1/29/2005

NINATAMANI SANA SANA...

Ninatamani mambo mengi. Mojawapo ni hili: Ninatamani sana siku moja nikutane ana kwa ana na wananchi wanaoitwa, "wananchi wenye hasira kali." Hawa ni wale ambao wakisikia, "mwizi!" damu inawachemka, wanatafuta mawe, mitaimbo, nyundo, matairi, bisibisi, patasi, petroli, na viberiti ili wamuue mtu ANAYEDAIWA kuwa mwizi.

Ukikuta hawa wananchi wenye hasira kali wanaua binadamu mwenzao, mtafute aliyewasha kiberiti, kisha muulize, "Hivi jamaa kaiba nini?" au, "Kamwibia nani?" Utasikia majibu ya ajabu kweli.
"Ah, jamaa wanasema kaiba mtaa wa pili." Atakujibu. Anayekujibu hivyo ndiye aliyewasha moto uliomteketeza marehemu. Ukimuuliza akutajie majina ya hao " jamaa wanaosema" kuwa kaiba mtaa wa pili, atakachoweza ni kuwataja kwa jina la "jamaa." Atasema, "Jamaa waliomkamata ndio walimuona."
Jamaa ndio akina nani hao?
Hajui.

Msimamishe yule aliyemwangushia tofali kichwani lililomfanya marehemu atoe damu puani na machoni. Muulize swali, "Kafanya nini marehemu?"
Atakujibu, "Wamezidi hawa!"

Nimesema kuwa ninatamani sana kukutana na "wananchi wenye hasira kali." Nataka kuwauliza swali hili: Wezi wa kuku mnawapeleka jela. Wezi wa shilingi 1,000 mnawapiga mawe na kuwachoma moto hadi kufa, JE WEZI WA MAMILIONI YA UMMA MNAWAFANYA NINI?
Hizo "hasira kali" zinakuwa wapi wakati nchi ikipigwa mnada??

Natamani sana sana kukutana nao. Ukikutana nao naomba nisaidie kuwauliza swali hilo kisha nitumie majibu.
***********************************************************************************
Yesu akauambia umati, "Asiye na dhambi awe wa kwanza kurusha jiwe." Mara wakaondoka mmoja mmoja na kumwacha na yule mwanamke aliyeshatakiwa kwa uzinzi.

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com