10/29/2004

TOVUTI YA HIP HOP SUMMIT TANZANIA NA KISWAHILI

Desemba mwaka huu wana Hip Hop wa Tanzania watafanya mkutano mkubwa katika ukumbi wa Diamond Jubilee. Kwa habari zaidi tembelea tovuti yao kwa kubonyeza hapa. Nimepata tarifa hizi toka kwenye blogu mpya ya Furahia Maisha Yako.
Wale tunaona kuwa lugha yetu ya Kiswahili ina umuhimu sana katika ujenzi wa taifa na utamaduni wetu, tunashindwa kuelewa kwanini Watanzania wamelewa namna hii huu mvinyo wa utumwa wa kifikra. Wazo la Hip Hop Summit na tovuti yao ni zuri mno. Ninawapongeza. Kutumia muziki na falsafa nzima ya hip hop kama moja ya njia ya kupambana na tatizo la ajira kwa vijana nchini Tanzania ni wazo la kuungwa mkono na kila mtu. Lakini swali langu kila siku ni hili: kama unaanzisha jambo kwa ajili ya Watanzania kwanini unatumia lugha ya watu wengine?? Hili ni swali la msingi. Nimetembelea hii tovuti ya hip hop summit nikajiona kama ninasoma jambo linalohusu Marekani, Canada, au Uingereza. Kumbe ni jambo linalotuhusu Watanzania. MOja ya madhumuni ya hip hop summit ni kuwaunganisha watu wote wanaohusika katika nyanja ya muziki huu, kubadilishana mawazo na kutazama jinsi ambavyo muziki unavyosaidia kuondoa tatizo la ajira na umasikini Tanzania. Kama nia yao ni hii, kwanini webu yao wameandika kwa kiingereza? Kwanini wameita Hip Hop Summit? Hao vijana wanaowazungumzia ambao hawana ajira na masikini wanatumia lugha gani katika maisha yao ya kila siku? Mara nyingi vyama, mashirika huanzishwa kwa ajili ya wafadhili, kutokana na sababu hii utaona majina ya mashirika au vyama hivyo ni ya kiingereza (lugha inayotumiwa na hao wafadhili). Nimetembelea tovuti yao kutafuta kiswahili bila mafanikio. Tukumbuke kuwa wanamuziki ndio watatumia uwezo na ubunifu wao kutuondoa katika utumwa wa fikra. Ukombozi wetu na mapambano dhidi ya umasikini Tanzania mwanzo wake ni kwenye fikra.

Tafadhali nenda kwenye hii webu. Waandikie hawa mabwana. Waombe watumie lugha yetu ya Kiswahili. Hii lugha haina mapungufu yoyote. Ni lugha nzuri. Ni lugha ya maendeleo. Ni lugha inayotumiwa na walalanjaa ambao hip hop summit inataka kuwasaidia. Msaada wao uanze kwenye fikra zetu. Watusaidie tujue kuwa uhai wa taifa uko kwenye utamaduni na historia yake. Tafadhali fanya hivi. TUJIKOMBOE!

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com