8/26/2004

MAMBO YA NYAKATI

Mazungumzo hapo chini yalikuwa yanafanywa na jamaa wawili katika bustani iliyoko nyuma ya kanisa la Kilutheri la mzunguko la Magomeni, jijini Dar Es Salaam, 2001. Nimetoa kwenye mkusanyiko wa mazungumzo, visa, na kejeli za mtaani "Mambo Ya Nyakati." Mkusanyiko huu nimekuwa nikiufanya muda mrefu kwa kalamu na rekoda.
*************************************************************************************


“Usimwone hivi jamaa yule.”
“Kwani vipi? Si chizi yule?”
“Kafika chuo kikuu.”
“Chuo kikuu kaenda lini kila siku yuko mtaani?”
“Hawa ndio wale waliofukuzwa na Mwinyi.”
“Mwinyi aliwaonyesha dawa yao. Ile mijinafunzi ya jabu sana. Walitaka serikali iwape hela hadi za sigara!”
“Sasa walipofukuzwa waliambiwa waandike barua za kuomba msamaha. Jamaa unayemwita chizi akakataa.”
“Mbishi huyo. Nenda kacheze naye drafti pale dukani kwa Mangi…hakubali kushindwa. Kila jioni hakosi taarifa za BBC. Akitoka hapo ni kubishana mambo ya siasa mtaa mzima.”
“Sio siasa tu. Usimuone vile, Kurani imefika na Kiingereza ndio usiseme. Anashusha aya kwa Kiarabu kama vile kaandika Kurani yeye.”
“Kujua Kiarabu na Kiingereza au kukariri Kurani huku huna kitu mfukoni ndio nini sasa? Anaishi kwa nyanya yake hadi leo. Unavyomuona pale kazi hana.”
“Tatizo lake watu wanadai ni laana. Eti kaachiwa radhi na wazazi.”


0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com