9/27/2005

Gumzo Kuhusu Kiongozi cha Wanablogu na Wanaharakati Mtandaoni

Lile gumzo na mkurugenzi wa masuala ya intaneti wa Wanahabari Wasio na Mipaka kuhusu kitabu kipya kiitwacho Handbook for Bloggers and Cyber-Dissidents limemalizika. Unaweza kusoma yote yaliyozungumzwa katika gumzo hilo lililotumia teknolojia ya Internet Relay Chat. Nenda hapa.

1 Maoni Yako:

At 9/27/2005 05:05:00 PM, Anonymous Anonymous said...

Kwa Ndugu Ndesanjo,

Nafurahi kupata nafasi hii kukuandikia kwani muda mrefu nimekuwa na lengo hili. Nimesoma, hoja zako mbili tatu katika magazeti ya nyumbani Tz na ni ya kuelemisha tosha. Naomba usichoke kutuelemisha kwani upeo na uelewa wako ni mkubwa. Umetembelea mataifa na watu mbalimbali duniani kitu ambacho kwa wenzio ni ndoto.

Mfano, huko Helisinki ulikokwenda umetutonya kuwa mama mmoja kasema nchi zetu si masikini. Tumeelimika hapo wenzio. Kwa upane mmoja ni kweli, mfano Tz tu masikini vipi rasilimali zote za maendeleo? (1) watu karibia milioni 40 (2) ardhi yenye rutuba (3) hali ya hewa isiyoua kwa baridi au joto kali (4) nchi isiyo matetemeko wala vimbunga (5) maji baridi na maji chumvi bwerere (6) mbuga za wanyama, misitu hadi lwamba (7) madini nchi nzima (8) lugha moja kama jua duniani, maajabu hayo, eti masikini!!. Wakati mkono mtupu haulambwi, hao matajiri kila kukicha wanafuata nini kwa masikini ?. Sijui! lakini nakubaliana na huyo mama 100%, tumeitwa maskini tukalipokea bila kupinga hadi kujibatiza jina hilo sisi wenyewe!!.

Lakini kwa upande wa pili, si kweli, na nampinga huyo mama kwa 200%! kwani tu masikini wa ki-kwelikweli na waziwazi. Kisa, hatuna ELIMU. Sasa je, asiyesoma ana-utajiri gani hata awe na rasilimali zote duniani?. Akiwa nazo atamtafuta msomi aje amshauri jinsi ya kuzitumia. Wasomi wetu toka enzi wakiitwa wanakuja kushauri jinsi ya kudhani unazitumia wakati kumbe wanakuibia. Tulikubali elimu ni UTI wa mgongo wa taifa na ndiyo msingi ya utajiri na maendeleo ya nchi lakini hatukuelewe kuwa itakuwa hivyo tu endapo itaambatana na UBONGO wa taifa ambayo ni lugha ya kwanza au ile inayounganisha jamii katika nchi hiyo (uti wa mgongo hauna manufaa bila ubongo?). Na ndiyo hapo tulipotetereka. Hivyo wa-Tz tuongelee elimu pale tu kiswahili kitakapoanza kutumika katika ngazi zote za mafunzo. Kuendelea na lugha za kigeni ambazo kwa watu wetu wengi siyo hata lugha ya pili, ni sawa sawa na kupanda shambani makuti kwa kudhania kuwa umepanda miche ya minazi.

Tusome kwa kiswahili watoto waelewe kinachofundishwa kisha waelimike ili na jamii yote ishirikishwe katika elimu papo kwa papo. La sivyo, tunakoelekea, tunalea maafa makubwa kuliko yote yaliyokwisha kutupata. Si utumwa, ukoloni, ukoloni mambolea, utandawazi, n.k.

Wasalaamu

Masumbuko

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com