1/21/2005

RUMI JUU YA MAANA YA MAISHA NA KIFO

Watu wengi wanahofu kifo sana. Ingawa lazima kila mmoja wetu atafariki. Moja ya sababu kubwa ya kuhofia kifo tunaambiwa na wanasaikolojia ni kuwa hatujui tuendako. Tuna hofu ya tusikokujua. Tukifa tunakwenda wapi? Mbinguni, jehanamu, kuzimu, kusikojulikana, sayari ya mbali, mbingu ya saba, hatuendi kokote...
Imani nyingi duniani zimekuwa na mtazamo kuwa ukifa unazaliwa tena. Hii inaitwa Reincarnation. Maisha ni mzunguko kama wa jua. Kukicha jua linafufuka. Kukichwa jua linazama. Linafariki. Mzunguko wa maisha (kufa na kurudi).
Kuna wengine kama wafuasi wa Gautama Buddha (waumini wa Kibudha) wana imani kama hii lakini kuna tofauti fulani. Badala ya Reincarnation wanapendelea Rebirth.
Dr. Remmy Ongala kaimba sana juu ya kifo. Katika wimbo mmoja anauliza, "Kwanini nife?" Hili ni swali moja kati ya maswali makubwa mawili yanayomsumbua mwanadamu juu ya kifo. Jingine ni siku ya kufa. Hakuna ajuaye. Kuna wanaodai kuwa kila mmoja wetu kapangiwa siku yake ya kufa na Mungu. Wenye hoja hii inakuwa kama vile wanasema kuwa Mungu ndiye anatuua. Je mtu akifariki kwa kugongwa na mlevi ni Mungu kapanga? Mlevi kasaidia mpango wa Mungu? Au labda Mungu anapanga siku ila hapangi kifo kitakukuta vipi.

Dr. Ongala katika wimbo mwingine anasema siku ya kufa ni siku ya udongo. Lakini kuna wengine hawaendi udongoni. Wanachomwa moto. Hii inaitwa cremation. Wanahistoria wanatuambia kuwa hapo zamani kabla jamii nyingi hazijawa na makazi ya kudumu na wakati huo wakiona kuwa moto una nguvu fulani za kiroho, uchomaji wa marehemu ulikuwa ulifanyika. Kitendo cha mwili kuchomwa moto kilionekana kama ni mwili kuliwa na roho kuu ya moto. Tendo hili liliaminiwa kuwa lilimsaidia marehemu.


Ninachotaka hasa kukwambia ni hiki: Ukiamka asubuhi unatakiwa kukumbuka jambo moja. Kumbuka kuwa umepunguza siku moja katika maisha yako. Yaani umekaribia ile siku unayoiogopa kwa siku moja! Inatisha, eeh?

Mmoja wa washairi niwapendao mno, Jelaluddin Rumi, alipokuwa akifikiria suala hili la kifo na hasa lile swali la siku ya kufa na akifa atakwenda wapi aliandika maneno haya:

Siku nzima ninaliwaza,
kisha usiku ninalisema.
Ninatoka wapi ?
Ninapaswa kufanya nini hapa duniani ?
Sijui.

Nafsi yangu imetoka mbali na hapa,
hilo nina uhakika nalo...
Sikuja hapa kwa amri yangu.
Na siwezi kuondoka kwa amri yangu.
Yeyote aliyenileta hapa anapaswa kunichukua nyumbani...

0 Maoni Yako:

Post a Comment

<< Home

FREE hit counter and Internet traffic statistics from freestats.com