7/04/2005

Monbiot: Bara Zima La Afrika Litakuwa Mali ya Makampuni

Leo mji ulisimama. Maanakisti walikuwa wakifanya vitu vyao. Toka asubuhi hadi usiku saa mbili barabara kuu hapa Edinburgh, Princes, ilikuwa imefungwa. Askari wa kuzuia fujo walikuwa wametanda kila mahali, helikopta zikizunguka angani. Waandamanaji wenye msimamo mkali na itikadi inayopinga aina yoyote ya utawala walikuwa wakipimana na polisi. Polisi na waandamanaji hawa walitazamana siku nzima. Polisi wakiwa wamebeba ngao na vikopo vya gesi walizuia njia, maanakisti wakasimama barabarani hapo wakipiga ngoma, filimbi, wakiimba, na kucheza. Nilipopita mitaa hiyo kwenye saa kumi na moja jioni na mwandiki toka Kenya, John Kamau, tulijiuliza kama maandamano hayo yalikuwa yakifanyika Kenya au Tanzania ni kitu gani kingetokea? Tulisema, kwa utani, kuwa Waingereza wangetuma ndege ikachukue Askari wa Kuleta Fujo (wao hujiita askari wa kuzuia fujo) toka Kenya na Tanzania ili wawaonyeshe jinsi ya kuwashughulikia waandamanaji.
"Hivi unadhani askari wa Bongo au Kenya wangeweza kusimama wakitazamana na waandamanaji siku nzima?," nilimuuliza Kamau.
"We, askari kule nyumbani wana muda wa kupoteza? Saa hizi watu wangekuwa wanapelekea ndugu zao chakula cha jioni hospitali na wengine wakitafauta namna ya kuwatoa ndugu zao vituo vya polisi." Alinijibu. Mwandishi toka Sierra Leone Salamatu Turay amechukua picha hizi toka kwenye maandamano hayo. Mwandishi wa BBC Paul Mason naye ana picha toka katika maandamano hayo.
Maandamano haya yalikuwa yameandaliwa na jamaa ambao wamekuja hapa Uskoti kuwazuia wezi nane wanaotaka kukutana kuzungumzia jinsi ya kuifanya dunia kuwa shamba la mtu binafasi.

Leo tumekutana na kufanya mahojiano na mwanasafu wa gazeti la the Guardian George Monbiot. Monbiot amewahi kufanya kazi nchini Tanzania na Kenya. Moja ya mambo aliyokuwa anazungumzia leo ni suala la mbinu za viongozi wa nchi nane kutaka kubinafsisha bara zima la Afrika. Anasema kuwa tatizo moja la kampeni kama Make Poverty History na Live 8 ni kuwa kampeni hizi hazitishii madaraka na maslahi ya mfumo wa ubepari. "Watu wanadhani kuwa unaweza kuondona umasikini bila kuondoa mfumo wa soko huria." Monbiot anaamini kuwa mfumo wa soko huria ni moja ya vyanzo vya umasikini duniani. Anasema kuwa lazima tuanze kuelewa ubaya wa mfumo huu kwa kutazama jinsi ambavyo viongozi wa nchi nane tu duniani wana uwezo wa kutoa maamuzi juu ya wananchi wote duniani. Nchi hizi nane ndio pia zenye nguvu za kupitisha maamuzi yao kwenye vyombo kama Benki ya Mabepari (benki ya dunia), Shirika la Fedha Duniani, Umoja wa Mataifa, n.k.

Monbiot anasema kuwa wanachofanya viongozi wa nchi nane zinazoongoza kwa wizi duniani ni kutoa maamuzi yanayoonekana kama vile nia yake ni kusaidia watu masikini, vyombo vya habari vinaingia kwenye mtego, na watu kama Bob Geldoff na Bono wanashangilia kwa kunywa mvinyo na viongozi hao. Viongozi wa Afrika, alituambia, wanachofanya hivi sasa ni kukubali lolote lile ambao wanaambiwa na viongozi wa nchi za Magharibi. "Wanampenda sana rais wako Benjamin Mkapa." Aliniambia huku akicheka. Nilimwambia kuwa nikiona kiongozi anapendwa na kukumbatiwa na mtu kama Kichaka au Blair, ninakuwa na mashaka sana na kiongozi huyo. Kiongozi wanayempenda ni yule ambaye anawasaidia katika jitihada zao za kuliweka bara la Afrika katika mikono ya makampuni ya marafiki zao.

****************************************************************************

Mwandishi toka Sierra Leone, Salamatu Turay, ambaye tuko naye hapa Edinburgh ameandika makala kwenye gazeti la hapa Uingereza juu ya maandamano ya kwanza ya amani aliyohudhuria maishani mwake. Gazeti hili kila siku litakuwa habari tutakazokuwa tukiandika kwa mtazamo wa Afrika.

John Kamau toka Kenya
ameandika makala nzuri sana kwenye gazeti la The Guardian.

2 Maoni Yako:

At 7/04/2005 10:05:00 PM, Anonymous Anonymous said...

Bara wamelichukua toka siku nyingi

 
At 7/05/2005 01:05:00 AM, Anonymous Anonymous said...

Ukikutana na Mkapa utashangaa jinsi mtakavyotofautiana. Atakuambia kwake ni heshima kubwa kualikwa. Si kila siku unamsikia akijisifu kwamba nchi wahisani zina imani naye? Sijuhi anaongoza wahisani?

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com