8/10/2004

Hii Ni Dar Es Salaam

Kawaida mimi hutembea na kitabu cha kumbukumbu. Naandika matukio, mazungumzo, visa, mikasa, na masuala yote ninayoona yanafaa kurekodiwa na mwandishi mpita njia. Hii ni sehemu ya mambo niliyoandika nilipokuwa Dar mwaka jana. Soma:

DAR ES SALAAM, 2003
Zimepita siku kadhaa toka niwasili ndani ya Bongo. Niko ndani ya basi katika kituo cha mabasi Mwenge. Naelekea Mbezi Beach.
Mpiga debe anadai shilingi 100. Kondakta anagoma kutoa. Mpiga debe anakuja juu. Kondakta anakuwa mbogo. Mpiga debe naye anakuwa simba mla watu. Hasira zinawapanda kwa kasi ya mwanga. Mishipa inawatoka. Damu inachemka. Mpiga debe anatoa vitisho. Kondakta anatoa matusi. Vitisho. Matusi. Mate yanaturukia abiria. Matusi yanatuparamia. “Twende mnasubiri nini?”, abiria wanakuja juu. Mpiga debe anatafuta jiwe. Kondakta anachomoa chupa toka chini ya kiti. Wanatishiana. Abiria mmoja anayenuka pombe ananyanyuka na kumaka, “Yuko wapi? Aje huku tumwonyeshe kilichomyoa kanga manyoya.” Hivi ni nani alinyoa kanga manyoya?

Basi linaondoka kituoni kwa kasi. Tunabaki na mlevi ndani ya basi. Ataongea njia nzima. Jambo moja ambalo haachi kusema kila baada ya dakika mbili ni, “Mimi sijalewa hata kidogo. Mtu asije akafikiri kuwa nimelewa.” Hivi kwanini walevi hupenda kusema hawajalewa hata wakati ambapo hakuna aliyesema kuwa wamelewa? Huenda mlevi huyu akifika nyumbani ataamsha wanawe bila sababu. Huenda mke wake akapata kipigo bila kosa lolote. Njia nzima anashusha lawama nyingi tu kwa Mkuu wa Mkoa, Makamba. Makamba ameamuru baa zifungwe mapema. “Yaani anataka tukanywe bia nyumbani? Hana akili kabisa. Nani kamwambia bia ya nyumbani ina ladha? Nyumbani watu tunakunywa chai na maji. Bia ni baa sio nyumbani!” Anaongea kwa sauti ya juu.

Harufu ya pombe iliyochanganyika na mdomo unaonuka vinachafua zaidi hewa nzito na jasho ndani ya basi. Tumejazana. Joto ni kali. Hewa ni nzito. Mlevi anaendelea, “Hivi nyie makonda na wapiga debe wenu, nani aliwaambia kuwa abiria hatujui mabasi ya kupanda mpaka mtuelekeze?”

Hadi hivi sasa mimi bado najiuliza hili swali. Na jingine: nani alimyoa kanga manyoya? Mpiga debe yule naye bado hajui nini kilimyoa kanga manyoya. Walalanjaa wa nchi hii nadhani hivi sasa wanajua kilichomsibu kanga. Maisha yao ya kila siku ni sawa na mtu anayeonyeshwa cha “mtema kuni”.

Hivi mtema kuni alifanya nini? *****************************XXX******************************

1 Maoni Yako:

At 8/12/2004 08:04:00 PM, Anonymous Anonymous said...

Mtema kuni alitema kuni.

 

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com