuitazama kwa kwenda hapa: http://www.baobabconnections.org/artikel.php?id=198 .

WATAZAME NA KUWASIKILIZA X PLASTAZ

Unaweza kuitazama video na kusikiliza nyimbo za kundi la X Plastaz kwa kwenda hapa: www.xplastaz.com. Ukifika hapo bonyeza palipoandikwa: LISTEN/WATCH. Pale kuna video kama Bamiza, Ushanta, Aha!, n.k. na nyimbo toka albamu ya MasaiHiphop - 2004.
Haya furahia wasanii wanaoteleza kwa mashairi na mdundo mzito.

9/04/2004

MSIKILIZE SUGU (MR II)

Kwa wale wanaopenda mashairi ya MR II nenda hapa unaweza kusikiliza baadhi ya nyimbo zilizomo katika albamu yake mpya iitwayo SUGU. Bonyeza hapa. Pia fuatilia tovuti/webu yake hii: www.sugumusic.com. Tovuti hii bado iko kwenye ujenzi.

HATIMAYE NURU AFUNGULIWA MINYORORO

Yule binti, Nuru, aliyekuwa amefungwa minyororo kama mnyama na mama yake kwa miaka miwili sasa ameshafunguliwa. Binti huyu alikuwa akiishi kama nusu binadamu. Alikuwa akila kinyesi chake! Kwanini walimfunga Nuru minyororo badala ya mbwa? Soma habari hiyo kwa kubonyeza hapa.

MSOME FREDDY MACHA

Tayari nimeweka baadhi ya makala na hadithi za Freddy Macha katika blogu hii. Nenda mkono wa kuume baada ya makala zangu zinafuata makala na hadithi za Freddy. Kongoli juu ya makala au hadithi yoyote usome. Kwa mengi zaidi juu ya Freddy Macha unaweza kumtembelea hapa: www.freddymacha.com. Leo nimeweka hadithi moja: Mbwana na Mariamu. Hii hadithi iko kwenye mkusanyiko utakaochapwa karibuni katika kitabu kitakachoitwa MPE MANENO YAKE. Nyingine zote ni makala ambazo zimetoka katika magazeti ya Mwananchi na The Guardian nchini Tanzania.

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com