11/30/2004

ENZI ZA JESHINI

Nimekumbuka jeshini! Da! Historia ile sitakaa nisahau. Nakumbuka siku naondoka na Nickson Malisa kuelekea tusikokujua. Kwanza tulipangwa kwenda kule Mgambo, Tanga. Mwanzoni tulitaka kujipeleka…ile kambi ya Arusha inaitwaje tena? Nimeisahau jina. Hata hivyo tukaamua kuelekea Tanga. Lakini tukiwa ndani ya basi tukaamua kwenda Maramba badala ya Mgambo. Tulisikia habari za kutisha kuhusu Mgambo na habari njema kuhusu Maramba. Basi hao tukamua kuchagua kambi wenyewe. Wakati huo tayari tumeshachelewa kuripoti. Tarehe zilishapita siku nyingi. Tukaingia Maramba jioni jioni hivi na vibegi vyetu na makubazi. Nakumbuka tulikuwa tunapenda sana kuvaa soksi za bluu na yale makubazi. Tulipoingia Maramba tuliamua kuwa hakuna haja ya kuripoti. Kuripoti kosa. Soo. Tulikuwa tunatumia mbinu za juu kabisa za kikachero. Ukifika mahali, kaa chini. Tafuta wajuaji. Ongea nao. Chunguza, “Kilitoka wapi, kikaishia wapi.” Hii ilikuwa ndio mbinu yetu ya kwanza.

Na wajuaji ndio akina nani? Wajuaji si wengine bali ni wale wanaolipia siku. Wale ambao hawajaruhusiwa kwenda nyumbani na wenzao kutokana na makosa kama utoro. Hawa ndio tuliwatafuta giza lilipoingia. Tuliingia bweni hadi bweni tukiwatafuta na kuongea nao. Nakumbuka, kama kumbukumbu hainihadai, kuna bwana mmoja ambaye hivi sasa anaishi Kinondoni. Nadhani ni fundi wa elektroniki. Alisoma Chuo cha Ufundi Mbeya. Basi huyu alikuwa ni mmoja wa jamaa waliotupa “picha” halisi. Jamaa poa sana. Usiku huo baada ya kuongea na watu kadhaa, tukaenda pembeni (mimi na Nickson Malisa) na kuanza kuchambua taarifa tulizokusanya. Kabla jimbi hajawika tulishaamua kuwa Maramba sio kambi yetu. Tutakaa hadi kesho yake usiku, kisha tutatoroka.

Sasa swali likaja, kwakuwa tunatoroka na hatutaki kujiandikisha, tutafanya nini siku nzima ili tusishtukiwe?

Wazo hili sijui nani alikuja nalo kati yangu na Nickson. Kesho yake asubuhi wakati jamaa wengine wanaelekea kwenye “kazi za ujenzi wa taifa” sisi tulielekea nje ya ofisi ya mkuu wa kambi! Tulijua kuwa watu wanaongopa sana eneo lile. Afande yeyote akituona pale hawezi kutubugudhi. Lazima atajua kuwa tumeamriwa kusubiri mtu hapo. Basi tulikaa pale hadi saa ya kula. Tukaenda kula. Wakati tunachukua chakula tukashtukiwa. “Sura ngeni hizi.” Tukajitetea ni wageni na tumetakiwa tuonane na mkuu wa kituo na anavyotuona hivyo tukimaliza chakula tunaenda ofisini kwake. Tukala, kisha hao tukarudi kwenye “ofisi” yetu. Tukasimama nje ya ofisi ya mkuu wa kituo tukipiga gumzo na kubishana. Tulikuwa tunapenda kubishana sana enzi zile. Kubishana na kucheka. Na kuzidi watu akili! Hakuna kitu kilichotufurahisha kama kuzidi watu akili. Hasa watu kama maafande.

ITAENDELEA
***************************************++*****************************************
Nabakisha uhondo kwa ajili ya siku nyingine. Njoo nitaendelea. Nitakupa pia na kisa cha kambi ya Ruvu nilipokutana na bwana Obey Nkya amekusanya watu anahubiri ukombozi…Obey, mpaka leo sikumalizi. Sitakaa nisahau pale Ruvu. Mimi na Nickson tulikutazama kisha tukatazamana na kusema, “Huyu jamaa ni nani? Lazima tujuane naye.”

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com