7/02/2005

maandamano na tamasha la Live 8

Leo watu, nadhani ni zaidi ya laki mbili, wameandamana katika jiji la Edinburgh. Nilikuwa katikati ya msongamano wa watu waliokuwa wamebeba mabango, wakipiga ngoma, filimbi, wakicheza, wakisambaza vipeperushi, n.k. Waandishi wote tulikwenda kwa pamoja lakini muda sio mrefu tulishapoteana. Kazi kubwa niliyokuwa nikifanya ilikuwa ni kuongea na waandamanaji toka Afrika. Nimekutana na Waafrika toka Tanzania, Uganda, Nigeria, Ghana, Msumbiji, n.k. Mimi nilirudi yapata saa tisa nikiwa nimechoka kabisa. Kwakuwa ninafanya kazi kwenye blogu mpya ya Panos na pia tovuti yao, nitakuwa naandika kifupi hadi nikipata muda wa kutosha. Hivi sasa tamasha la Live 8 linaendelea. Tunatazama kwenye luninga. Muda mfupi uliopita alikuwa akiimba Mariah Carey. Jukwaani alipanda na kwaya ya watoto wa Afrika Kusini, ambao ni yatima kutokana na wazazi wao kufariki kwa Ukimwi. Kama saa moja lililopita, ilionyeshwa filamu ya wimbo aliyotumia Bob Geldof kuchangisha fedha kwa ajili ya baa la njaa Ethiopia. Mara akashangaza watu pale alipoonyesha picha ya mmoja wa watoto walionekana kukaribia kufa kwa njaa na kusema kuwa mtoto huyo alinusurika na kuwa yuko Hyde Park, London. Mara binti mmoja mzuri mno akajitokeza na kusalimu kwa lugha ya Amharic. Baada ya hapo Madonna alipanda jukwaani na kumkumbatia binti huyu na kumbusu kwenye pambaja za mdomo. Mmoja wa wahariri tulio nao hapa akashtuka, "Ah, anambusu Madonna!"

Hivi sasa kuna jamaa anaimba ambaye simfahamu na sidhani kama nina nia ya kumfahamu!

Toka tuanze kutazama nimemuona Kanda Bongo Man na Youssou Ndour wakitumbuiza kule katika ukumbi walikopelekwa wanamuziki toka Afrika. Kamera zikielekezwa huko tunaonyesha dakika mbili kisha tunarudishwa kwa wanamuziki weupe. Dunia hii ya ajabu sana, Hata wale wanaodai wanatetea masikini na Waafrika wanatakiwa kusaidiwa sana kuondokana na kitu wazungu wanaita White Supremacy, dhana kuwa weupe ni bora kuliko watu wengine duniani.

Tazama blogu ya Panos hapa.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com