9/28/2005

Wikipedia Ya Kiswahili

Ile kamusi elezo ya Kiswahili (Kiswahili wikipedia) ambayo inaandikwa na kuhaririwa na mtu yeyote anayezungumza Kiswahili inahitaji msaada wako wewe mpenda lugha yetu tamu...kumbuka Shaban Robert na "titi la mama litamu ingawa la mbwa..." Kamusi hii ukilinganisha na kamusi elezo za lugha nyingine kama vile wikipedia ya kiingereza , kifaransa au Kidachi iko nyuma kidogo. Yeyote yule ambaye ana muda anaweza kushirika kuipanua kwa kufanya mambo kadhaa: kuandika makala mpya, kuhariri zilizopo, kuitangaza (hawa wanablogu wana nafasi ya kuitangaza), n.k. Ukienda hapa utapata taarifa zaidi juu ya mambo ya kufanya ili kuiboresha. Ukurasa mkuu wa wikipedia yetu huu hapa.

9/27/2005

Gumzo Kuhusu Kiongozi cha Wanablogu na Wanaharakati Mtandaoni

Lile gumzo na mkurugenzi wa masuala ya intaneti wa Wanahabari Wasio na Mipaka kuhusu kitabu kipya kiitwacho Handbook for Bloggers and Cyber-Dissidents limemalizika. Unaweza kusoma yote yaliyozungumzwa katika gumzo hilo lililotumia teknolojia ya Internet Relay Chat. Nenda hapa.

Muhtasari wa Mkutano wa Utandawazi na Demokrasia Helsinki

Niliandika muhtasari huu hivi majuzi kwa ajili ya blogu ya Sauti za Dunia (Global Voices) kuhusu mkutano niliohudhuria majuzi kule Helsinki, Ufini. Usome kwa kubonyeza hapa.

JALO KARIBU SANA...

Jalo karibu sana. Ni masika nyingi zimepita...karibu sana sana. Hapa ni sebuleni kwangu.
Zimepita siku nyingi. Miaka mingi. Toka pale namba saba (nadhani ilikuwa namba sana), kule darinini...
Hongera sana.
**Ujumbe huu ni wa mafumbo. Ni mtu mmoja tu atakayelewa na ndiye anayepaswa kuelewa.

Nitakwenda Mkutano wa ConvergeSouth na Pop!Tech

Nitakapomaliza mkutano wa We Media: Behold the Power of Us kule New York tarehe 5 mwezi ujao, nitaondoka nikikimbia nikikatiza "shotikati" moja ya kupitia kwenye mashamba ya mahindi kuelekea North Carolina kwa ajili ya mkutano mwingine mkubwa kuhusu zana mpya za mawasiliano (masuala ya blogu yakiwa yamepewa kipaumbele) utakaofanyika tarehe 7 na 8 mwezi ujao katika chuo kikuu cha A and T, North Carolina. Mkutano huu utakaomshirikisha mwanablogu anayesukuma vuguvugu la kidemokrasia nchini Irani kwa kutumia blogu, Hoder, unaitwa ConvergeSouth. Kisha tarehe 19-22 mwezi Oktoba nitakuwa katika mji wa kizamani wa Camden katika jimbo la Maine kuhudhuria mkutano wa kila mwaka unaokutanisha watu toka sekta mbalimbali kujadili na kubadilishana mawazo juu ya teknolojia na mabadiliko ya jamii. Mkutano huu unaitwa Pop!Tech 2005.


Mikutano! Mikutano! Mikutano!

Nadhani hadi "mwokozi" akija mara ya pili atatukuta wanadamu tuko kwenye mikutano. Wanadamu tunapenda sasa kukutana...na kuongea na kupanga mikakati. Bila kusahau kula na kunywa mvinyo.

Haya hekaheka za mikutano hazijaniisha. Tarehe tano mwezi ujao nitakuwa New York kwa mkutano wa siku moja ulioandaliwa na Kituo cha Habari cha Taasisi ya Habari ya Marekani (API) uitwao We Media: Behold the Power of Us.


Ninahudhuria mkutano huu wa siku moja kupitia udhamini wa Kituo cha Habari kwa watu 15. Orodha ya waliopata udhamini huo hii hapa:

* Nathalie Applewhite, Candidate, Master of International AffairsSchool of International and Public Affairs, Columbia University
* Anjali Arora, Freelance Consultant in Information Architecture /User Experience Design
* Dr. Ralph Braseth, Director of Student Media & Assistant Professorof Journalism, The University of Mississippi
* Kent Bye, Director, The Echo Chamber Project
* Andy Carvin, Director, Digital Divide Network, EDC Center for Media& Community
* John Mwendwa Gitari, Fanning Fellow, Kettering Foundation
* Timothy Karr, Campaign Director, Free Press
* Kathryn Kross, Deputy Director, Center for Public Integrity
* Katie Lips, Creative Technologist and Co-Founder, Kisky Netmedia
* Ndesanjo Macha, Blogger, Jikomboe and Digital Africa
* Ron Mwangaguhunga, Editor, The Corsair
* Steven C. Podd, Principal, Nesaquake Middle School
* John Schott, Chairman, Cinema & Media Studies, Carleton College
* Elina Shcop, Founder, Kaleidoscope of Living (KOL)
* Nichelle Stephens, Blogger, nichellenewsletter

Usikose Mahojiano Kuhusu Kiongozi cha Wanablogu Leo

Mambo mengi yametokea na yanaendelea kutokea toka niandike mara ya mwisho. Yapo ambayo nisingependa yakupite. Kwanza kabisa leo hii kutakuwa mahojiano kati ya mkurugenzi wa masuala ya mtandao wa Wanahabari Wasio na Mipaka, Julien Pain, kuhusu kitabu kizuri sana walichokitoa kuhusu uanaharakati wa mtandaoni. Kitabu hiki ambacho ni kiongozi cha wanablogu na wanaharakati wa mtandaoni kinapatikana bure hapa. Mtu yeyote anaweza kushiriki kwenye mahojiano hayo ambayo yatafanyika kwa kutumia teknolojia ya Internet Relay Chat (IRC). Taarifa kamili kuhusu saa na jinsi ya kuingia kwenye mtandao huo wa IRC nenda hapa.

Rebecca MacKinnon amechambua kwa ufupi yaliyomo katika kiongozi hiki. Msome hapa.

Huenda Niko Karibu Nawe

Baada ya kuondoka kwenye ule mkutano wa kuuziana maneno kama ilivyo mikutano mingi niliingia mitini kimya kimya. Nilikwenda mahala kwa mapumziko kisha nikaenda kwa Kichaka. Kisha nikaondoka tena, kimya kimya. Sasa niko mahala fulani ambapo sipendi kusema ni wapi! Lakini utashangaa...huenda niko jirani nawe. Huenda niko mtaa wa pili na hapo ulipo. Kwahiyo tukikutana barabarani, kijiweni, au mgahawani usije sema sikukwambia. Huenda niko Aruba. Au labda visiwa vya mtakatifu Helena. Au pengine niko pembeni ya kwa msikiti wa Kwa Mtoro jijini Dasalama. Au labda pembeni ya soko la Kiboriloni mjini Moshi. Au ufukweni mwa bahari Mambasa (yaani Mombasa). Au kwa Bibi Lizabeti. Au Trenchtown kwa Bob Malya, nchini Jamaika. Utajaza mwenyewe.
Nilipo ninavaa miwani nyeusi kila siku. Na kichwani kofia kubwa. Unaweza usinitambue. Jaribu kutafuta mtu mwenye miwani nyeusi ya ki-KGB na kofia kubwa ambaye anatembea na kompyuta ndogo ya mapajani akitafuta mawimbi ya mtandao usiwaya (wi-fi). Ni mimi.
Nina picha tulizopiga pale klabu ya Chelsea, jijini Helsinki. Hapa ndio wanapokutana Watanzania wanaoishi Helsinki. Basi wageni na wenyeji tulikutana hapo na kupiga picha. Kabla sijazitundika nitawauliza kwanza walioko kwenye picha kama ni sawa kuziweka hapa.

9/11/2005

Helsinki: Rushwa na Maendeleo

Kati ya mijadala iliyokuwa mikali ni ule kuhusu rushwana maendeleo. Ilikubalika kuwa moja ya chanzo kikubwa cha rushwa katika jamii mbalimbali duniani ni rushwa. Ami Mpungwe wa Namitech East Africa alidai kuwa tofauti na mtazamo wa wengi rushwa sio tatizo la nchi masikini tu. "Tatizo ni kuwa rushwa ikitokea nchi tajiri inaitwa kashfa, ikitokea nchi masikini inaitwa rushwa," alisema.

Naye Waziri wa Serikali za Mitaa wa Kenya Musikari Kombo alidai kuwa tatizo kubwa kwa nchi za Afrika ni kuwa fedha zinazopatikana kwa rushwa Afrika hupewa sehemu ya kuhifadhiwa katika nchi tajiri.

Naye Birgit Errath wa Global Compact akiongea nami kwenye mahojiano kuhusu rushwa alisema kuwa dunia inapoteza kiasi cha cha dola zisizopungua trilioni moja kwa mwaka kutokana na rushwa.

Nini hasa dawa ya rushwa?

Helsinki: Mtengeneza Filamu anayetetea Waislamu

Mmoja wa washiriki wa mkutano wa Helsinki, Naeem Mohaiemen, alisema jambo ambalo limekuwa midomoni mwa wajumbe toka alipozungumza. Naeem ambaye ni mtengeneza filamu (bofya hapa uone moja ya filamu zake) alidai kuwa wakati ambapo mkutano huu nia yake ni kuunganisha washika dau mbalimbali ili kuweza kujenga demokrasia na usawa sauti za waislamu zimesahaulika. Alisema kuwa kutokana na mtazamo wa watu wengi duniani kuhusu waislamu na uislamu ni vyema waislamu wakahusishwa kikamilifu katika miradi kama hii. Pia alitaka wasanii nao kuhusishwa zaidi kwani wao wana uwezo mkubwa wa kushawishi na kuelimisha umma kutokana na kazi zao.

HELSINKI: MALAIKA NAKUPENDA MALAIKA

Jana nilisahau kuelezea jinsi Watanzania "tulivyowakilisha" kwenye tamasha la kufunga mkutano wa Helsinki. Wakati watumbuizaji kadhaa wa hapa Finland wanafanya vitu vyao, Mama Maria Shaba, mwenyekiti wa Tango, alikujanje ya ukumbi kutubeba mkikimkiki. Kisa? Alisema lazima Watanzania tukatumbuize. Da! Sauti tunazo? Akasema lazima. Basi Watanzania wote hao jukwaani. Mama Shaba akashika kipaza sauti na kutambulisha kundi la muziki la Tanzania likiongozwa naye akiwa na sauti ya kwanza na Muhidini Issa Michuzi sauti ya nne. Mimi sauti yangu sijui wala ni ya ngapi. Basi tukashusha Malaika nakupenda malaika huku tukijinesuanesua. Ukumbi ukabaki mdomo wazi, waliokuwa mbali wakasogea karibu, mtu wa taa akazitengeneza vyema, zikatumulika. Tukaimba. Tukawakilisha. Tukashangiliwa. Tukafurahi.
Tulipomaliza malaika ikawa sio mwisho. Tukaondoka ukumbini huku tukiimbisha watu wote kiitikio cha wimbo wa Bob Marley wa Get Up Stand Up....Stand Up for Your Rights....come one everybody...Get Up Stand Up....huku tumenyoosha mkono uliokuja ngumi hewani.

9/10/2005

Helsinki: Onyesho la kumaliza mkutano

Baada ya wajumbe wa mkutano wa Helsinki 2005 kukubaliana kuwa mwaka 2007, serikali ya Tanzania itaandaa mkutano mwingine kutazama utekelezaji wa maazimio ya mkutano huu....na kuwa kabla ya mwaka huo kamati ndogondogo zitakuwa zikikutana kuratibu juhudi za kufanikisha nia ya kujenga demokrasia na kuondoa umasikini, wajumbe waliagwa kwa tamasha kubwa. Kwanza nilitaka kuacha kwenda mkutanoni maana nilikuwa nimealikwa kwenye harusi moja iliyokuwa inavuma maana ilikuwa inasherehekewa kiafrika na pia nilikuwa nimekaribishwa klabu ya Chelsea kukaa na kujiburudisha na Watanzania wanaoishi hapa Helsinki. Lakini baadaye niliamua kuwa nitakwenda klabu ya Chelsea kisha baadaye niende kwenye tamasha. Na ninasema kuwa sijilaumu kwenda kwenye tamasha.

Kwenye klabu ya Chelsea nilishuhudia mjadala mzito sana sana katika ya wajumbe wa kikao kile, au tuiite kiti moto. Issa Michuzi alikuwa ndio mwenyekiti, akikazana kuzuia wajumbe kupunguza hamasa na kuacha kila mjumbe kumaliza anayotaka kusema. Fide alikaribia kupanda juu ya meza akielezea kuwa mifano tunayotoa ya kusema kuwa nchi kama Malaysia na Singapore zilitawaliwa kama Tanzania lakini zimepiga hatua. Mjadala ulikuwa mpana hasa ukigusia karibu kila jambo kuhusu Watanzania, viongozi wetu, na mfumo wetu wa maisha na utawala.

Kwanini Watanzania tuko nyuma hivi? Lilikuwa swali kuu.

Kulikuwa na mtazamo tofauti kidogo kati ya Watanzania wanaoishi nje na wale waliotokea nyumbani. Sikuongea sana, nilipenda kusikiliza. Baadaye usiku nilifikiri kwa undani yaliyozungumzwa nikagundua kuwa kila lililokuwa linasemwa na pande zote lilikuwa ni sahihi. Ingawa kulikuwa na kutokukubaliana kila mmoja akionyesha mapungufu ya uchambuzi yakinifu wa mwingine, ninaona kuwa wote walikuwa wanasema mambo ambayo yana ukweli ndani yake. Kubwa nadhani ni kutafuta eneo ambalo litaweza kuunganisha mitazamo hiyo ambayo kwa juujuu utaona kuwa inakizana.

Basi baadaye mimi na Michuzi na Vkii wa gazeti la mtandaoni la Malyasiakini la nchini Malaysia tukaenda kwenye tamasha ambapo tulikaa hadi leo asubuhi (Michuzi aliwahi kuondoka) na kuishia kuzunguka mji mzima tukitafuta chakula.

Sisiti kusema kuwa onyesho lile, hasa lile la mpiga kinanda cha mkono (accordian) Kimmo Pohjonen ni kati ya maonyesho ya hisia kali sana ambayo nimetazama karibuni. Mama Maria Shaba wa Tango alichoweza kusema ni kuwa, "Huyu bwana alikuwa anafanya tambiko la kujiponya kama tunavyofanya kule Bwagamoyo kwenye sherehe za kupandisha maruhani. Sisi kwetu tunadharau sanaa kama ile huyu unaona alivyoweza kuteka umati."

Kumtazama Kimmo ilikuwa ni kama vile kuwa katika ibada fulani hivi. Matumizi yake ya viungo, sauti, kelele, teknolojia, na taa vilinifanya kujisikia kama niko hekaluni.

Namtafuta Mama Shaba nimwambie kuwa aliitaja Bwagamoyo alipokuwa akimzunguzia Kimmo bila kujua. Kwani baada ya onyesho niliongea na Kimmo. Alinishangaza sana alipoanza kuongea nami Kiswahili. Kumbe amesoma muziki wa asili wa Kigogo kule Bwagamoyo na Dodoma. Na alisema kuwa itakuwa ni dhambi asiponiambia kuwa hakuna mtu hapa duniani anayemweshimu kama marehemu Hukwe Zawose. "Muziki wangu na kila kitu nilichokuwa nafanya naweza kusema ni hisia nilizopewa na Zawose.

9/09/2005

Tumeanua Jamvi

Haya, ndio mkutano umefungwa hivyo. mabango yanaondolewa. Viti vinakusanywa. Vitambaba vya mezani vinakujwa. Picha zinapigwa. Anuani kubadilishana. Mvinyo wa mwisho mwisho. Na karanga pia (ila mpishi kazimwagia chumvi kabisa).
Baada ya miezi michache, kutakuwa na mkutano mwingine utakaoitishwa na serikali za Tanzania na Ufini utakaojumuisha washika dau zaidi ambao kazi yake utakuwa ni kuweka mtandao wa kuhakikisha kuwa maazimio ya mkutano huu yanatekelezwa.
Pichani hapo juu ni Watanzania waliokuwa wakishiriki mkutanoni hapa.

Chakula cha hapa na mengineyo

Sisemi kwa ubaya. Ila sidhani kama rais wa Ufaransa, mzee Chirac, alikosea sana alipotoa mawazo yake mwezi wa saba mwaka huu juu ya chakula cha Kifini. Maneno yake yalikuwa makali kidogo. Jana wakati wa chakula cha usiku, mwandishi mmoja mwandamizi toka Afrika Kusini (amenisihi nisimtaje jina) aliniambia, "Kwetu bwana Macha ukila chakula hiki unakuwa ni sawa tu na mtu aliyelala njaa."
Nikamwambia, "Mbona?"
Akashangaa, "Yaani wewe huoni? Kwani hiki ni chakula? Unajua wajumbe toka India kila siku wanajipikia wenyewe kwa zamu kule jikoni."
Tuache chakula chao, Finland kama hufahamu ni nchi ambayo utenzi uliisaidia ikapata uhuru. Huu ni ule utenzi wa Kalevala. Mwaka 2000 nilishuhudia kundi la Parapanda likiigiza utenzi huu katika juma la makumbusho pale Dasalama. Kaiti ya mambo ambayo nchi hii inajivunia ni kazi za mchora ramani za majengo wa Kifini, Alvaro Aalto. Jengo la Finlandia Hall ambamo mkutano wa Helsinki unafanyika limechorwa na huyu bwana.
Katika mazungumzo na watu mbalimbali kumezuka mjadala kuhusu nchi za Afrika kusemekana kuwa ziko nyuma kimaendeleo kwakuwa zilitawaliwa. Swali hili limeulizwa: iweje Finland iliyotawaliwa karibu miaka 700 na Waswidi na miaka 150 na Warusi iwe mbele namna hii kiuchumi na kijamii?
Kwa mujibu wa Transparency International Corruption Perceptions Index Finland ndio nchi ambayo ina vitendo vichache kabisa vya rushwa. Na pia ndio nchi ambayo ina uchumi wenye ushindani mkubwa duniani kwa mujibu wa the World Economic Competetiveness Index.
Elimu na afya katika nchi hii hutoi hata sumni. Tofauti na nchi ya kibeberu kama Marekani, Finland hakuna shule au vyuo vikuu vya binafsi/kulipia.
Ingawa Finland ni nchi inayoelezewa kuwa tayari imeshaingia kwenye zama za jamii-habari, teknolojia ya blogu bado haijapokewa na wengi. Mmoja wa wanablogu wazuri hapa Finland ni Mmarekani mmoja mtalaamu wa mambo ya kompyuta.

KUNA RISASI MBILI KWA KILA KICHWA DUNIANI

Katibu Mkuu wa shirika la kutetea haki za binadamu, Amnesty International, Irene Khan, akiongea hapa Helsinki jana, alisema kuwa vita dhidi ya ugaidi vimekuwa ni kisingizio cha baadhi ya nchi duniani kutupilia mbali haki za msingi za binadamu.
Akizungumzia kuhusu vita duniani alisema kuwa silaha ndogo ndogo, ambazo ndio zinazotumika katika vita sehemu mbalimbali duniani, ndio hasa silaha za maangamizi. Mataifa makubwa yanayopata faida kubwa kutokana na biashara ya silaha hizo lazima yabanwe ili kuacha biashara hiyo chafu. Zaidi ya watu nusu milioni huuliwa na silaha ndogondogo kila mwaka.
Alimaliza kwa kutuambia kuwa idadi ya risasi zilizoko duniani ni kubwa mno kwani kuna risasi mbili kwa kila binadamu hapa duniani.

9/08/2005

Blogu mpya ya Muhidin Issa Michuzi


Mpiga picha maarufu wa gazeti la Daily News Tanzania, Muhidin Issa Michuzi amekata shauri. Hajakata shauri kumpokea bwana, bali kuwa mwanablogu wa picha (photoblogger). Basi kuanzia leo umtembelee. Ninakuhakikishia kuwa hutajilaumu. Picha zake nimekuwa nazipenda toka zamani. Tumekutana hapa Helsinki. Bofya hapa umtembelee na kumkaribisha.
Kwenye picha hii tuko kwenye tafrija fupi ys kumkaribisha kwenye uwanja wa blogu.

Onyesho la "man free yourself"


Wanaharakati Philipina, Halima, Felista Rugambwa, na Angel Damas tukitazama onyesho la "man free yourself!" ndani ya jengo la Finlandia Hall.

** Picha na Muhidin Issa Michuzi.



Watanzania wanaohudhuria mkutano hapa Helsinki


Muhidin Issa Michuzi kamaliza kutuchukua picha hii. Hawa wote ni Watanzania wanaohudhuria
mkutano hapa Helsinki. Kutoka kushoto ni ndesanjo mwenyewe, Abubakar Rajab ambaye ni katibu mkuu wizara ya kazi na maendeleo ya vijana, Philipina Labia wa shirika la Faraja Human Development Trust Dodoma na mjumbe wa bodi ya TANGO, Halima Zinga wa Chama cha Elimu ya Watu Wazima Tanzania, Angel Damas wa Youth of the United Nation Association (ambaye ndiye miss Tanzania 2005), Abdulkader Shareef (Naibu Waziri, wizara ya mambo ya nje), Felista Rugambwa wa Youth of the United Nations Association (ambaye ni Miss University 2005), anayefuata nitatafuta jina lake, Omary Mjenga wa wizara ya mambo ya nje, na Robert Kahedaguza toka wizara ya mambo ya nje, anayefuata nimemsahau jina ila katoka maendeleo ya jamii

MKAPA AND HALONEN WAKIONGEA HELSINKI


Marais Benjamin Mkapa wa Tanzania na Tarja Halonen wa Ufini wakiongea asubuhi hii. Marais hawa wamesisitiza kuwa muundo wa kisiasa na kiuchumi duniani unahitaji kubadilishwa. Mkutano wa Helsinki ni hatua muhimu katika kutafuta namna ya kujenga duniani ambayo inajali utu na haki za msingi za binadamu. Umuhimu wake unatokana na ushirikishwaji wa washikadau wa sekta mbalimbali.
** Picha kwa hisani ya mpiga picha maarufu wa Tanzaia, Muhidini Issa Michuzi

MAMA SHABA ANAULIZA KAMA KWELI WAAFRIKA NI MASIKINI

Mama Maria Shaba, mwenyekiti wa Tanzania Association of Non-Governmental Organizations (TANGO), aliongea jana wakati wa mjadala kuhusu wanawake na maendeleo. Alisema kuwa kuna umuhimu wa kubadili tafsiri ya umasikin. Alionya kuwa Waafrika wanatakiwa kuwa makini sana kutokana na vyombo vya habari/uongo vya magharibi kusema kila mara kuwa sisi ni masikini. Unapoambiwa kuwa wewe ni masikini kila kukicha mwishowe unaamini kabisa kuwa wewe ni masikini hata kama ukweli ni kuwa wewe ni tajiri.
Akauliza kama sisi ni masikini kwanini mabepari wamekazana kuwekeza Afrika? Kwanini makampuni yao yanapeleka huduma na bidhaa zake kwa waafrika? Na kama ni kweli kuwa sisi ni masikini kiasi ambacho hata fedha wanazodai kutukopesha hatuwezi kulipa kwanini basi wanaendelea kutukopa kila siku??
Hivi sasa kuna kwaya moja inatumbuiza. Kumbe Wafini wanajua kuimba kama wagogo?

9/07/2005

MKAPA ANAONGEA HIVI SASA

Hivi sasa tunamsikiliza rais wa Tanzania, Benjamin Mkapa, ambaye anasema kuwa kizazi chetu ndio kizazi ambacho kinaweza kutazama umasikini duniani na kuamua kuupiga vita na kuumaliza. Sababu ni kuwa tuna uwezo wa kifedha na teknolojia. Anasema kuwa watu wote duniani tunapaswa kujua kuwa dunia hii ni yetu wote na kuishi kama kaka na dada.
Kumbuka unaweza kutazama mkutano huu kupitia mtandao wa kompyuta. Bofya hapa.

HELSKINI: KARIBU NISEME MKONO WA MTU

Nimefika hapa Helsinki kama masaa matatu yaliyopita. Nadhani kama nilikuwa ninaishi Bwagamoyo ingebidi niende kwa Mzee Shomari kutazama nyota yangu isije ikawa ni mkono wa mtu.
Kwanini nasema mkono wa mtu? Ilianza alhamisi jumatano iliyopita nilipotuma pasipoti yangu ubalozi wa Ufini kule New York. Jamaa wa Fedex akaniambia kuwa nitume kwa njia ya gharama kuliko zote ndio itafika haraka. Kwakuwa siku zilikuwa zimebaki mbili kabla wiki kuisha, na jumatatu yake ilikuwa ni sikukuu na ndio nilitakiwa kuondoka, nikafanya alivyoniambia. Basi kifurushi changu kikafika ubalozini asubuhi alhamisi saa moja na dakika ishirini. Ubalozi saa hiyo umefungwa! Kumbe ukituma kwa njia ile ya haraka kabisa kifurushi kinapelekwa asubuhi ya majogoo. Ningetuma kwa njia nyingine kingefika kati ya saa nne hadi saa sita ambapo ofisi ingekuwa wazi. Basi walipokipeleka kifurushi mara ya pili tayari wanaohusika na visa walishaondoka kazini. Hiyo ni alhamisi!
Kijasho kikaanza kutoka. Ijumaa baada ya kupiga simu mara tisa, kila mara nikiambiwa kuwa maofisa wa visa wana wageni, nilipata nafasi ya kuongea na anayehusika. Akasema amepokea maombi asubuhi hiyo ya ijumaa, ila tatizo ni kuwa kompyuta zina matatizo. Kama zikiwa zimeshatengenezwa kwenye saa sita atashughulikia, kama bado basi hatakuwa na la kufanya.
Kijasho kikazidi.
Saa nane nikapiga simu kuulizia. Nikaambiwa ameshatoa visa na kutuma kwa Fedex kwahiyo nitaipata jumamosi. Basi jumamosi nikasubiri weeeeeeeee.......wapi! Nikapiga simu kwa jamaa wa Fedex...yapata saa kumi jioni. Dada upande wa pili wa simu akatema maneno yaliyonimaliza nguvu kabisa. Akasema, "Desanjo Maka....." (Hivi ndivyo wengi wanatamka jina langu.) Kisha akasoma anuani na kuniuliza kama ni yangu. Nikajibu ndio. Akasema kuwa pasipoti yangu iko jimbo la Indiana na haitanifikia hadi jumanne wiki inayofuata (yaani jana) kwani jumatatu ilikuwa ni ni sikukuu!!
Mkono wa mtu!! Au ni kisirani tu ambacho naweza kukiondoa kwa kuoga kwa magadi???
Nifanyeje? Niende Indiana nikaichukue? Siwezi maana kisheria Fedex hawawezi kunipa hadi walete kwenye anuani inayotakiwa.
Haya. Ikabidi nibadili tiketi ili niondoke jummane kwani jamaa wa Fedex waliniambia kuwa nitapata kifurushi changu kabla ya saa nne na nusu asubuhi. Basi jummane asubuhi nimejiondokea zangu kwenda sehemu kwa dakika chache. Narudi nyumbani saa tatu nakuta karatasi inayosema kuwa jamaa wa Fedex ameniletea kifurushi ila kwakuwa hakunikuta ameondoka na ataleta tena kesho, yaani jumatano!
Kijasho tena...mkono wa mtu!
Nikapiga simu Fedex wakaniambia kuwa watamfuta derevea kwa njia ya simu ili wamwambie alete tena. Mpaka saa sita kasoro jamaa hajaja. Ndege inaondoka saa nane. Nikapiga simu tena Fedex. Wakaniambia kuwa bado wanajaribu kumtafuta dereva!
Kwanini nisiache kwenda? Nikaanza kujiuliza maana kukaa kiroho juu namna hii huwa sipendi. Lakini wakati huo huo nataka kunywa chai na kaka Ben na Jakaya. Saa sita inapofika jamaa wa Fedex huyo.
Nikapumua. Huyo mbio uwanja wa ndege. Kufika uwanja wa ndege nikakuta kumbe mambo bado. Jamaa wa Northwest Airline wanasema wanaona kuwa ninatakiwa kusafiri ila hawaoni tiketi...baada ya dakika kumi wananiambia kumbe natakiwa niende Continental Airline. Huko nako ilichukua dakika karibu 20 kabla hawajaweza kuona tiketi yangu. Lakini kabla hawajanipa lazima waende Northwest Airline...sikutaka wala kujua wanaenda kufanya nini. Nikabaki nawatazama wanaongea, wanaangalia kwenye kompyuta, mara wakapiga simu...zimebaki dakika 25 ndege kuondoka!
Haya, mwishoni nikapata tiketi. Sasa yule jamaa anayekagua mabegi akaanza kukagua begi langu kama vile ndege yangu inaondoka kesho...Naona itabidi nianze kuweka nyoka ndani ya begi. Jamaa kavuruga kila kitu nilivyopanga ndani ya begi. Viatu kule, nguo huku...ovyo.
Haya kuelekea ndani ya ndege. Kama kawaida (hii hunitokea mara zote ninazosafiri na kila mara nauliza wananiambia kuwa kinachochagua nani akaguliwe kwa kina ni kompyuta) nikaambiwa niende pembeni na kuanza kusachiwa kwa ustadi zaidi ya wengine na kuulizwa ninakokwenda, kuna nini, nani kanunua tiketi, ililipiwa kwa kadi au fedha taslimu na mambo kama hayo.
Basi nikapanda ndege hadi Newark, New Jersey. Pale nikapanda ndege nyingine ya kwenda hadi Amsterdam. Nikakuta kizaazaa kingine. Tiketi yangu ni 15E. Hapo kwenye kiti hicho kuna jamaa mwingine mwenye tiketi nambay 15E!! Suluhisho likapatikana. Nikakaa pengine.
Nafika Helsinki ndani ya basi nakutana na mhariri wa gazeti la mtandaoni la Malaysiakini, ndugu Vicknesan. Tunatazama ratiba tunakuta tumechelewa kongamano ambalo lilikuwa ni muhimu sana kwetu kuhusu vyombo vya habari. Tunakwenda hotelini na bila kubadili nguo (ndio, wala hatukuoga!) tunakwendá kwenye jumba la mkutano. Tunakuta wajumbe ndio wanatoka chumba cha mkutano.
Hivi sasa Maria Shaba wa Tanzania anaimba kufunga semina kuhusu wanawake na maendeleo duniani. Wimbo unakwenda:
I love my sisters
Deep down in my heart...
Kukumbusha ni kuwa ninahudhuria mkutano wa Helsinki kuhusu utandawizi na domokrasia. Matangazo ya mkutano huu yanarushwa moja kwa moja mtandaoni. Bofya hapa.

9/05/2005

Tovuti za habari za uchaguzi Tanzania

Tayari wameanza kuzunguka huku na kule. Wauza maneno. Wamebeba mabakuli, vikapu, makopo, viroba, n.k. vilivyojaa hadithi tamu tamu. Mwaka huu ukikosa ubwabwa, basi usikose fulana. Ukikosa fulana, jitahidi usikose mshiko. Ukikosa mshiko basi lazima upate udirinki kwenye viti virefu.
Ndio, uza nchi na utu wako kwa sahani ya ukoko wa ubwabwa. Hapana, akikupa ukoko usimpigie kura...hadi akupe utando.
Ndio umefika ule wakati. Tazama tovuti ya Kura Yako na Uchaguzi Tanzania kwa habari za mchezo huu wa kuigiza utakaofikia kilele chake mwezi wa kumi.

9/03/2005

Wanablogu niliowachagua wanasemaje?

Siku ya Blogu Duniani nilichagua, kama jinsi taratibu za siku hiyo zilivyokuwa, wanablogu watano. Baadhi yao wamesema haya:

Kongoli hapa uone aliyoandika Jilltxt kwenye blogu yake juu ya kuchaguliwa.

Mwanzilishi wa blogu hii hapa kwa ajili ya maafa ya Katrina, Andy Carvin, ameniandikia ujumbe huu: Thanks! I truly appreciate it.

Naye Marianna wa blogu hii hapa ameaniandikia ujumbe huu: Thank you! I surely couldn't read Kiswahili but I thank you for giving me the opportunity to tell your readers about Azerbaijan.

9/02/2005

Rangi wa "wanaoiba" na rangi ya "wanaochukua"



Baadhi wameshinda kufungua picha nilizokuwa nazungumzia zinazoonyesha chembechembe za mtazamo wa kibaguzi ambao umejificha kwenye vyombo vya habari hapa Marekani. Bonyeza juu ya picha kuikuza ili usome maelezo yake vizuri. Tazama maelezo ya picha ya mweusi yanaonyesha kuwa yeye ni kibaka. Na picha za weupe, maelezo yanaonyesha kuwa wao wamejichukulia tu chakula (ingawa hawakupewa na wenye duka)!

Hivi sasa taarifa zaidi zinaanza kutoka katika vyombo vya habari kuonyesha jinsi ambavyo rangi ya wahusika wengi katika janga la Katrina imechangia kufanya juhudi za msaada kwenda polepole zaidi ya kinyonga. Wakati huo huo vyombo vya habari vimechukua habari ya maduka kuvunjwa kuwa ni kubwa zaidi ya maelfu ya watu wasio na chakula, madawa, maji, makazi, n.k. Wakati ambapo barabara zimejaa maiti zinazoliwa na mapanya. Wakati ambapo watoto wachanga wanakufa kwa njaa...ndani ya Marekani! Hata serikali yenyewe imetuma wanajeshi, sio kwenda kuokoa watu bali kulinda usalama wa maduka na mali nyingine za matajiri. Askari hao wameambiwa wasisite kufyatua risasi, sio kuvunja mguu bali kuua. Baadhi ya watu ndio wanang'amua kumbe ni kweli kwenye ubepari kitu muhimu ni kile kiitwacho "private property" zaidi ya uhai na heshima ya binadamu masikini. Ndio maana unaona askari wanatumwa kwenda kuzuia uporaji wa mali za matajiri na sio kusaidia masikini wasiojua waende wapi au wafanye nini. Wamepoteza hata kile kidogo walichonacho.

Nakwenda Helsinki

Jumatatu ijayo ninaondoka kwenda kwa Wafini (nchini Finland). Nitakuwa katika jiji la Helsinki kushiriki na kublogu mkutano wa Helsinki 2005 kupitia mradi wa Sauti ya Dunia na Wizara ya Mambo ya Nje ya huko Ufini.. Kwa kuwa mkutano huo unahudhuriwa na rais anayemaliza muda wake na pia rais ajaye wa Tanzania, huenda nikapata nafasi ya kunywa nao kahawa kujadili "maendeleo" ya nchi.

Hivi sasa ninajisomea mambo mawili matatu kuhusu nchi hii. Mwandani, asante kwa simu ya "meya" wa jiji la Helsinki.

Nitaandika zaidi juu ya safari hii.

Msangi Mdogo na Msangi mwingine washiriki Siku ya Blogu Duniani

Kumbe Msangi Mdogo naye ameshiriki kwenye Siku ya Blogu Duniani kwa kuchagua wanablogu wake. Msome hapa. Msangi kichwa cha blogu yake kinanifurahisha. Kinasema: Tukazane Kujenga kwa Mioyo Yetu, Mtafune kwa Meno Yenu?

Hajasema anazungumzia akina nani, ila najua mimi na wewe tunafahamu ni akina nani hao anawarushia madongo.
Jeff Msangi ambaye anablogu toka Kanada kwa kiingereza na Kiswahili naye hakubaki nyuma. Hizi hapa ndio blogu alizochagua kwa ajili ya siku hiyo.
Sijawahi kuwauliza akina Msangi kama ni ndugu. Labda.

Wanablogu Nipendao Kuwasoma Wametimiza Mwaka

Wanablogu wawili ninaopenda kuwasoma toka Kenya wanasherehekea kutimiza mwaka mmoja toka waanze kublogu. Wanablogu hawa wamekuwa ni mfano wa kutia moyo kwa wanablogu wengi toka Afrika na kwingne. Nawatakia kila la heri.
Na hao sio wengine bali ni Mshairi na Mama Junkyard's. Wanablogu hawa hivi sasa wanaishi kwa Bibi Lizabeta.

Mwanablogu wa Kiswahili achaguliwa kwa Siku ya Blogu Duniani

Nilikuwa natazama wanablogu wa Kiswahili walioshiriki kwenye siku ya blogu duniani. Katika pitapita nimekuta kumbe kuna mwanablogu wa Kiswahili aliyechaguliwa. Mawazo na Mawaidha katika orodha ya wanablogu wake watano amemchagua mwanablogu mpya wa Kiswahili. Huyo ni mtaalamu wa uchawi wa kizungu, ndugu Swai. Blogu ya Swai sijui jinsi ya kuielezea. Ninadhani Swai ni mpenda ucheshi sana.

9/01/2005

Nini Tofauti ya Kuiba na Kuchukua Kisicho Chako?

Tofauti ya kuiba na kuchukua ni hii: watu weusi ndio huiba na weupe huchukua!
Maafa ya kimbunga cha Katrina hayaelezeki. Wakati maafa haya yakitawala vyombo vya habari kuna habari moja ambayo huenda imekupita. Habari hiyo ni kuhusu picha mbili ambazo zimezua mjadala kwenye mtandao wa kompyuta. Picha moja, hii hapa, inamuonyesha kijana mweusi akiwa na bidhaa kadhaa. Maelezo ya picha hiyo yanaonyesha kuwa huyu kijana katoka kuiba kwenye grosari moja. Picha nyingine, hii hapa, inaonyeshwa watu weupe wawili, nao wakiwa "wamechukua" mikate na soda toka kwenye grosari moja. Ila maelezo ya picha hii hayasemi kuwa wameiba. Tunaambiwa kuwa wamebeba mikate na soda "waliyoikuta" kwenye duka moja. Kwa maneno mengine hawa weupe hawakuiba bali walichukua. Ila yule mweusi ameiba!
Sasa mjadala huu umepelekea jamaa wa Yahoo! kuondoa picha hiyo ya watu weupe. Halafu wametoa tamko hili. Ajabu ni kuwa ile ya mweusi "aliyeiba" imeachwa. Wameona kuliko kubadili maneno na kusema kuwa wale weupe nao wameiba ni afadhali waitoe ile ya weupe na kuacha ya jamaa weusi "wezi."

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com